• HABARI MPYA

    Thursday, October 31, 2013

    BRANDTS AKALIA KUTI KAVU YANGA SC

    Na Mahmoud Zubeiry, Dar es Salaam
    UONGOZI wa Yanga SC unafuatilia mwenendo wa timu kwa ujumla na utendaji wa kocha wake, Mholanzi Ernstus ‘Ernie’ Wilhelmus Johannes Brandts kwa mechi zilizobaki za mzunguko wa kwanza na baada ya hapo itaamua kumuongeza Mkataba au kuachana naye mwalimu huyo.
    Brandts ametimiza mwaka mmoja wa Mkataba wake Yanga mwezi huu, lakini kuhusu Mkataba mpya ametakiwa kusubiri hadi mwisho wa mzunguko wa kwanza wa ligi mwezi ujao.
    Yanga SC hawajaonyesha wasiwasi juu ya uwezo wa Brandts katika kufundisha, lakini wanatilia shaka mambo matatu; sera zake, usimamiaji wake wa nidhamu ya wachezaji na kutokuwa na maamuzi ya haraka.
    Kuti kavu; Kocha wa Yanga SC anakabiliwa na changamoto kali kwa sasa

    Brandts analaumiwa kwa kitendo cha kuruhusu wachezaji wasikae kambini muda mrefu, akidai wachezaji si wafungwa wanatakiwa huru na mara nyingi Yanga imekuwa ikiingia kambini siku mbili kabla ya mechi.
    Kwa kuzingatia wapinzani wao wa jadi, Simba SC wako kambini muda wote Bamba Beach, Kigamboni, Dar es Salaam, Yanga nao wanaona hata kwao inawezekana, lakini Brandts amekuwa akikataa utaratibu huo.
    Yanga SC pia wana wasiwasi Brandts ameshindwa kusimamia vyema nidhamu ya wachezaji katika timu hiyo, jambo ambalo limesababisha baadhi yao viwango kushuka.
    Aidha, Brandts analaumiwa kutokuwa na maamuzi ya haraka hususan katika kubadilisha timu na wachezaji, mara anapoona aliowapa majukumu wanashindwa kuyakeleza ipasavyo na mambo hayo matatu ndiyo yanabeba mustakabali wake katika timu hiyo hivi sasa.
    “Aliona kabisa Barthez (Ally Mustafa) amemtumia muda mrefu, kachoka, lakini akashindwa kumpumzisha hadi akaja kuigharimu timu. Hata upangaji wake wa timu, namna anavyofanya subs (mabadiliko) ni mashaka matupu,”kilisema chanzo kutoka Yanga jana.
    Brandts alibadilisha karibu nusu ya kikosi chake cha kwanza baada ya sare ya 3-3 na Simba SC Oktoba 20, timu ikitoka kuongoza 3-0 hadi mapumziko na tangu hapo, Yanga imeshinda mabao matatu mechi mbili mfululizo bila kuruhusu nyavu zake kuguswa, langoni akisimama Deo Munishi ‘Dida’. 
    Tayari Yanga SC imeachwa hatua katika kadhaa katika mbio za ubingwa wa Ligi Kuu msimu huu, wakiwa wanazidiwa pointi moja na Azam FC na Mbeya City wanaokabana kileleni kwa pointi zao 23 kila timu. Azam ipo kileleni kwa wastani wake mzuri wa mabao.
    Yanga inatarajiwa kushuka tena dimbani kesho kumenyana na JKT Ruvu, Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, wakati leo wapinzani wao, Simba SC wanamenyana na Kagera Sugar kwenye Uwanja huo.
    Brandts, beki wa zamani wa kimataifa wa Uholanzi na klabu ya PSV Eindhoven ya Uholanzi, alirithi mikoba ya Mbelgiji Tom Saintfiet Oktoba mwaka jana, akitokea APR ya Rwanda aliyoifundisha tangu 2010.
    Mtaalamu huyo, aliyezaliwa Februari 3, mwaka 1956 mjini Nieuw-Dijk, Gelderland, mbali na PSV Eindhoven, awali alichezea klabu za Roda JC Kerkrade, MVV Maastricht na De Graafschap za kwao.
    Brandts aliichezea mechi 28 timu ya taifa ya Uholanzi na kuifungia mabao matano na pia alicheza Fainali za Kombe la Dunia mwaka 1978. 
    Katika fainali hizo, Raundi ya pili kwenye mechi na Italia, aliweka rekodi ya kuwa mchezaji pekee aliyezifungia mabao timu zote katika mechi moja kwenye fainali za Kombe la Dunia.
    Alianza kujifunga dakika ya 18, kisha akaisawazishia Uholanzi dakika ya 50 katika mechi ambayo, mchezaji mwenzake Arie Haan baadaye aliifungia timu yake bao la ushindi na kutoka kifua mbele kwa mabao 2–1.
    Alipostaafu soka akawa kocha na katikati ya msimu wa 2007–2008, Brandts aliambiwa hataongezewa mkataba NAC-Breda, licha ya matokeo mazuri ya kushika nafasi ya tatu katika Ligi Kuu Uholanzi (Eredivisie), ingawa uamuzi huo haukuwafurahisha mashabiki wa timu hiyo na nafasi yake akapewa Robert Maaskant kuanzia msimu wa 2008–2009.
    Akateuliwa kuwa Kocha wa Rah Ahan mwaka 2009, kabla ya kufukuzwa Desemba 2009 na kuibukia APR ya Rwanda mwaka 2010, ambako alifanya kazi hadi mwaka jana alipohamia Jangwani. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: BRANDTS AKALIA KUTI KAVU YANGA SC Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top