KOCHA wa Chelsea, Jose Mourinho ameingilia sakata la mshambuliaji Raheem Sterling kugoma kuongeza Mkataba Liverpool kwa kusema anaweza kumuuza mchezaji yeyote anayetaka kuondoka klabu yake.
Uwezekano wa Sterling kuendelea kuchezea Liverpool ni mdogo baada ya mshambuliaji huyo kusema katika mahojiano na Televisheni Jumatano kwamba aligoma kusaini Mkataba mpya.
Mshambuliaji huyo chipukizi wa kimataifa wa England aliyepewa nyongeza ya mshahara kwa zaidi ya nusu hadi Pauni 100,000 katika Mkataba huo mpya, amesema kiu yake si fedha bali mataji.
Inafahamika, Chelsea ni miongoni mwa timu zinazommezea mate mkali huyo mwenye umri wa miaka 20, nyingine zikiwa ni Arsenal na Manchester City, ingawa mwenyewe amesema anataka kucheza nje.
Raheem Sterling, pichani Alhamisi akiwa mazoezini na Liverpool
Jose Mourinho amesema anaweza kumuuza mchezaji yeyote anayetaka kuondoka katika klabu yake
Kocha wa Liverpool, Brendan Rodgers atamuanzisha Sterling leo katika mechi ya Ligi Kuu ya England dhidi ya Arsenal, licha ya mchezaji huyo kusema anapagawishwa na kutakiwa na klabu hiyo ya Kaskazini mwa London.
Rodgers amesistiza Sterling hatauzwa mwishoni mwa msimu kwa bei yoyote, licha ya kugoma kusaini Mkataba mpya.
Lakini Mourinho amesema: "Sipendi wachezaji ambao hawataki kuchezea timu yangu. Maoni yangu ni kila mchezaji ana bei. Haijalishi ni mchezaji gani. Ukiniuliza mimi kwa mfano, ninataka kumuuza Eden Hazard aondoke Chelsea? Hapana. Ikiwa anataka kuondoka na hataki kufanya kazi na mimi, hataki kuchezea Chelsea, ana bei? Nafikiri anayo,".
"Lakini pia ninafahamu falsafa za makocha na klabu ambao wanataka kuwabakiza wachezaji kwa gharama zozote. Falsafa yangu si nzuri zaidi ya zao, hiyo ni yangu," amesema Mourinho.


.png)
0 comments:
Post a Comment