• HABARI MPYA

    Tuesday, December 23, 2014

    SIMBA, YANGA SI LAZIMA KUWA KAMPUNI ILI KUJIENDESHA KIBIASHARA

    Na Hemed Hamisi, DAR ES SALAAM
    MARA kadhaa kumekuwepo na wazo la kutaka au kuzifanya klabu za Simba na Yanga zijiendeshe kibiashara. Wazo la klabu hizi kujiendesha kibiashara lipo vichwani mwa wadau wa michezo na limekuwa likishauriwa mara kwa mara ili kuzifanya klabu kuondokana na utegemezi. Tatizo linabaki kuwa ni njia ipi itumike kuzifanya zijitegemee.
    Mara nyingi mawazo mengi hukwama au kutokutimia kwa sababu kubwa moja; nayo ni kwamba binadamu kwa asili hutamani kitu kizuri pasipo kutaka misingi halisi ya upatikanaje wake, au kutotaka kuwa na pa kuanzia ili kujenga uzoefu au kujipa nafasi ya kukosolewa. 
    Uongozi mbalimbali katika klabu hizi umekuwa ukijaribu kupenyeza wazo hili kwa wanachama wao, ila limekuwa likikinzana na utashi wa baadhi ya wanachama.
    Mwenyekiti wa Yanga SC, Yussuf Manji kulia akiwa na Makamu wake, Clement Sanga

    Katika klabu ya Yanga, zilikuwapo jitihada za kuifanya Yanga kuwa kampuni, tangu enzi za George ‘castro’ mpondela, Tarimba abass hadi zile za Jamal malinzi. Jitihada hizi zilikwama na hata kuchangia kuzua migogoro mikubwa ya mara kwa mara. Kwa upande wa Simba, wao utashi wa kuwa kampuni ulibaki mioyoni mwa baadhi ya viongozi au baadhi ya wanachama labda kwa hofu ya kuona yasije tokea yale yaliyokuwa yakiendelea kwa watani zao. Na mwanzoni mwa miaka ya 2000 Simba ikiwa chini ya udhamini wa METL, inasemekana wazo hili lilipenyezwa na mdhamini lakini mwitikio ukawa haupo hadi kufifisha jitihada za mdhamini.
    Kwa ujumla tunaweza ona wazo la klabu kujiendesha lipo, na wengi kama siyo wote wanaliafiki. Isipokuwa klabu kuwa kampuni ndipo penye ukakasi kama siyo mgogoro. Na hapa ndipo msingi wa mada yangu kwa leo utakajikita.
    Kimantiki ukiangalia msingi wa uanzishwaji klabu chochote cha michezo ni kwa ajili ya burudani na si kampuni ya burudani. Hata mimi binafsi ntashangaa nikisikia klabu yangu ninayoipenda ya Man utd imegeuzwa nakuwa Man utd Co.ltd. kama itatokea hivyo, nafikiri kuanzia hapo ntaangalia namna mbadala ya kuanzisha mahusiano mapya nayo, kama vile kuangalia ofa yao ya mwanzo (Initial Public Offer) kwenye soko la hisa la London kwamba imesimamia paundi ngapi kwa kipande ili nione uwezekano wa kununua hisa kadhaa.[ angalizo; hisa ninazozizungumzia hapa ni Company shares, na siyo Ownership shares. Kwa maana mtu kuinunua klabu kama ilivyokuwa Moro utd hapo ananunua umiliki, haimaanishi kuwa Moro utd ilikuwa ni kampuni].
    Kimsingi, klabu kujiendesha kibiashara haimaanishi klabu iwe kampuni. Na kwa klabu ya wanachama kama Simba au Yanga (open public club) inaweza kujiendesha kibiashara kwa namna kuu mbili;
    1. Kuuza huduma (service rendering)
    Hili ni eneo pana linalojumuisha mambo mengi kama vile viingilio uwanjani vinavyotokana na klabu kutoa burudani. Pia mapato ya klabu kutokana na ushiriki wa mashindano mbalimbali, tuzo na zawadi, fedha za wadhamini n.k. kadiri klabu inavyoimarika katika kutoa burudani kwa mashabiki ndivyo dhana ya ‘customer royalty’ (kiwango cha mteja kuiamini bidhaa) klabu machoni mwa wadau inavyokuwa kubwa, na kisha kuvutia zaidi udhamini. Mfano mzuri ni Mbeya City katika msimu wa ligi uliopita ilipata customer royalty kubwa, kiasi cha kufanikisha wadhamini wapya wawili. Na hata mapato ya viingilio kati ya timu na timu hutofautiana kulingana na customer royalty ya timu husika. Hivyo basi iwapo klabu itaboresha misingi inayopelekea customer royalty kuwa kubwa, moja kwa moja itakuwa ni hatua kunako kujiendesha kibiashara. Mbali na mapato ya viingilio, pia klabu inaweza toa huduma ya kununua na kuuza wachezaji, kulea vipaji na kuuza (hapa ndipo uwekezaji wa akademi ulipo). Pia kuna mapato yatokanayo na udhamini kwa klabu kuitangaza kampuni Fulani hadharani wakati wa utoaji burudani kwenye matukio mbalimbali. Hapa uwezo wa viongozi katika nguvu ya kujadili maslahi (bargaining power) sharti uwe mkubwa. Kwa maana siyo lazima klabu kuwa na mdhamini mmoja katika matukio yote. Haiwezekani malipo ya mdhamini kwa klabu kuwa sawa kila mwaka bila kujali ushiriki wa klabu katika mashindano ya kimataifa iwapo nako mdhamini ataendelea kutangazwa.
    Ni lazima vilabu vitenganishe ujazo (packages) mbalimbali katika ofa zao za kutangaza mdhamini, ili mdhamini anunue ofa anazoona zinafaa. Mathalani iwepo ofa yenye ujazo (packages) hizi;
    - Udhamini wa mazoezi
    - Udhamini wakati wa safari
    - Udhamini wa mechi za ligi
    - Udhamini wa mechi za kirafiki
    - Udhamini wa matangazo uwanjani wakati klabu inacheza
    - Udhamini wakati wa mechi za kimataifa
    Ofa hizi zitangazwe kama zabuni mathalani kila mwaka mpya wa mahesabu ya klabu. Kampuni mbalimbali ziweke tenda, halafu kila ‘package’ ishindanishwe. Ikitokea mdhamini mmoja akashinda ofa zote kwa kutoa dau la juu, basi hakuna ubaya maana kilichohitajika ni kukuza mapato ya udhamini na si idadi ya wadhamini( kuna usemi kwamba; ubora wa paka si wingi wa manyoya, bali ni uwezo wa kukamata panya). Hivyo iwapo mapato ya udhamini yakiwa makubwa, inatoa msingi wa klabu kujiendesha kibiashara.
    Malipo mengine yanayohusu huduma ni kwa klabu kukodisha (renting-out) nembo yao. Hapa klabu inawezakuzishawishi kampuni mbalimbali kutumia nembo yao katika mauzo ya bidhaa mbalimbali.
    Rais wa Simba SC, Evans Aveva kulia akiwa na kocha Patrick Phiri

    Baada kuangalia maeneo ambayo klabu za wanachama zinaweza kuyakuza ili zifikie kujiendesha, sasa ndipo tunajiuliza kama hayo yote yapo au ni rahisi kuwapo, kwanini zinashindwa kujiendesha?
    Jibu ni kwamba, tatizo lililopo katika namna hii ya kwanza ambayo klabu ingepelekea kujiendesha kibiashara ni kwamba klabu hazina mfumo maalumu wa kuyashughulikia haya. Ni lazima klabu kuanzisha mfumo maalumu wa kiutawala (kiutendaji) ili kuweza kuyasimamia haya. Mfumo uliopo kwa sasa ni kuundwa kwa kamati za kuratibu haya, mfumo huu wa kiujumla hauna msingi wowote wa kiuwajibikaji (kwamba, hakuna njia ya mtu kupangiwa na kulazimika kuyatekeleza majukumu aliyopangiwa). Ni lazima pawepo na mfumo wa kuwajibika na siyo mfumo wa kujitolea. Ili kuwa na mfumo wa kiuwajibikaji ni lazima yafanyike yafuatayo;
    Kuunda muundo wa ki-utawala
    Tunaona mfumo wa sasa wa klabu kudhani kwamba uwepo pekee wa kamati mbalimbali unaweza kutosha kuratibu shughuli za kila siku ni kukosea. Huwezi kuendesha klabu hizi kwa muundo wa ki-uongozi pekee pasipo muundo wa ki-utawala. Mfumo wa kuibua na kuendesha mambo kupitia kamati tu kunafanya kamati zifanye kazi kwa matukio. Hakuna namna nzuri ambayo kamati hizi zinaweza pimwa ufanisi wake, achilia mbali namna zinavyoweza kuwajibishwa. Kamati zinaundwa na watu wenye shughuli zao binafsi, ambapo hawawezi kuratibu mwenendo wa kila siku wa klabu.
    Lakini kama zitabadilisha mfumo wake na kuwa na mfumo wa kiutawala, basi watakuwepo wataalamu walioajiriwa na klabu katika kada mbalimbali ambao watawajibika kwa mamlaka yao ya ajira (ambayo ni uongozi wa klabu). Panapokuwepo na mfumo huu wa kiuwajibikaji ni rahisi kuwepo na mpango na kisha kupimwa kiwango cha utekelezaji wake ambao utawasilishwa kwenye vikao mbalimbali hadi mkutano mkuu. 
     Kwa kuwa hoja hapa ni kujiendesha kibiashara, ntatoa mfano unaoendana; mathalani, kurugenzi ya fedha ya klabu yenye vitengo vya uhasibu, ugavi na manunuzi, masoko n.k itakuwa na shughuli za kila siku za kuratibu maendeleo ya klabu kulingana na mpango wa utekelezaji na bajeti vya mwaka husika au kipindi husika. Utendaji wa kurugenzi hii itawasilisha ripoti yake ya utekelezaji kwa kamati ya fedha na uchumi ya klabu, iliyoteuliwa. Kamati ndiyo itashauri, itakosoa ama kuagiza nini mahitaji yao, na kuwaachia wataalamu hawa wabangue bongo zao katika kufanikisha maazimio ya kamati. Huu ndiyo mtindo unaotumika kuendesha taasisi za watu/umma/jumuia (public entities). Mfano; kwa serikali, haiwezekani kamati ya miundombinu ya bunge ndiyo iratibu shughuli za utendaji wa miundombinu ya nchi, au kamati ya miundombinu ya halmashauri ndiyo iratibu shughuli za miundombinu ya halmashauri, bali ni wataalamu ndiyo hufanya kazi hizo, kisha wao kuripoti kwa kamati husika, maana ndiko wanawajibika. Baada ya hizi kamati kupokea na kujadili utekelezaji wa mipango ya klabu unaofanywa na watendaji ndipo wenyeviti wa kamati hizi watawasilisha maazimio kwenye kikao cha juu cha kamati ya utendaji tayari kwa maamuzi.
    Iwapo Simba na Yanga kweli zinataka zijiendeshe kibiashara, hazina budi zibadilishe mfumo wao wa uratibu shughuli, toka wa kiuongozi kwenda wa kiutawala. Na hili halihitaji mpaka ziwe kampuni au mpaka zibadilishe katiba.
    Japokuwa hata sasa vipo vyeo vya kiutawala kama vile katibu na msemaji wa klabu, lakini cheo bila muundo wa kiuwajibikaji au wa ki-muunganiko (administrative link) ama bila viashiria vya upimaji (performance indicators) kinakosa maana. Kwa ukubwa wa taasisi kama Simba na Yanga, huwezi kuwa na katibu tu ndiyo aratibu kila kitu cha kiutendaji kitakachokidhi matarajio ya wadau mbalimbali wa klabu. (yaani kuanzia kushughulikia bili za maji na umeme, bima za afya za wachezaji, mikataba ya wapangaji, maelekezo ya TFF, ukarabati wa majengo, vikao vya kamati, ununuzi wa maji na glucose za mazoezini, matengenezo ya gari lililoko gereji hayo kwa uchache, n.k) si tu kwamba ni majukumu mengi, tatizo ni kwamba hayana ‘link’. Na hata awe ‘genious’ kiasi gani mtaishia kumlaumu bure. Ndiyo maana kila siku klabu hizi zinaajiri na kuacha makatibu kwa kuwaona wanapwaya au hawakidhi matarajio. Kwa mfumo huu uliopo wa kutokuwa na administrative back-up, hata klabu hizi zikafanikiwa kumshawishi mkuu wa chuo mstaafu, Prof; Mathew Luhanga aje awe katibu mkuu pale, bado naye akimaliza mkataba wake hawatamuongeza mwingine, maana wataona hakuna alichosaidia.
    Ili klabu zijiendeshe, hazina namna zaidi ya kuingia mfumo huu wa kiutawala wenye watendaji wataalamu walioajiriwa kwa kazi na fani tofauti kulingana na muundo wa kimahitaji ya klabu utakaowekwa. Hivyo hakuna njia ya mkato kwa hili. Wataalamu wa hesabu wanasema f(0)=0, maana yake; “there is no more mana from the heaven”(hakuna mana zaidi itashuka toka mbinguni). Ili upate kitu, sharti uweke kitu. 
    2. Klabu kuanzisha shirika
    Katika mfumo wa uendeshaji taasisi za umma/jumuia, upo utaratibu unaozifanya taasisi za namna hii kushiriki moja kwa moja kwenye biashara au uzalishaji mali.utaratibu huu hufanyika kwa taasisi za namna hii kuanzisha divisheni ya shirika linalojiendesha kibiashara lililo chini ya taasisi hizo. Ifahamike kwamba, katika msingi huu,taasisi (klabu) haibadiliki na kuwa shirika/kampuni, bali taasisi/klabu inakuwa inamiliki shirika/kampuni. Hivyo menejimenti ya kampuni hii inawajibika kwa klabu. Na bodi ya udhamini ya klabu ndiyo bodi ya udhamini wa shirika/kampuni (kwa maana, ndiyo yenye wajibu wa kisheria kuweka zuio la mali za kampuni hii).
    Nawatoa hofu wanachama na wapenzi wa vilabu vya Simba na Yanga kwamba, utaratibu wa kuzifanya klabu zao kumiliki kampuni/shirika siyo jambo la hatari litakalogeuza madhumuni ya uanzishwaji wa klabu zao, bali ni kuzifanya ziwe madhubuti zaidi kiuchumi. Hapa ntatoa mifano michache ya taasisi za umma zilizoanzisha mashirika ya uzalishaji mali yanayojiendesha kibiashara bila kuathiri misingi ya uanzishwaji wa taasisi hizo. Mfano; taasisi nyeti kabisa kwa ulinzi wa nchi (jeshi la wananchi) linalo shirika la uzalishaji (biashara) linaloitwa MZINGA, wakati jeshi la kujenga taifa nalo linalo shirika lake linaloitwa SUMA-JKT. 
    Kwa upande wa serikali za mitaa, halmashauri ya jiji la dar es salaam linalo shirika la DDC   (ambapo UDA,soko la k’koo na sehemu ya hisa za DCB-BANK) vipo chini ya umiliki wake. Hivyo kadiri vyombo hivi tanzu vinapopata faida, ndivyo gawiwo la faida linavyokwenda kwa halmashauri ya jiji na kuongeza pato lake. Kwa maana hiyo, upo uwezekano wa vilabu vya Simba na Yanga kumiliki mashirika/makampuni yake, kwani nembo zao tu ni kampuni tosha.
    Mara klabu ianzishapo kampuni, kampuni husika itashindana sokoni kama kampuni nyingine, na itajiendesha kwa misingi ile ile ya makampuni. Na mwisho wa siku manufaa yanakwenda kwa klabu. Na hapa ieleweke kwamba, zipo biashara ambazo zina majanga kidogo ambazo klabu hailazimiki kuzizalisha yenyewe kuanzia mwanzo mpaka mwisho, bali kuongeza thamani tu ya nembo yake. Iwapo klabu itakuwa na kampuni yake, ni rahisi kwa kampuni hii kutoa oda toka kampuni nyingine inayotengeneza bidhaa Fulani (mfano viatu vya watoto vya kuchezea mpira, iwatengenezee viatu vyenye nembo ya klabu) hapa tunaona kwamba, kumbe ni kampuni ya klabu ndiyo inaagiza kampuni nyingine, na si kama ilivyosasa kwa klabu kuiomba kampuni Fulani itumie nembo yake ili klabu ipewe gawiwo. Jamani, siyo ulimwengu mzima unazijua Simba na Yanga! Ni ngumu kwao kuingia dhamana ya kujibebesha mzigo wakati hawajui wigo wa soko la nembo hiyo ukoje, siyo tu nje ya Tanzania, bali hata ndani ya Tanzania yenyewe. (ni ngumu kuipata Nike kuja kuingia ubia kuuza bidhaa za coastal, lakini inawezekana kwa coastal kuipa kazi Nike kutengeneza bidhaa zake).
    Ni vipi klabu inaweza kumiliki kampuni?
    Njia madhubuti ya klabu kumiliki kampuni ni ile ambapo kampuni inakuwa chini ya klabu. Katika mfumo wa mgawanyo wa kampuni kunakuwa na makundi mawili kufuatana na aina ya kadi za wanachama.
    - Kundi la kadi za kawaida za awali
    Kadi hizi kawaida za awali ndiyo msingi mama wa kampuni. Kila mwanachama hai wa klabu ni mbia wa kampuni. Na pato la mchango wa wanachama hawa kwa vyovyote vile ndiyo litahesabika kama hisa za klabu kwenye kampuni anzishwa. Na gawio la faida kwa kundi hili, linakuwa moja kwa moja ni mali ya klabu. Kwa lugha nyepesi linaingia katika kapu la kawaida la siku zote, linalopelekea mpira uchezwe. (kuleta furaha ya mashabiki)
    - Kundi la kadi za amana
    Hizi ni kadi za amana ambazo zinawakilisha umiliki wa mtu mmoja mmoja kwenye kampuni ya klabu. Katika kadi hizi, mtu atanunua hisa kadiri atakavyoona kwake ni faida. Si lazima hisa hizi ziuzwe kwenye soko la hisa, bali kuafiki tu kuwa na kadi hii ya amana unaingia moja kwa moja kwenye umiliki wa kampuni. Suala hapa ni kufanya ‘marketing’ tu kimkakati kulingana na eneo au tukio katika kusajili wanachama wa kadi hizi (hapa klabu inaweza ika toa ‘out-source’ kazi kwa wakala ambaye atalipwa kamisheni kulingana na idadi ya usajili). Lakini pia, kadi hizi za amana zinaweza uzwa kwenye soko la mtaji, na haitajalisha mnunuzi ni nani.
    Kwa upande wa manufaa, klabu itanufaika kwa namna mbili. Kwanza ni kwakuwa kundi lote la kadi za awali ni wanahisa wanaounda hisa za klabu kwenye kampuni. Pili, hata ikitokea mtu mmoja kuwa na umiliki mkubwa wa hisa za kampuni ya klabu, mtu huyu hatohusiana na mwenendo wa uendeshaji klabu, bali mwenendo wa kampuni ya klabu. Na iwapo ataingiza utaratibu unaoongeza faida ya kampuni, basi klabu nayo itanufaika na ongezeko la gawio.
    Nazihakikishia Simba na Yanga kwamba; kama zitaanzisha divisheni tanzu ya zenyewe kumiliki kampuni/shirika zitakuwa moja kwa moja zimeingia katika kujiendesha kibiashara. Kwanini? Kwa sababu biashara ni chombo tofauti na mmiliki (business is a separate entity from the owner). Dhana hii ni muhimu sana kibiashara, kwani huiwezesha kampuni/taasisi ndiyo ihusiane na wadau wake, na siyo mtu aliye kwenye taasisi kuhusiana na taasisi nyingine.
    Kama kampuni ya klabu itafanya vizuri sokoni, itavutia zaidi watu kukata kadi amana (naamini kwa utamaduni uliopo Tanzania hii wa mtu kuweka upendeleo katika ununuzi wa bidhaa maadam tu ina rangi ya timu aipendayo) vipi itakuwa pale ambapo mteja atakutana sokoni  na bidhaa inayosambazwa na kampuni ya klabu yake? 
     Namalizia kwa kusema kwamba; siyo lazima kwa Simba na Yanga ziwe kampuni ndipo zijiendeshe kibiashara. Mabadiliko katika mfumo wa kiuendeshaji toka uliopo wa kamati kuratibu shughuli za klabu kwenda mfumo wa kiutawala ambapo watendaji watawajibika kwenye kamati mbalimbali za usimamizi, kisha kuwajibika kwenye chombo cha juu ambacho ni kamati ya utendaji ya klabu, kunaweza kuzifanya klabu hizi kujiendesha kibiashara.
    Pia utaratibu wa klabu kumiliki shirika/kampuni ya biashara kwa mujibu wa sheria kutazifanya klabu kunufaika na gawio la faida, kunaweza kuvifanya vilabu hivi kujiendesha kibiashara, achilia mbali uwekezaji mbalimbali unaoweza fanywa kwa ubia na kampuni nyingine, hususani kwa klabu kuongeza thamani ya bidhaa kwa kutumia nembo yake.
    Leo niishie hapa. Panapo majaaliwa, siku nyingine tutaangazia muundo wa kiutawala na mgawanyo wa kazi unaoweza tumika na klabu ili kuzifanya zijiendeshe kibiashara.
    “Kabla hatujatumia muda mwingi wa kufikiria kasi ya chombo kitakapokuwa angani, ni vema basi kukesha tukiwaza ni namna gani chombo kitanyanyuka toka ardhini ili kiweze kupaa angani”.
    Nawasilisha. 

    Imeandikwa na Hemed HR, ni mshauri huru masuala ya uchumi na fedha (Freelance Consultant), 0762 955454. sangameydi@yahoo.co.uk
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SIMBA, YANGA SI LAZIMA KUWA KAMPUNI ILI KUJIENDESHA KIBIASHARA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top