• HABARI MPYA

    Friday, December 26, 2014

    LIGI KUU YAREJEA LEO, SIMBA SC NA KAGERA HAPATOSHI TAIFA

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    LIGI Kuu ya Vodacom Tanzania Bara inarejea leo baada ya kuwa mapumzikoni tangu Oktoba 12 na nyasi za Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam zinatarajiwa kuwaka moto kwa mchezo kati ya wenyeji Simba SC na Kagera Sugar ya Bukoba.
    Kutakuwa na mchezo mmoja tu leo wa Ligi Kuu katika siku ya kupeana vifurushi, maarufu kama Boxing Day, wakati kesho kutakuwa na mechi tatu zaidi na keshokutwa tatu nyingine kukamilisha raundi ya nane.
    Kagera Sugar watakuwa wageni wa Simba SC Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam 

    Mechi za kesho vinara wa Ligi Kuu, Mtibwa Sugar wataikaribisha Stand United ya Shinyanga Uwanja wa Manungu, Turiani mkoani Morogoro, Prisons watakuwa wenyeji wa Coastal Union Uwanja wa Sokoine mjini Mbeya, wakati JKT Ruvu wataikaribisha Ruvu Shooting Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, Dar es Salaam.
    Raundi ya nane itahitimishwa kwa mechi tatu Jumapili, Uwanja wa Taifa, Yanga SC wakiwa wenyeji wa Azam FC, wakati Mbeya City wataikaribisha Ndanda FC Uwanja wa Sokoine na Polisi Moro itakuwa mwenyeji wa Mgambo JKT Uwanja wa Jamhuri, Morogoro.
    Hadi Ligi Kuu inasimama baada ya raundi ya saba, Mtibwa Sugar walikuwa kileleni kwa pointi zao 15, wakifuatiwa na Azam FC na Yanga SC zilizofungana kwa pointi 13 kila moja na hata wastani wa mabao ukiwa sawa.
    Coastal Union iliyomaliza na pointi 11 ilikuwa nafasi ya nne, ikifuatiwa na Kagera Sugar yenye pointi 10 sawa na JKT Ruvu, wakati Simba SC walimaliza na pointi tisa katika nafasi ya saba sawa na Polisi Moro, Mgambo JKT na Stand United.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: LIGI KUU YAREJEA LEO, SIMBA SC NA KAGERA HAPATOSHI TAIFA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top