• HABARI MPYA

    Saturday, November 30, 2013

    MICHAEL WAMBURA: WATU WANADHANI NIMETEULIWA SIMBA KUMLINDA RAGE,LAKINI...

    "Hivi karibuni niliteuliwa na Mwenyekiti wa Klabu ya Simba Mhe Ismail Aden Rage  kuwa mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya Simba.Wanachama na wapenzi wengi wa Simba kutoka sehemu mbali  nje na ndani ya nchi walinipiga simu, wengine wakinitaka nikatee uteuzi na wengine wakinitaka nikubali uteuzi, kila mmoja  akiwa na sababu zake,  Wakati napokea uteuzi huu na kutafakari ilibidi nijiridhishe  katika mambo mbalimbali  yakiwemo yafuatayo:

    1. Uhalali wa uteuzi huu kisheria na  hasa  kwa kuzingatia hali halisi  ya sasa ya siasa za Klabu.
    2. Nini mantiki ya  kuteuliwa kwangu  wakati huu wa mgogoro na nini hasa nafasi yangu.
    3. Nini utakuwa mchango wangu katika kamati ya Utendaji katika wakati huu na baadaye.
    4. Wajibu wangu ni nini kama mwanachama wa Simba.
    5. Nini chanzo cha mgogoro huu wa Simba na ulazima wa wanachama wa Simba Kuingia Katika Mgogoro huu.
    6. Utayari wa pande mbili zinazopingana kurudi katika meza ya Mazungumzo
    7. Athari za muda mfupi na Mrefu kwa Klabu ya Simba  kwa kurejea migogoro mbali mbali iliyo wahi  kutokea  katika siku za Nyuma.
    8. Kina nani hasa watakaofaidika zaidi na mgogoro huu (viongozi wa Simba, Wanachama wa Simba, Klabu ya Simba  au wapinzani na maadui wa Simba).
    9. Nini Nafasi ya TFF katika kutatua na Kupatia ufumbuzi wa mgogoro huu.

    Baada ya kujiuliza na kutafakari nilitambua na kujiridhisha kama ifuatavyo:

    1. MAMALAKA YA MWENYEKITI KUTEUA WAJUMBE WAWILI WA KAMATI YA UTENDAJI YA SIMBA
    Kwa mujibu wa Katiba ya Simba Ibara ya 28(1)(d) mwenyekiti anaweza kuteua wajumbe wawili kuingia kwenye Kamati ya Utendaji ya Simba , bila kutoa  nafasi ya Wateuliwa kuuliza wameteuliwa kutoka katika kundi lipi kati ya Wajumbe wawili. Kwa mantiki hiyo mwenyekiti anapewa  nguvu za kikatiba kuteua wajumbe wawili ambao anaona wanaweza kumsaidia katika shughuli  mbalimbali za kuendesha klabu na sio zawadi au shukurani kama ambavyo wengi wamekuwa wakitafsiri,nadhani jambo muhimu la kuhoji ni wanaoteuliwa wanakwenda kufanya nini kwenye kamati ya Utendaji kwa maana ya uwezo wao kuisaidia Simba na sio nani ateuliwe na nani asiteuliwe kwani hilo liko katika mamalaka ya  mteuzi alimradi tu anayeteuliwa ni mwanachma wa Simba na ataongeza tija kwa klabu.
    2. NINI MANTIKI YA KUTEULIWA  KWANGU   KATIKA WAKATI HUU WA MGOGORO  NA NINI HASA NAFASI YANGU
    Wanachama na wapenzi wengi wa Simba walitafsiri uteuzi huu umefanyika kwa nia ya kumsaidia mwenyekiti ili aendelee kukaa madarakani, watu wenye mawazo hayo pamaoja na wengine waliokuwa na mawazo  tofauti na hayo hawakuangalia na kuzingatia  kwa upana sababu za uteuzi huu, Ukweli ni kwamba wajumbe wote wa kamati ya Utendaji ya Simba akiwemo mwenyekiti walikuwa ni sehemu ya mgogoro huu hivyo isingekuwa rahisi  pande zinazopingana  kutafuta suluhu kama itahitajika, hivyo ni wazi ni mtu  mwingine mwenye uzoefu na  uwezo wa kutatua mgogoro huu na  ambaye hakuwa na upande wowote katika mgogoro huo alihitajika , aidha ninamini kuwa  Uzoefu wangu katika uongozi wa mpira wa miguu na Elimu  yangu Ulifaa  kuingia katika Kamati ya Utendaji ya Simba ili pamoja na mambo mengine niweze kutafuta na kurejusha amani katika Simba , ninapenda ieleweke kuwa katika mgogoro huu mimi sikuwa na sina pande wowote katika pande  mbili zinazopingana , jambo lililonifanya  kujiuliza ikiwa nitakubali uteuzi  huu Simba Itafaidika na nini na kama nikikataa uteuzi  Smba itapata hasara kiasi gani, niligundua kukataa kuna athari kubwa zaidi kwa Simba aidha ingekua pia ni udhaifu na kukosa ukomavu katika uongozi ambao kwa kiasi kikubwa uamuzi huo ungetafsiriwa ni kuweka mbele ubinafsi badala ya maslahi ya walio wengi na klabu, watu wengi walijiuliza inakuwaje Rage  kumteua Wambura  na mimi kukubali kufanya kazi nae  hasa ukizingatia mahusiano yao katika siku za nyuma katika utawala wa mpira wa miguu, Jibu langu ni kuwa SIMBA KWANZA  MAHUSIANO YA MTU NA MTU BAADAYE.




    3. NINI UTAKUWA MCHANGO WANGU WA SASA NA SIKU ZA BAADAYE  KWA SIMBA.

    Baada ya kutafakari kwa  kina mchango wangu kama mjumbe wa kamati ya Utendaji ya Simba kwa siku za usoni, niligundua ya kuwa sitakuwa na msaada wowote kwa klabu yangu kama mgogoro huu hautakwisha na viongozi kurudi katika meza moja na kufanya kazi ambayo wanachama wa Simba walitegemea wafanye wakati wanawachagua,  hivyo niliona ni vyema nikachukua jukumu la kuingilia kati mgogoro huu ili niweze  kujua nini hasa kiini cha mgogoro huu katika Uongozi wa Simba. Nilipata nafasi ya kuongea na Mwenyekiti wa Simba na  kisha kuongea na mjumbe mmoja moja waliochaguliwa  wa Kamati ya Utendaji na Kisha kukutana nao kwa pamoja katika siku tofauti tofauti, ili kujua kiini na sababu za sintofahamu iliyokuwa inaendelea ndani ya Uongozi wa Simba, Kwanza nina penda kuwashukuru wajumbe  wote wa kamati ya Utendaji ya Simba Kwa Ushirikano mkubwa na mzuri walionipa, ufahamu wao  na uelewa wao wa masuala ya Simba umeonyesha  ukomavu mkubwa na weledi  katika uongozi wa Simba, tumefanya mazungumzo marefu , makubwa na ya Kina juu ya mstakabali wa Klabu yetu,  wajumbe walikuwa na masikitiko na manung’uniko mbalimbali ya msingi ambayo kimsingi mwenyekiti atakaporejea atakutana na kamati yake ili mamabo ya msingi yaliyozungumzwa yafanyiwe kazi na kupanga utekelezaji  wake. Mwenyekiti ameisha taarifiwa juu ya auamuzi huu.  Msingi wa mazungumzo yetu uliegemea zaidi athari ambazo Klabu yetu ingeezipata katika kipindi hiki kuelekea ligi Mzunguko wa pili na mchezo kati yetu na Mahasimu wetu YANGA katikati ya mwezi wa December pamoja na  athari  nyingine ambazo klabu yetu ingepata kimapato kupitia wadhamini  na wafadhili mbali mbali walio na mikata na wasio nayo, aidha wapenzi na wanachama wengi wasiopenda migogoro  wameamu kukaa mbali na Timu yetu viwanjani na nje ya uwanja, aidha wapenzi wengi wa Simba wamepoteza ujasiri wa kuizungumzia na kuitetea Klabu yao mitaani popote walipo kwa kuwa hawajui siku inayofuata kutatokea  jambo gani litakalo wakarahisha, kwa kuzingatia hayo yote ndio maana wajumbe wakaridhia mazungumzo ya kutafuta amani na umoja katika klabu yaendelee na sasa anasubiriwa mwenyekiti ili nae atumie busara zake kumaliza mvutano huu ambao kwa sasa umeisha fikia tamati kati ya 85%-90%.
    Kwa mujibu wa Katiba ya Simba Ibara 28(1)MUUNDO WA KAMATI YA UTENDAJI “Kamati ya Utendaji inaundwa na Mwenyekiti na Makamu Mwenyekiti na wajumbe waliochaguliwa  na Mkutano Mkuu pamaoja na wajumbe walioteuliwa”aidha ibara hiyo inasomeka pamoja na ibara ya 33(1)&33(3)a,b,c,d,e,f,g,h. Kwa mantiki hiyo bila Mwenyekiti hakuna Kamati ya Utendaji na Mwenyekiti bila wajumbe hakuna Kamati ya utendaji jambo ambalo lingepelekea Simba kusimsmisha shughuli zote kwani shughuli zote za Simba muhimu zitafanyawa na kuidhinishwa na kamati ya Utendaji kwa mujibu wa katiba ya Simba ibara ya 30(1)a,b,c,d,e,f,g,h,i,j,k,l,m.

    Aidha katika kuendeleza nia ya kuifanya Simba Moja nitajitahidi katika siku za hivi karibuni nikitane na wanachama wa  Matawi ambayo yanaonekana au kuhisiwa  kutokuwa na uhusiano mzuri na uongozi wa Simba kama (Mpira Pesa, Vuvuzela na mengine) ili kujua sababu za kutokuwa na mahusiano Mazuri na uongozi ili kutafuta suluhisho la kudumu na hatimae washirki katika shughuli za klabu na  kuifanya Simba Moja isiyokuwa na wanachama wenye matabaka kwa sabau yoyote ile.
    4. NINI WAJIBU WANGU KAMA MWANACHAMA WA SIMBA

    Wajibu wangu wa uwanachama kama walivyo wanachama wengine  ni wa hiari kwani kila mmoja wetu alichagua kuipenda Simba kwa hiari yake bila Shuruti lolote na bila kujali atapata nini kibinafsi aidha kimaslahi au kiuongozi zaidi ya furaha na maendeleo ya Simba, hivyo  kila mwanachama anawajibu kikatiba na kikanuni kuilinda , kuitumikia na kuiteteta klabu ili ifikie malengo bila kuvunja taratibu na misingi tuliojiwekea, inasikitisha kuona siku hizi kuna baadhi ya watu wako hiari kuona na kusababisha timu ifungwe eti tu kwa kuwa hampendi kiongozi Fulani aliyeko madarakani, hiyo haikubaliki na ninawaomba wanachama na wapenzi wa Simba ikiwa watambaini mtu wa aina hiyo Katika klabu yetu ashughulikiwe mara moja , kwani kuna watanzania wengi  na wapenzi mbali mbali wa Simba nje na ndani  ya Dar-es-salaam(MARA , MTWARA,MANYARA, SONGEA nk) ambao hawajui nini kinachoendelea hapa ila wanaumia sana timu inapofanya vibaya katika michezo mbalimbali. Kuhujumu klabu sio tu kwa kufungisha timu bali hatu kununua na kuuza  vifaa bandia vya michezo vinavyojitambulisha na klabu huku ukijua wazi  klabu haipati  mapato yoyote  wote hawa wanastahili adhabu sawa na stahiki, kutokana na matukio mbalimbali ya kujaribu kuondoa viongozi kabla ya muda wao wa uongozi  kuisha na bila mafanikio inapashwa kuwa somo tosha kwa wanachama kuwa makini wakati wa uchaguzi kuchagua viongozi wanaowafahamu uwezo wao bila kurubuniwa kwa zawadi na pesa ndogo ndogo, kwani katika mfumo wa dunia ya leo sio tu kwenye Siasa hata katika mpira kuanzi FIFA,CAF,TFF mapinduzi yamefutwa na hayakubaliki tena kwa sababu yoyote ambayo iko nje ya utaratibu wa kikatiba.
     Mwanachama unamchagua kiongozi awe madarakani kwa miaka 4 ambayo ni sawa na siku 1460, ukifanikiwa kuuza kura yako kwa Shs 50,000 wakati wa uchaguzi  ni sawa na kuuza na kulipwa shilling  34.24 kwa siku  ambayo haikutoshi hata nauli ya kuja mjini huko ni kuhujumu klabu  kama wengine, nawaomba wanachama wenzangu tuamke tutoke kwenye usingizi huo usioleta tija wala maendeleo na mwisho ni migogoro isiyokwisha katika klabu.
    5. NINI CHANZO CHA MGOGORO HUU  WA SIMBA NA ULAZIMA WA WANACHAMA  WA SIMBA KUINGIA KATIKA MGOGORO HUU.

     Baada ya kuongea na pande zote mbili katika mgogoro huu nimebaini sababu kubwa za mgogoro ni:
    (i) Mawasiliano(communication) hafifu ndani ya kamati ya utendaji jambo linalosababisha baadhi ya wajumbe kutokujua baadhi ya mambo
    (ii) Kukosekana kwa  Dira na mwelekeo (Vision) jambo linalofanya kamati ya utendaji wote au mmoja mmoja kukosa mwongozo wa kujua wapi klabu inaelekea.
    (iii) Kukosekana kwa uamuzi wa pamoja na uwazi (collective Decissions and Transparence)  katika baadhi ya  mambo katika uendeshaji wa klabu.
    (iv) Kukosa kuaminiana (Trust) miongoni mwa wajumbe wa kamati ya utendaji
    (v) Kukosekana kwa Kanuni (regulations) mbalimbali za uongozi na Utawala, usimamizi wa  Fedha, nk.
    (vi) Kukosekana kwa mafuzo, warsha , semina na kozi mbali mbali za utawala kwa kamati ya utendaji ili kila mmoja ajue wajibu na mipaka ya madaraka  yake katika Klabu.
    Baada ya kubaini  mapungufu hayo, niliona  hizi ni kasoro ambazo zinaweza kurekebishika ndani ya kamati ya utendaji yenyewe ikiwa pande zote zinaweza kukiri mapungufu haya na kutenga wasaa na rasilimali ili kuondoa kasoro  hizo.
    Kuhusu wanachama kuingilia mgogoro huu nina amini wanachama wana nafasi yao katika kuleta na kutatua migogoro mbalimbali, lakini katika mgogoro huu wa sasa ulikuwa kati ya mwenyekiti na Wajumbe wake wa Kamati ya Utendaji, hivyo ilikuwa mapema mno kwa wanachama kuingilia mgogoro huu kwa sababu bado ulikuwa ndani ya uwezo wa kamati ya utendaji ya Utendaji ya  Simba.

    6. UTAYARI WA PANDE MBILI ZINAZOPINGANA KURUDI KATIKA MEZA YA MAZUNGUMZO

    Baada yakuwasiliana na kukutana na pande zote mbili za mgogoro huu, ninapenda kuzishukuru kwa kukubali kukutana ili kumaliza tofauti zao, ni wazi kwenye usuluhishi ni lazima pande zote zitapata na kupoteza kiasi cha matarajio yake sio rahisi upande mmoja ukapata ilichohitaji yenyewe kwa 100% hivyo ni wazi pande zote  kwa kuzingatia umuhimu wa mapatano kwa mustakabali wa Simba Watakaa na kukubaliana kuondoa tofauti zao na kisha kila pande utafuata na kuheshimu  katiba na kanuni kama muongozo katika kufanikisha malengo ya Simba, mwisho wa usuluhishi hakuna upande utakao kuwa umeshinda au kushindwa isipokua Simba  ndio itashinda, ni imani yangu watatambua nje ya Simba hakuna aliyemaarufu miongoni mwao, na pia nana penda kuwashauri wapambe wa pande zote kujiepusha na kutoa  maneno ya kuudhi na kejeli kwa upande mwingine ili kujenga umoja katika Simba.

    7. ATHARI ZA MUDA MFUPI NA MREFU KWA KLABU YA SIMBA  KWA KUREJEA MIGOGORO MBALI MBALI ILIYO WAHI  KUTOKE KATIKA SIKU ZA NYUMA.

    Mgogoro wowote una matokeo Chanya au Hasi (+ve or –ve results) wakati mwingine migogoro imesaidia kuwakumbusha watawala umuhimu wa kuwatawala watawaliwa  kama walivyo kubaliana kupitia Katiba lakini wakati mwingi migogoro inaishia kuboma kama ilivyo kuwa kwa Yanga kuzaliwa Pan Africa na kwa Simba Kuzaliwa Red Star, hivyo ni jukumu la wahusika kupima kabla ya kuingia katika mgogoro juu ya matokeo yake ya mwisho, kumbukumbu zangu zinanionsha hakuna kiongozi aliyewahi kupita Simba bila migogoro kutokea na hakuna hata mgogoro mmoja uliowahi kuleta matokeo chanya zaidi ya kurudisha nyuma maendeleo ya simba, baadhi ya migogoro ilipelekea hadi  baadhi ya viongozi kupoteza maisha(marehemu Mzee Juma Salum na mhasibu wa Simba)  wakiwa safarini wakijaribu kumaliza mgogoro, baadhi ya viongozi wa Simba waliokutana na  migogoro ni  pamoja na Mzee Hassan Brashi,Marehemu Ngonya, Marehemu mzee  Bamchawi,Mzee Hazali,Mzee Chamshama, Mzee Dalali na wengine wengi ambapo migogoro yote hiyo haikuisaidia  wala kuleta tija kwa Simba, kuna wakati Simba ilikaa karibu  ya miaka mitatu bila ya kuwa na uongozi wa kuchaguliwa Kisheria. Hivyo ni wajubu wa wana Simba tupime na tuamue kama mgogoro huu una tija hasa ukizingatia muda wa uongozi huu inaishia mwezi wa 5(may) 2014 na uchaguzi kufanyika, rai yangu kwa wanasimba kufikiria, kumpima na kutafakari ni kiongozi gani tuna muhitaji kutaongoza kwa miaka 4 ijayo kuanzia 2014 badala ya kusinzia na kuamka wakati wa uchaguzi na kuchagua mtu asiye sahihi na baada kujaribu  kumng’oa kwa kupitia mlango wa nyuma, “mke mzuri hupewa na mwenyezi Mungu ila kiongozi mbovu humchagua wewe mwenyewe na mungu hukubariki ukae nae kwani umemchagua mwenyewe kwa hiari yako”.

    8. KINA NANI HASA WATAKAOFAIDIKA ZAIDI NA MGOGORO HUU (VIONGOZI WA SIMBA, WANACHAMA WA SIMBA, KLABU YA SIMBA  AU WAPINZANI WA SIMBA)

    Kimsingi wanaoipenda na kuitakia mema Simba hawawezi kwa njia moja au nyingine kufurahia migogoro ya Simba kwani inatia maudhi na kukatisha tamaa ninaamini hata wanachama wengi binafsi hawapendi  hali hii, ila kuna baadhi ya watu wachache hawasemi ila wanafaidika binafsi  kimapato na hali ilivyo sasa na wakati mwingine wa migogoro, viongozi wa Simba hawana faida na migogoro hii kwani inawafanya washindwe kufanya kazi waliyowaahidi wapiga kura wao wakti wa uchaguzi.
    Wanaofaidika kwa kiwango kikubwa na mgogogro wetu ni mahasimu na wapinzani  wetu kwani wana hakika bila umoja, mshikamano na upendo hatuwezi kuwa na timu ya Ushindani, hivi sasa timu yetu iko nafasi ya 4 mgogoro huu ukiendelea unaweza kutupeleka pabaya zaidi hata kufika kushuka daraja, wanaokumbuka historia ya Simba  wakati wa Marehemu J.D.Ngonya, tuliwahi kuponea kushuka daraja mechi ya mwisho ya ligi sababu ya migogoro, na wakati ule upinzani haukuwa mkali kiuchumi na kimiundombinu ya mpira  kama wakati huu,  hivyo wana Simba tusitumiwe na kutumia mikono yetu wenyewe kuivunja klabu yetu, tupambane na adui wa nje halafu ndio tuulizane wenyewe tukiwa ndani hakuna haja ya kuchochewa na maadui zetu na kisha



     kuyatangaza matatizo yetu hadharini halafu tunaona ujiko, sifa na ufahari, hii ni hatari kwa Klabu hasa katika biashara kwa maana ya uwekezaji na udhamini kwani  hakuna mfanyabiashara anayependa kuwekeza mahali kwenye fujo na kusiko na utulivu.

    9. NAFASI YA TFF KATIKA KUTATUA NA KUPATIA UFUMBUZI WA MGOGORO HUU.                                                                                                                        Simba ni mwanachama wa TFF ambapo TFF ni mwanachama wa FIFA, kimsingi  chombo kikuu kinachosimamia Mpira wa Miguu hapa nchini ni TFF hivyo katika mfumo wa uongozi na uendeshaji wa mpira duniani kila nchi ina chombo kinacho tambuliwa na FIFA katika kusimamia mpira wa miguu katika nchi mwanachama hivyo kwa Tanzania ni  TFF , kwa mantiki hiyo kupingana na TFF kunaweza kuleta hatari na madhara makubwa zaidi kwa Simba, kwani TFF haiwezi kuifutia Simba usajili wake ila inaweza kuisimamisha au kuifukuza uanachama  pale inapoona inapingana na maamuzi yake, mfano  ulitokea kwa Tanzania kufungiwa na FIFA 2000 baada ya kukataa maagizo ya FIFA japo wakati huo FAT ilikuwa na katiba yake, mwaka 2004 Fifa ilifupisha kipindi cha uongozi wa FAT kutoka miaka 4 hadi 3 kwani uchaguzi ulikuwa ufanyike 2005 kama katiba ya FAT/TFF ilivyo kuwa inaelekeza, hivyo sio busara kwa Simba ambaye ni mwanachama wa TFF kupingana nayo,Katiba ya Simba Ibara ya 11(1)f  inazungumzia Wajibu wa Mwanachama “Asiwe na uhusiano wowote wa kimichezo na wanachama waliosimamishwa au kufukuzwa” na hata katiba ya  TFF  inacho kifungu hicho hivyo Simba inaweza kujikuta katika kisiwa ikiwa itatengwa na TFF.                                                                                                         Kwa kuwa suluhisho linaelekea kupatika ni matarajio yangu kuishirikisha TFF katika kufikia makubaliano na kusimamia utekelezaji wa makubaliano ya suluhu .                   Ni matumaini yangu wahusika watanielewa kwani huu ni mtazamo wangu binafsi bila kushauriwa na upande wowote na  ambao hauna lengo la kuusaidia upande wowote wa mgogogoro huu zaidi ya kuzingatia maslahi na mustakabali wa Simba Sports Club kwa Sasa na kwa siku zijazo, ni matumaini yangu Viongozi na Wanachama wa Simba watachukulia maoni haya kama changamoto na sio vinginevyo, na kwa wale ambao wengependa kuhukumu basi vyema kwanza kuzingatia yafuatayo i): Laws(sheria zilizopo),ii) Evidence(Ushahidi uliopo) na  Iii) Facts of the matter(Uhalisia wa jambo).  
    MUNGU IBARIKI SIMBA, MUNGU IBARIKI TANZANIA. AHSANTENI
    Michael Richard Wambura.                                                                          
    Nakala:                                                                                                                 :Mwenyekiti Simba Sports club                                                                                              
    :Rais- TFF                                                                                                                                                   :Wajumbe Kamati ya Utendaji SIMBA
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MICHAEL WAMBURA: WATU WANADHANI NIMETEULIWA SIMBA KUMLINDA RAGE,LAKINI... Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top