• HABARI MPYA

    Wednesday, April 24, 2013

    BREAKING NEWS; HANS POPPE AREJEA MADARAKANI SIMBA SC BAADA YA KUFANIKISHA KUSULUHISHA MGOGORO WA RAGE NA WAPINZANI WAKE

    Mpatanishi; Zacharia Hans Poppe amerudisha amani Simba SC 

    Na Mahmoud Zubeiry
    SASA ni shwari Simba SC. Hivyo ndivyo unavyoweza kusema, kufuatia pande mbili zilizokuwa zinavutana, uongozi chini ya Mwenyekiti Alhaj Ismail Aden Rage na wapinzani wake kumaliza tofauti zao.
    Pongezi kubwa ziende kwake, Kapteni wa zamani wa Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ), Zacharia Hans Poppe aliyefanikisha kumaliza mgogoro wa chini kwa chini baina ya Rage na wapinzani wake.
    Akizungumza na BIN ZUBEIRY jioni hii, mpatanishi huyo wa mgogoro uliorejesha amani na umoja Simba SC, amesema; “Tofauti zilizokuwapo tumekwishazimaliza na sasa Simba SC ni shwari, tunaanza upya kazi,”alisema.
    Poppe aliyepigana vita dhidi ya Nduli Iddi Amin Dada kuokoa ardhi ya Tanzania na Watanzania waliokuwa wakinyanyswa na askari na rais huyo wa zamani wa Uganda, aliongeza; “Na kwa maana hiyo, natamka rasmi, nami nimerejea ndani ya Simba SC kwa nafasi zangu zote kama nilivyoombwa baada ya kujiuzulu,”alisema.
    Poppe alikuwa Mjumbe wa Kamati ya Utendaji na Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili- wakati huo huo Mwenyekiti wa Friends Of Simba na aliamua kukaa kando kabisa wakati mgogoro kutofungana na upande wowote, akishughulikia amani ya klabu.
    Poppe alisema kwa sasa wanalekeza nguvu zao katika kumalizia Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara kwa heshima na baada ya hapo watatengeneza timu mpya itakayoiteka soka ya nchi hii msimu ujao.
    “Tumevuna matunda ya ugomvi na migogoro katika klabu, tulianza msimu vizuri na tukawa juu kwa muda mrefu, lakini baada ya hapo naona tukalewa mafanikio tukaanza kugombana bila sababu,”.
    “Matokeo yake ndiyo haya, tumepoteza mwelekeo, lakini madhali tumemaliza tofauti baina yetu, na tumefikia makubaliano ya msingi ya kudumisha umoja na amani ndani ya klabu, ambavyo ndivyo chimbuko la mafanikio, hakuna shaka wana Simba watafurahi tena,”alisema Hans Poppe.
    Mambo yalitibuka Simba SC miezi kadhaa iliyopita kufuatia mgogoro wa chini kwa chini baina ya Rage na wapinzani wake, uliosababisha mgawanyiko hadi ndani ya uongozi.
    Makamu Mwenyekiti, Geoffrey Nyange ‘Kaburu’ alijiuzulu sambamba na Hans Poppe na tangu hapo, Simba imekuwa ikienda kama jahazi liso na Nahodha na matokeo yake ni kutaka kuzama kwa kupoteza mwelekeo.
    Matokeo yake, timu imepoteza ubingwa wa Ligi Kuu na kukosa hata nafasi ya pili, ambayo ingewawezesha kucheza Kombe la Shirikisho Afrika mwakani. 
    Amani inarejea Simba SC zikiwa zimebaki takriban wiki tatu kabla ya kumenyana na wapinzani wa jadi, Yanga SC katika mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.  
    Yanga SC walitaka sana kutumia mwanya wa mgogoro ndani ya Simba SC kulipa kisasi cha kufungwa 5-0 mwaka jana, lakini sasa inaonekana shughuli itakuwa pevu Mei 18 Uwanja wa Taifa.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments
    Item Reviewed: BREAKING NEWS; HANS POPPE AREJEA MADARAKANI SIMBA SC BAADA YA KUFANIKISHA KUSULUHISHA MGOGORO WA RAGE NA WAPINZANI WAKE Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top