• HABARI MPYA

    Thursday, July 19, 2018

    ZAHERA ATAJA SABABU ZA YANGA KUPEWA KIPIGO CHA ‘MBWA KOKO’ JANA NAIROBI

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    KOCHA Mkongo wa Yanga SC, Mwinyi Zahera amesema kwamba kipigo cha mabao 4-0 kutoka kwa wenyeji, Gor Mahia katika mchezo wa Kundi D Kombe la Shirikisho Afrika usiku wa jana Uwanja wa Moi Kasarani mjini Nairobi kimetokana na wachezaji kutokuwa fiti.
    Katika video iliyosambazwa na klabu ya Yanga leo, Zahera anaonekana akizungumza baada ya kikosi kuwasili Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) mjini Dar es Salaam akisema kwamba kuna wachezaji walisafiri na timu bila kufanya mazoezi kwa muda mrefu.
    Zahera amesema wengine walijiunga na timu siku nne kabla ya mchezo huo wa ugenini na kwa ujumla Zahera amesema Yanga haikuwa tayari kwa mchezo huo, bali ililazimika kucheza.

    Mwinyi Zahera amesema wachezaji wa Yanga hawakuwa fiti ndiyo maana wakafungwa 4-0 na Gor Mahia jana

    Yanga SC iliendelea kuvurunda jana ikikamalisha mechi tatu za mzunguko wa kwanza bila ushindi, ikifungwa mbili zote 4-0, ya kwanza dhidi ya MC Alger nchini Algeria Mei 6 na sare ya 0-0 na Rayon Sport mjini Dar es Salaam Mei 16. 
    Katika mchezo huo uliochezeshwa na marefa kutoka Somalia ambao ni Hassan Mohamed Hagi aliyepuliza kipyenga akisaidiwa na Hamza Hagi Abdi na Bashir Sh. Abdi Suleiman, hadi mapumziko tayari Yanga walikuwa wamekwishachapwa 2-0.
    Alianza mshambuliaji wa kimataifa wa Rwanda, Jacques Tuyisenge kutumia makosa ya safu mbofu ya ulinzi ya Yanga kuwahi kutokea miaka karibuni kufunga bao la kwanza dakika ya 21 akimalizia krosi ya Samuel Onyango.
    Mshambuliaji Muivory Coast, Ephrem Guikan akamalizika pasi ya kiungo Mkenya, Francis Kahata kuifungia Gor Mahia bao la pili dakika ya 44. 
    Beki wa pembeni, Mwinyi Hajji Mngwali aliyekuwa anacheza kiungo leo akajifunga dakika ya 65 katika harakati za kuokoa kabla ya Guikan kukamilisha shangwe za mabao Gor Mahia dakika ya 86.
    Yanga wataikaribisha Gor Mahia Julai 29 Uwanja wa Taifa mjini Dar es Salaam kwa mchezo wa marudiano kabla ya kurudiana na USM Alger Agosti 19 na kwenda kukamilisha mechi zake za kundi hilo kwa kumenyana na wenyeji, Rayon Sport Agosti 28.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: ZAHERA ATAJA SABABU ZA YANGA KUPEWA KIPIGO CHA ‘MBWA KOKO’ JANA NAIROBI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top