• HABARI MPYA

    Wednesday, October 23, 2013

    YANGA SC YAFUFUA MATUMAINI YA UBINGWA LIGI KUU BAADA YA KUBOMOA KIKOSI

    Na Prince Akbar, Dar es Salaam
    YANGA SC imefufua matumaini ya kutetea ubingwa wake, baada ya kuibuka na ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya Rhino Rangers ya Tabora hii leo katika mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
    Matokeo hayo yanawafanya mabingwa hao watetezi watimize pointi 19, baada ya kucheza 10, ingawa wanaendelea kubaki nafasi ya nne, nyuma ya Simba SC, Azam na Mbeya City, ambazo kila moja ina pointi 20.
    Kocha Mholanzi, Ernie Brandts leo alifanya mabadiliko makubwa katika kikosi chake cha kwanza kutoka kile kilicholazimishwa sare ya 3-3 na Simba SC Jumapili kikitoka kuongoza 3-0 hadi mapumziko.   
    Mfungaji wa mabao mawili ya Yanga SC leo, Hamisi Kiiza kulia akishangilia na wenzake Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam leo 

    Deo Munishi ‘Dida’ alichukua nafasi ya Ally Mustafa ‘Barthez’ langoni, Juma Abdul akacheza beki ya kulia nafasi ya Mbuyu Twite aliyehamia kwa Nadir Haroub ‘Cannavaro’ katikati, Rajab Zahir akachukua nafasi ya Athumani Iddi ‘Chuji’ katika kiungo cha chini na Simon Msuva akacheza wingi ya kulia badala ya Mrisho Ngassa aliyechukua nafasi ya Didier Kavumbangu mbele.
    Hadi mapumziko, Yanga walikuwa mbele kwa bao 1-0 lililofungwa na Hamisi Kiiza dakika ya 12 na kipindi cha pili, Frank Domayo akafunga la pili dakika ya 73 kabla ya Diego wa Kampala, Kiiza kufunga la tatu dakika ya 81.
    Yanga SC leo ilicheza vizuri na kwa nidhamu ya hali ya juu, ikikwepa kurudia makosa iliyoyafanya katika mchezo dhidi ya Simba SC Jumapili.
    Yanga SC; Deo Munishi ‘Dida’, Juma Abdul, David Luhende/Oscar Joshua, Mbuyu Twite, Kevin Yondan, Rajab Zahir, Simon Msuva/Nizar Khalfan dk60, Frank Domayo, Hamisi Kiiza, Mrisho Ngassa na Haruna Niyonzima.
    Rhino Rangers; Mahmoud Othman, Ally Mwanyiro, Hussein Abdallah, Julius Masoga, Ladislaus Mbogo, Stanslaus Mwakitosi, Shijja Mongo, Imani Noel/Msafiri Hamisi dk52, Victor Hangaya/Kamana Salum dk60, Saad Kipanga na Nurdin Bakari. 
    Katika mechi nyingine za leo, Simba SC imetoka sare ya bila kufungana na Coastal Union Uwanja wa Mkwakwani, Tanga, Prisons imetoka sare ya 1-1 na Kagera Sugar Uwanja wa Sokoine mjini Mbeya. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: YANGA SC YAFUFUA MATUMAINI YA UBINGWA LIGI KUU BAADA YA KUBOMOA KIKOSI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top