• HABARI MPYA

    Thursday, May 21, 2015

    ‘BEKI WA REAL’ AANGUKA MIAKA MITATU SIMBA SC, NDEMLA NAYE AJITIA KITANZI MSIMBAZI HADI 2018

    Na Princess Asia, DAR ES SALAAM
    BEKI aliyewahi kuripotiwa kutakiwa na Real Madrid Castilla, inayoshiriki Ligi Daraja la Kwanza Hispania, maarufu kama Segunda B, Hassan Isihaka (pichani kulia) amesaini Mkataba mpya wa miaka mitatu na Simba SC.
    Mapema mwaka huu, maskauti wa Real Madrid waliozuru Tanzania, walivutiwa na wachezaji wawili wa SImba SC, beki Isihaka Hassan na kiungo Ramadhani Singano ‘Messi’.
    BIN ZUBEIRY iliripoti timu hiyo ya pili ya mabingwa wa Ulaya, Real Madrid inayocheza mechi zake Uwanja wa Alfredo di Stefano, kupitia mwakilishi wake, Rayco Garcia iliwasilisha rasmi maombi yake kwa klabu ya Simba SC juu ya wachezaji hao.
    Garcia alisema anawataka wawili hao Juni mwaka huu waende Hispania kufanyiwa majaribio katika timu hiyo na kama wakifuzu wataanza maisha mapya Ulaya.
    Wakati bado Juni inabisha hodi, Isihaka anarefusha muda wa kuendelea kuitumikia Simba SC hadi mwaka 2018.
    Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Simba SC, Zacharia Hans Poppe ameiambia BIN ZUBEIRY jana kwamba, mbali na Isihaka, kiungo chipukizi Said Hamisi Ndemla naye ameongeza Mkataba wa miaka mitatu pia.
    “Chipukizi hawa wawili, wote wataendelea kufanya kazi Simba SC hadi mwaka 2018, na bado tunapitia ripoti ya benchi la Ufundi, ili kuboresha mikataba ya wachezaji wengine ambao tunahitaji kuendelea nao,”amesema Kapteni huyo wa zamani wa Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ).
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: ‘BEKI WA REAL’ AANGUKA MIAKA MITATU SIMBA SC, NDEMLA NAYE AJITIA KITANZI MSIMBAZI HADI 2018 Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top