• HABARI MPYA

    Tuesday, March 19, 2013

    SAMATA, ULIMWENGU WARIPOTI STARS

    Samatta kulia na Ulimwengu kushoto; Vijana wamekuja kufanya kazi ya nchi

    Na Boniface Wambura
    WASHAMBULIAJI wa Taifa Stars, Mbwana Samatta na Thomas Ulimwengu wanaochezea klabu ya TP Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo (DRC), wamewasili nchini jana usiku na kwenda moja kwa moja kambini.
    Ujio wa washambuliaji hao unafanya idadi ya wachezaji walioripoti kambini kufikia 20 kati ya 23 walioitwaa baada ya mshambuliaji Khamis Mcha aliyekuwa na kikosi cha timu yake ya Azam nchini Liberia naye kuripoti kambini leo asubuhi.
    Wachezaji John Bocco na makipa Mwadini Ally na Aishi Manula ambao pia nao walikuwa Liberia na timu yao ya Azam wataripoti kambini leo alasiri. Wachezaji hao ni sehemu ya msafara wa timu ya Azam ambao utakuja na ndege ya mchana kutokea Nairobi kwa vile ile ya asubuhi waliyotangulia nayo wenzao kuwa imejaa.
    Taifa Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager ikiwa chini ya Kocha Kim Poulsen leo inaendelea na mazoezi Uwanja wa Taifa. Mazoezi hayo yataanza saa 9 alasiri.
    Wakati huo huo: Mwamuzi Msaidizi wa zamani wa kimataifa wa Tanzania, Leslie Liunda ameteuliwa kuwa mtathimini wa waamuzi (referee assessor) kwenye moja ya mechi za mchujo za Kombe la Dunia.
    Shirikisho la Soka la Kimataifa (FIFA) limemteua Liunda kutathimini waamuzi kwenye mechi kati ya Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo (DRC) na Libya itakayochezwa Jumapili (Machi 24 mwaka huu).
    Mechi hiyo itafanyika kwenye Uwanja wa Martyrs jijini Kinshasa kuanzia saa 9.30 alasiri kwa saa za Afrika ya Kati (CAT).
    Waamuzi watakaochezea mechi hiyo William Selorm Agbovi atakayekuwa mwamuzi wa kati, Malik Alidu Salifu (mwamuzi msaidizi namba moja), David Laryea (mwamuzi msaidizi namba mbili) na mwamuzi wa mezani (fourth official) Cecil Amatey Fleischer. Waamuzi wote hao wanatoka Ghana.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments
    Item Reviewed: SAMATA, ULIMWENGU WARIPOTI STARS Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top