• HABARI MPYA

    Thursday, July 19, 2018

    AZAM FC YATAKA KUMREJESHA KIPRE TCHETCHE…YUSSUF BAKHRESA ATUA MALAYSIA KUMALIZA KAZI

    Na Mahmoud Zubeiry, DAR ES SALAAM
    AZAM FC imeanza mchakato wa kumrejesha mshambuliaji wake wa zamani, Muivory Coast Kipre Herman Tchetche ambaye kwa sasa anachezea Terengganu FC ya Ligi Kuu ya Malaysia.
    Mkurugenzi wa Azam FC, Yussuf Bakhresa yupo nchini Malaysia kwa mipango ya uhamisho ya mchezaji huyo mwenye nguvu na kasi uwanjani.
    Akizungumza na Bin Zubeiry Sports – Online leo kwa simu kutoka Malaysia, Bakhresa amesema kwamba yuko katika mazungumzo na Terengganu FC juu ya kumrejesha Tanzania Tchetche.

    Azam FC inataka kumrejesha mshambuliaji wake wa zamani, Muivory Coast Kipre Herman Tchetche ambaye


    “Kipre Tchetche amebakiza miezi mitatu katika mkataba wake na hii timu na kiungwana nipo katika mazungumzo na klabu yake waturudishie mchezaji wetu,”amesema Bakhresa.  
    Tchetche aliondoka Azam FC mwaka 2016 baada ya kucheza tangu mwaka 2011 alipojiunga nayo akitokea Jeunesse Club ya Abidjan, nyumbani kwao, Ivory Coast.
    Na Azam FC ilipendezewa na Kipre Tchetche pamoja na pacha wake, Kipre Michael Balou walipokuja na kikosi cha pili cha timu ya taifa ya Ivory Coast kwenye michuano ya CECAFA Challenge mwaka 2010 nchini Tanzania na kuwasajili wote kabla ya wote kuondoka kuhamia Oman. Kipre alichezea Al-Suwaiq nchini Oman wakati Balou bado yupo Fanja SC.
    Baada ya misimu miwili ya kufanya vibaya, Azam FC imedhamiria kujiumba upya na kuwa tishio tena katika soka ya Tanzania.
    Imeanza kwa kuunda kikosi imara na kuajiri makocha wapya, Mholanzi Hans van der Pluijm na Msaidizi wake, Juma Mwambusi ambao walifanya kazi kwa pamoja kwa mafanikio Yanga SC.
    Na mapema tu Azam FC imeanza kuvuna matunda ya uwekezaji huo mpya, baada ya kutwaa taji la Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati, Kombe la Kagame mapema mwezi huu, ikiifunga Simba SC 2-1 katika fainali mjini Dar es Salaam. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: AZAM FC YATAKA KUMREJESHA KIPRE TCHETCHE…YUSSUF BAKHRESA ATUA MALAYSIA KUMALIZA KAZI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top