• HABARI MPYA

    Tuesday, June 23, 2015

    NOOIJ AAGA MBELE YA WAANDISHI WA HABARI NA KUSEMA; “NITAWAKUMBUKA WATANZANIA”

    Na Baraka Kizuguto, DAR ES SALAAM
    ALIYEKUWA kocha wa Taifa Stars, Mholanzi Mart Nooij amesema ataikumbuka Tanzania baada ya kipindi cha takriban mwaka mmoja cha kufanya kazi.
    Akizungumza na Waandishi wa Habari wakati wa kuagwa leo hoteli ya Tansoma eneo la Gerezani, Dar es Salaam, Nooij amesema anawashukuru Watanzania wote, Serikali, wadau wa mpira wa miguu nchini na TFF kwa sapoti waliyompatia wakati akiwa kocha mkuu wa timu ya Taifa.
    Nooij alisema alifurahia maisha yake akiwa Tanzania kwa kipindi chote alichokua akifundisha timu ya Taifa, lakini kwa sababu imefikia mwisho wa ajira yake hana jinsi anaondoka, lakini ataendelea kuikumbuka Tanzania na watanzania wote kila siku kwa ukarimu wao.
    Ilibidi Mart Nooij atolewe nje kwa msaada wa Polisi Jumamosi usiku Uwanja wa Amaan, Zanzibar

    Mapema Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Jamal Malinzi alisema wameamua kuagana nae mbele ya vyombo ya habari kama iliyofanyika pia wakati wa utambulisho wake wakati wa kuanza kazi.
    “Mpira wa miguu unachangamoto nyingi, Watanzania tuna safari ndefu katika mafanikio ndio maana  TFF imeanza kuwekeza katika soka la vijana, sababu ndio msingi wa kuwa na timu bora ya Taifa” alisema Malinzi.
    Duniani kote chimbuko la timu bora ni soka la vijana na watoto, tukiwa na vijana wengi walioanza kucheza mpira katika umri mdogo wanapofikia umri wa kuchezea timu ya Taifa tutakua na kikosi bora.
    Nchi za wenzetu inapofikia kocha kuita wachezaji wa timu ya Taifa anakuwa na wigo mpana, kwetu sisi wachezaji wanocheza soka nje ya nchi wanahesabika, hivyo ni lazima tuanze kuwekeza kwenye soka la vijana
    TFF ilishaanza mkakati huo ndio maana kuna timu za U13, U15 ambazo zitakua zikiingia kambini na kucheza michezo ya kirafiki ndani ya nje kwa lengo la kupata uzoefu kabla ya kushiriki kuwania kufuzu kwa fainali za vijana mwaka 2016.
    Kikosi cha U15 kinatarajiwa kufanya ziara mwezi Disemba mwaka huu katika nchi za Malawi, Zambia, Zimbambwe, Botswana na Afrika Kusini, kisha mwakani mwezi April 2016 kitaenda Rwanda, Burundi, Uganda na Kenya kucheza michezo ya kirafiki.
    Mchezo wa Jumamosi ulikuwa wa tano mfululizo, Taifa Stars inafungwa chini ya Nooij aliyerithi mikoba ya Mdenmark Kim Poulsen Aprili mwaka jana na kwa ujumla timu hiyo imecheza mechi tisa bila ya ushindi chini ya Mholanzi huyo. 
    Kwa ujumla, Nooij ameiongoza Stars katka mechi 18 tangu arithi mikoba ya Mdenmark, Kim Poulsen Aprili mwaka jana, kati ya hizo ameshinda tatu tu, sare sita na kufungwa tisa- akifunga mabao 17 na kufungwa 28.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: NOOIJ AAGA MBELE YA WAANDISHI WA HABARI NA KUSEMA; “NITAWAKUMBUKA WATANZANIA” Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top