• HABARI MPYA

    Wednesday, December 09, 2020

    CHAMA ATOKEA BENCHI NA KUIFUNGIA SIMBA SC MABAO YOTE IKIICHAPA POLISI TANZANIA 2-0 DAR

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    MABINGWA watetezi, Simba SC usiku wa leo wameiadhibu Polisi Tanzania ya Kilimanjaro kwa mabao 2-0 katika mchezo wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara Uwanja wa Benjamin Mkapa Jijini Dar es Salaam.
    Kwa ushindi huo, Simba SC inayofundishwa na Mbelgiji Sven Ludwig Vandenbroeck inafikisha pointi 26 baada ya kucheza mechi 12, ingawa inabaki nafasi ya tatu sasa ikizidiwa pointi moja tu na Azam FC ambayo hata imecheza mechi mbili zaidi.
    Vigogo, Yanga SC ndio wanaoongoza Ligi Kuu ya Tanzania Bara kwa pointi zao 34 walizovuna kwenye michezo 14 hadi sasa.

    Katika mechi ya leo iliyochezeshwa na refa Ahmed Aragija aliyekuwa anasaidiwa na Leonard Mkumbo wote wa Manyara na Martin Mwalyaje wa Tabora, Simba SC walilazimika kusubiri hadi dakika 30 za mwisho kupata pointi hizo tatu na pongezi kwa kiungo Mzambia Clatous Chotta Chama aliyefunga mabao yote hayo.
    Na Chama, mchezaji wa zamani wa Nchanga Rangers, ZESCO United, Lusaka Dynamos za kwao Zambia na Al Ittihad ya Misri alifunga mabao hayo baada ya kutokea benchi dakika ya 62 akichukua nafasi ya winga Mghana, Bernard Morrison. 
    Alifunga bao la kwanza dakika ya 63 akimalizia pasi ya mtokea benchi mwenzake, Nahodha wa timu, mshambuliaji John Raphael Bocco na p[ili dakika ya 89 akimalizia pasi ya kiungo mwenzake, Said Hamisi Ndemla.
    Mechi nyingine ya Ligi Kuu leo, wenyeji Namungo FC walilazimishwa sare ya bila kufungana na Biashara United ya Mara Uwanja wa Majaliwa, Ruangwa mkoani Lindi.
    Kikosi cha Simba SC kilikuwa; Aishi Manula, Joash Onyango, Gardiel Michael, Ibrahim Ame, Pascal Wawa, Muzamil Yassin/Erasto Nyoni dk84, Luis Miquissone, Said Ndemla, Meddie Kagere, Francis Kahata/John Bocco dk62 na Bernard Morrison/Clatous Chama dk62.
    Polisi Tanzania; Msafiri Mkumbo, Datus Peter, Juma Ramadhani, Iddi Mobby, Mohammed Kassim, Pato Ngonyani, Pius Buswita/Daruwesh Saliboko dk76, Hassan Nassor, George Mpole/Rashid Juma dk71, Marcel Kaheza/Deusdedit Cossmas dk53 na Tariq Seif.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: CHAMA ATOKEA BENCHI NA KUIFUNGIA SIMBA SC MABAO YOTE IKIICHAPA POLISI TANZANIA 2-0 DAR Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top