• HABARI MPYA

    Saturday, November 23, 2013

    RAGE AJICHUKULIA ‘POINTI TATU’ NYINGINE LEO, KINESI ATOKA MKUKU HADI AIBU, ILIKUWA KILA KONA “RAGE…RAGE…RAGE…”

    Na Mahmoud Zubeiry, Ilala
    MWENYEKITI wa Simba SC, Alhaj Ismail Aden Rage leo aliiteka hadhira alipotokea Uwanja wa Karume, Ilala, Dar es Salaam, ambako timu ya vijana ya klabu yake, Simba B ilikuwa inamenyana na Ruvu Shooting katika michuano ya timu za vijana chini ya umri wa miaka 20. 
    Rage alitokea Uwanja wa Karume wakati wa mapumziko akiwa anatembea kwa miguu na wakati anafika tu yowe za kumshangilia zilichukua nafasi yake; “Rage, Rage Rage” na Kaimu Makamu Mwenyekiti, Joseph Itang’are ‘Kinesi’ akaondoka mara moja akikimbiza gari lake kama mtu anayekimbizwa.
    Hapa vipi, tunapotosha? Rage akiingia Karume huku akipunga mkono na watu wakimshangilia. Angalia na chini.

    Rage aliingia katika uzio wa Uwanja na kuinua mikono juu akiwapungia mashabiki ambao walimshangilia kama limefungwa bao. Wengine wakaenda kumkumbatia.
    Baada ya hapo, Rage akaenda nyuma ya jukwaa ambako wachezaji wa Simba walikuwa wanapewa mawaidha na kocha wao Suleiman Matola.
    Alipofika alitulia kwanza kumsubiri kocha amalize kuhutubia na baada ya hapo akasema; “Mimi si mtu wa maneno, mzigo huu hapa (Sh. 500,000) chukueni, mimi nataka ushindi,”alisema Rage na kuwaachia fedha hizo na kwenda kuketi kutazama mpira.
    Bahati mbaya, SImba B ilifungwa 2-1 ikitoka kuongoza 1-0. Wakati akiwa ameketi anatazama mpira, mashabiki waliokuwa wanatazama mpira kutoka jengo la Machinga Complex nao wakaripuka na yowe za kumsahngilia Rage. “Rage Rage Rage”.
    Anapendwa; Shabiki wa Simba SC akimkumbatia Rage kwa furaha. Angalia na chini.

    Sahau kuhusu blogu uchwara za ‘Mashauzi Mpwitompwito ’ zinazomkandia Rage kwa chuki binafsi, Mbunge huyo wa Tabora Mjini (CCM) bado ana mvuto mbele ya mashabiki na wapenzi wa Simba, pamoja na tuhuma kibao zinazomkabili juu ya matumizi mabaya ya madaraka yake.
    Rage ameagizwa kuitisha Mkutano Mkuu wa Dharura wa klabu ndani ya siku 14 kuanzia sasa na Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) limetoa agizo hilo baada ya kubaini kuwa mgogoro katika klabu hiyo, baada ya kupokea barua mbili; moja kutoka Kamati ya Utendaji ikielezea kumsimamisha uongozi Rage, na nyingine kutoka kwa Mwenyekiti huyo ikielezea kutotambua kusimamishwa huko.
    Uamuzi wa TFF umefanywa kwa kuzingatia Ibara ya 1(6) ya Katiba ya Simba inayosema: “Simba Sports Club ni mwanachama wa TFF, itaheshimu Katiba, kanuni, maagizo na uamuzi wa TFF na FIFA, na kuhakikisha kuwa zinaheshimiwa na wanachama wake.”
    TFF itatuma wawakilishi wake katika mkutano huo, na kumuagiza Mwenyekiti wa Simba kuhakikisha wanachama wote wenye hoja wanapata fursa ya kusikilizwa.
    Wajumbe wa Kamati ya Utendaji ya Simba walikutana Jumatatu wiki na kutangaza kumsimamisha Rage aliyekuwa Sudan kwa shughuli za kisiasa kwa tuhuma za kuamua mambo mengi bila kushirikisha wenzake.
    Anatoa fedha kwa Simba B, kocha Matola anapokea pembeni ya Ibrahim Masoud 'Maestro'. Kulia ni Madaraka Selemani 'Mzee wa Kiminyio'

    Hata hivyo, Rage alirejea jana usiku na kusema Kamati ya Utendaji haina uwezo Kikatiba kumsimamisha Mwenyekiti na akaahidi kuzungumza na Waandishi wa Habari leo. Lakini Rage akaahirisha Mkutano huo na kusema atazungumza kesho.  
    Anamsalimu aliyekuwa Makamu wake Mwenyekiti, Geoffrey Nyange 'Kaburu' kulia. Na Chini ameketi sasa eneo la VIP, nyuma yake ni mwanachama maarufu wa Simba, Daniel Tumaini 'Kamna'. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: RAGE AJICHUKULIA ‘POINTI TATU’ NYINGINE LEO, KINESI ATOKA MKUKU HADI AIBU, ILIKUWA KILA KONA “RAGE…RAGE…RAGE…” Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top