• HABARI MPYA

    Monday, January 27, 2014

    BIN SLUM AIWEKEA ‘NADHIRI YA KIFO’ YANGA SC MBELE YA COASTAL MKWAKWANI JUMATANO

    Na Mahmoud Zubeiry, Dar es Salaam
    MKURUGENZI wa Ufundi wa Coastal Union ya Tanga, Nassor Bin Slum amesema Yanga SC itakiona cha moto kwa timu yake keshokutwa katika mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, Uwanja wa Mkwakwani, Tanga.
    Akizungumza na BIN ZUBEIRY leo, Bin Slum amesema kwamba vijana wake wapo vizuri kuelekea mchezo huo na hakuna shaka Yanga itaacha pointi zote tatu Uwanja wa Mkwakwani Jumatano.
    “Tunakubali msimu huu tumeshindwa kutimiza malengo yetu, siyo kwenye ubingwa tu, bali hata nafasi za nne za juu. Malengo yetu ya sasa ni kumaliza nafasi ya tano,”alisema Bin Slum.
    Nassor Bin Slum katika picha tofauti, amesema Yanga watakiona cha moto kwa Coastal Jumatano

    Amesema ili wafanikiwe kumaliza katika nafasi hiyo, lazima wafanye vizuri katika mechi zilizobaki za Ligi Kuu na hawatakubali kuwa ngazi za timu nyingine kuelekea kwenye ubingwa.
    “Coastal Union hatutakubali kamwe kufanywa daraja la timu nyingine zenye kutaka ubingwa, na anayetaka kuamini haya Jumatano tunacheza na Yanga, mtawaonea huruma,”alisema.
    Coastal Union na Yanga SC ndizo timu pekee za Ligi Kuu zilizoweka kambi nje ya nchi kujiandaa na mzunguko wa pili wa ligi hiyo. 
    Wakati Yanga walikuwa Uturuki ambako walicheza mechi nne za kirafiki na kushinda mbili na kutoa sare mbili, Coastal walikuwa Oman ambako walicheza mechi nne pia na kushinda mbili, sare moja na kufungwa moja.   
    Katika mechi zao za ufunguzi za mzunguko wa pili Jumamosi, Yanga ilianza vyema kwa kuifunga Ashanti United mabao 2-1 Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, wakati Coastal ililazimishwa sare ya kufungana bao 1-1 na JKT Oljoro Mkwakwani.
    Yanga SC ambao ndio mabingwa watetezi wa Ligi Kuu, wapo kileleni mwa ligi hiyo kwa pointi zao 31, baada ya kucheza mechi 14, wakifuatiwa na Azam FC na Mbeya City zenye pointi 30 kila moja, wakati Coastal ni ya nane kwa pointi zake 17 baada ya mechi 14 pia.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: BIN SLUM AIWEKEA ‘NADHIRI YA KIFO’ YANGA SC MBELE YA COASTAL MKWAKWANI JUMATANO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top