• HABARI MPYA

    Saturday, February 21, 2015

    ‘MIKADI’ YAMPONZA MBUYU TWITE YANGA

    Na Prince Akbar, MBEYA
    YANGA SC itamkosa beki wake mahiri mwenye uwezo wa kucheza nafasi za kiungo pia, Mbuyu Twite katika mchezo wa kesho wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara dhidi ya wenyeji Mbeya City, Uwanja wa Sokoine Mbeya.
    Mchezaji huyo mwenye uwezo wa kucheza nafasi zote za ulinzi na kiungo, alipewa kadi ya tatu ya njano Alhamisi wiki hii, Yanga SC ikiifunga mabao 3-0 Prisons katika mfululizo wa ligi hiyo.
    Hakuna shaka, pengo lake katika beki ya kulia litazibwa na Juma Abdul katika nafasi ya kiungo wa ulinzi ataanzishwa Salum Abdul Telela ‘Master’. Hata hivyo, kitu kimoja Yanga SC watakosa kesho pamoja na ‘upambanaji’ wa Mbuyu Twite uwanjani, pia ni urushaji wa mipira kama amepiga kwa mguu, jambo ambalo mara kadhaa limekuwa likiisaidia timu hiyo kupata mabao.
    Mbuyu Twite kushoto ataukosa mchezo wa Yanga dhidi ya Mbeya City Jumapili kwa sababu ya kadi tatu za njano 

    Pamoja na ukweli huo, kocha Mholanzi wa timu hiyo, Hans van der Pluijm amesema kwamba Mbuyu Twite atakosekana, lakini Yanga SC itaendelea kuwa ile ile ya ushindi mjini Mbeya.
    “Ni mchezaji wetu muhimu, kweli. Lakini si tatizo kubwa kwa sababu wapo wa kucheza badala yake,”alisema babu huyo wa Kiholanzi.
    Beki wa kushoto chipukizi, Edward Charles aliyeumia kifundo cha mguu wiki iliyopita Yanga SC ikiifunga 2-0 Mtibwa Sugar Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam naye ataendelea kukosekana kesho.
    Yanga SC inahitaji pointi tatu katika mchezo wa kesho mjini Mbeya ili kujiweka katika nafasi nzuri ya kurejesha taji lao la ubingwa wa Ligi Kuu walilopokonywa na Azam FC msimu uliopita.  
    Yanga SC inaongoza mbio za ubingwa wa Ligi Kuu kwa pointi zake 28 baada ya kucheza mechi 14, sawa na mabingwa watetezi, Azam FC wenye pointi 26. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: ‘MIKADI’ YAMPONZA MBUYU TWITE YANGA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top