• HABARI MPYA

    Saturday, January 31, 2015

    BAHANUZI AZIDI KUNG’ARA POLISI MORO, AWAANGAMIZA MBEYA CITY JAMHURI LEO

    Na Mwandishi Wetu, MOROGORO
    MSHAMBULIAJI Said Rashid Bahanuzi (pichani kulia) anayecheza kwa mkopo Polisi Moro, leo amefunga bao lake la pili katika timu hiyo tangu asajiliwe Desemba.
    Mshambuliaji huyo alitolewa kwa mkopo Polisi baada ya kupoteza cheche za mabao Yanga SC, lakini akiwa katika timu mpya anaonekana ‘kufufuka’. Bahanuzi amefunga bao pekee Polisi ikiibwaga 1-0 Mbeya City Uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro katika mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara.
    Akicheza mechi yake ya nne tangu atue timu ya jeshi la Polisi, Bahanuzi alifunga bao hilo pekee dakika ya 66.
    Katika michezo mingine ya Ligi Kuu leo, Simba SC imeshinda 2-1 dhidi ya JKT Ruvu Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, mabao yake yote yakifungwa na Mganda, Dan Sserunkuma, la wapinzani likifungwa na George Minja.
    Nurdin Msiga ameifungia Prisons Uwanja wa Sokoine mjini Mbeya ikitoka sare ya 1-1 na Kagera Sugar, ambayo bao lake lilifungwa na Rashid Mandawa, wakati Coastal Union imelazimishwa sare ya 0-0 nyumbani na Mtibwa Sugar Uwanja wa Mkwakwani, Tanga. 
    Ligi Kuu itaendelea kesho kwa mechi mbili, Ruvu Shooting na Stand United Uwanja wa Mabatini, Mlandizi, Pwani na Yanga SC na Ndanda FC Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: BAHANUZI AZIDI KUNG’ARA POLISI MORO, AWAANGAMIZA MBEYA CITY JAMHURI LEO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top