• HABARI MPYA

    Thursday, April 25, 2013

    MAKUBWA YAMKUTA ISHA MASHAUZI, 'ABAMBIKIZIWA' KESI YA WIZI

    Pole dada; Isha Mashauzi

    MKURUGENZI wa Mashauzi Classic, Isha Ramadhani ‘Mashauzi’ jana alionja adha ya umaarufu baada ya kusoteshwa kituo cha polisi cha Msimbazi huku kamera za waandishi maarufu zikimsubiri nje ya kituo hicho.
    Isha alifikishwa kituoni hapo kwa kuhusishwa na upotevu wa shilingi laki saba uliotokea kwenye duka moja la Kariakoo jijini Dar es Salaam.
    Mmiliki wa duka hilo la nywele, amemfikisha Isha na mwenzake aitwae Halima kituoni hapo akidai alipotelewa na kiasi hicho cha pesa huku msanii huyo akiwa ni wa mwisho kuingia dukani mwake.
    Saluti5 ilifika kituoni hapo majira ya 5 za usiku na kukuta waandishi wengi wakimsubiri Isha atoke ili wapate picha, jambo ambalo walifanikiwa licha ya Isha kujitahidi kuwakwepa.
    Inaaminika mmiliki wa duka hilo alipiga simu karibu kwa kila chombo cha habari ili waandishi wafike hapo akiamini kuwa jambo hilo litasaidia kumdhalilisha msanii huyo.
    Akiongea na Saluti5 muda mfupi baada ya kutoka kituoni hapo, Isha alisema alifika dukani kwa dada huyo Jumamosi iliyopita lakini baada ya kukosa alichokifuata aliingia duka lingine na kuliacha gari lake jirani na duka hilo.
    Wakati anarudi kwenye gari lake, wafanyakazi wawili wa duka hilo wakamfuta na kumwambia kuna upotevu wa pesa umetokea.
    Isha anasema baada ya mjadala wa muda mrefu  akaawachia namba ya simu na kuwaambia iwapo bado watahitaji ufafanuzi zaidi wawasiliane.
    Isha anasema: “Kuanzia Jumatatu alianza kunipigia simu za vitisho na kuniambia atanikomesha na kunidhalilisha.
    “Vitisho vilipokithiri, Jumanne jioni nikaenda kituo cha Msimbazi kuripoti juu ya vitisho vyake, lakini kituoni wakaninyima ushirikiano wakaniambia niende Kinondoni ninakoishi.
    “Nikawaambia nimekuja Msimbazi kwa vile biashara ya mtu anayenipa vitisho hivyo ipo Kariakoo, lakini bado walikataa kunihudumia.
    “Nilirudi nyumbani nikipanga kuwa kesho yake niende kituo cha Oysterbay lakini leo (jana) nikapigiwa simu kutoka Msimbazi kuwa nifike kituoni hapo.
    “Nikadhani labda sasa wameamua kunisikiliza, nilipofika kituoni hapo nikawekwa chini ya ulinzi kwa tuhuhuma za wizi wa shilingi laki 7.”
    Baada ya kusota kwa masaa kadhaa Isha aliruhusiwa lakini akitakiwa kurudi tena kituoni hapo siku inayofuata (le0).
    Watu kadhaa walifika kituoni hapo kumwekea dhamana Isha ambaye aligoma kabisa kuingizwa mahabusu.
    Waliofika hapo akiwepo mtangazaji wa Times FM, Dida walifikia hata hatua ya kutaka kulipa pesa hizo lakini Isha alikataa kabisa jambo hilo lisifanyike akidai hii ni aina mpya ya utapeli.
    “Haiwezekani duka ambalo lina wafanyakazi wawili na wateja wengi wanaoingia useme mtu fulani kakuibia.
    “Kwanza mteja unakuwa nyuma ya kaunta yao na si rahi kujua pesa zilipo, utalivuka vipi hilo kaunta mpaka ufike kwenye pesa bila wahusika kukuona?
    “Kwanini wasinikamate muda huo huo na kunipigia kelele za mwizi?” alihoji Isha.
    Askari mmoja wa kituo hicho aliiambia Saluti5 kuwa malalamiko ya kesi hiyo yana mushkel na yamekaaa kiujanja ujanja ujanja.
    Ameshangaa ni kwanini tukio la Jumamosi liachiwe hadi Jumatano, akashaangaa pia namna waandishi walivyotaarifiwa tukio hilo ndani ya muda mfupi.
    IMEHAMISHWA KUTOKA SALUTI 5
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments
    Item Reviewed: MAKUBWA YAMKUTA ISHA MASHAUZI, 'ABAMBIKIZIWA' KESI YA WIZI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top