• HABARI MPYA

    Saturday, February 21, 2015

    MAHAKAMA NAYO YAAMRISHA HAKUNA MPIRA KENYA; HUJUMAAAA!!!

    Na Vincent Malouda, NAIROBI
    HAKUNA ligi kuu itapigwa Kenya kwa siku kumi na nne zijazo kuanzia Ijumaa ya tahere 20 Februari kwa mujibu wa hakimu mkuu katika mahakama ya Milimani, jijini Nairobi Bw. Mbogholi Msagha.
    Katika amri ya mahakama iliyotumwa kwenye vyombo vya habari alasiri ya leo, mahakama hiyo imesisitiza kuwa mlengwa au mhusika ametahadharishwa kuandaa, kuanza au kusimamia ligi isiyo rasmi kwa jina ligi kuu ya taifa la Kenya, KPL, hadi kesi hiyo itakaposikizwa tarehe 3 Machi 2015.
    Amri hiyo ya mahakama imemtaja mwenyekiti wa Shirikisho la Soka la Kenya, FKF, Sam Nyamweya kama mlalamishi aliesalimisha ombi lake la dharura leo hii.

    Hili ni pigo kwa kampuni inayosimamia ligi kuu, KPL, ambayo baada ya kutoafikiana na shirikisho kuhusu jumla ya timu katika ligi kuu msimu huu, iliahidi kung’oa nanga ligi yao hapo kesho japo wamepinga kupokezwa barua hiyo.

    “Hatujapata amri yoyote kutoka kwa mahakama, habari hizi pia sisi twazisikiza tu kupitia vyombo vya habari hivyo ligi itaanza ilivyoratibiwa hapo kesho,” afisa mkuu mtendaji wa KPL, Jack Oguda alisema.
    FKF na KPL  ziliapa kuendelea na ligi zao tofauti kumaanisha taifa la Kenya lingeshuhudia ligi kuu mbili; ya FKF yenye timu 18 huku ya KPL ikizishirikisha timu 16.
    Jumla ya mechi nne zilikuwa zimeratibiwa kupenua pazia la ligi kuu siku ya jumamosi. Thika United ikiwa nyumbani dhidi ya Tusker FC, KCB iwaalike Western Stima ugani City katika mechi ya awali huku Gor Mahia ikikanyagana na Mathare United katika mechi ya pili uwanjani humo.
    Kwingineko, wanajeshi Ulinzi Stars watakuwa wenyeji wa SoNy Sugar katika uchanjaa wa Afraha mjini Nakuru.
    Siku ya jumapili, Chemelil Sugar dhidi ya AFC Leopards (Afraha), Sofapaka kupambana na Ushuru FC yake mtanzania David Naftali Tevelu mjini Machakos huku Bandari ikimwalika Muhoroni Youth Mombasa.
    Iwapo vilabu vitaziba masikio ya amri ya mahakama na kucheza mechi hizo, tungali kuona.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MAHAKAMA NAYO YAAMRISHA HAKUNA MPIRA KENYA; HUJUMAAAA!!! Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top