• HABARI MPYA

    Monday, May 20, 2019

    SAMATTA AKABIDHIWA TUZO ZAKE NA KOMBE LA UBINGWA WA LIGI YA UBELGIJI GENK

    Na Mwandishi Wetu, GENK
    MSHAMBULIAJI wa kimataifa wa Tanzania, Mbwana Ally Samatta jana amekabidhiwa tuzo zake na kuvishwa Medali ya ubingwa wa Ligi Daraja la Kwanza A Ubelgiji, maarufu kama Jupiler Pro League baada ya sare ya 0-0 na Standard Liege kwenye mchezo wa mwisho wa msimu Uwanja wa Luminus Arena.
    Kwa matokeo hayo, KRC Genk inamaliza msimu na pointi 52, mbili zaidi ya Club Brugge iliyoshika nafasi ya pili na zote mbili zitacheza Ligi ya Mabingwa Ulaya msimu ujao. 
    Samatta alikuwepo uwanjani kwa dakika zote 90 na baada ya mechi hiyo sherehe za ubingwa zikafuatia, wachezaji wa Genk wakikabidhiwa Medali za Dhahabu na Kombe lao kubwa.
    Mbwana Samatta baada ya kukabidhiwa tuzo zake jana kufuatia sare ya 0-0 na Standard Liege kwenye mchezo wa mwisho wa msimu Uwanja wa Luminus Arena. 
    Mbwana Samatta akifurahia Kombe la ubingwa wa Ubelgiji na wachezaji wenzake jana Uwanja wa Luminus Arena
    Mbwana Samatta akipambana na wachezaji wa Standard Liege jana Uwanja wa Luminus Arena.  
    Mbwana Samatta akifurahia na wachezaji wenzake wa KRC Genk baada ya kukabidhiwa Medali na Kombe lao Uwanja wa Luminus Arena 

    Samatta akapewa tuzo yake Mwanasoka Bora Mwafrika anayecheza Jupiler Pro League baada ya kumaliza na mabao 23 msimu huu hivyo kuongoza.
    Kwa ujumla, Samatta mwenye umri wa miaka 26, ameifungia Genk mabao 62 katika mechi 156 za mashindano yote tangu amejiunga nayo Januari mwaka 2016 akitokea TP Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC).
    Katika ligi ya Ubelgiji pekee amefunga mabao 47 katika mechi 123, kwenye Kombe la Ubelgiji amefunga mabao mawili katika mechi tisa na Europa League amefunga mabao 14 katika mechi 24.
    Kikosi cha KRC Genk kilikuwa; Jackers, Seigers, Aidoo, Dewaest, De Norre, Heynen/Piotrowski dk75, Wouters, Samatta, Paintsil, Trossard/Ndongala dk56 na Gano/Ingvartsen dk68.
    Standard Liege; Ochoa, Fai, Kosanovic, Laifis, Pocognoli, Cimirot/Halilovic dk35, Marin, Bastien/Emond dk81, Lestienne/Carcela dk68, Mpoku na Oulare.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SAMATTA AKABIDHIWA TUZO ZAKE NA KOMBE LA UBINGWA WA LIGI YA UBELGIJI GENK Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top