• HABARI MPYA

    Saturday, November 30, 2013

    KENYA WAOTEA VIBONDE, WAWACHAPA 3-1 NYAYO

    Na Mahmoud Zubeiry, Nairobi
    KENYA imeshinda mechi ya kwanza Kombe la Mataifa ya Afrika Mashariki na Kati, CECAFA Challenge baada ya kuilaza Sudan Kusini mabao 3-1 kwenye Uwanja wa Nyayo, Nairobi jioni hii katika mchezo wa Kundi A.
    Ushindi huo unaifanya Harambee Stars ifikishe pointi nne baada ya awali kutoa sare ya bila kufungana na Ethiopia katika mchezo wa ufunguzi.
    Joackins Atudo aliifungia Kenya bao la kwanza dakika ya 16 kwa penalti, baada ya beki mmoja wa Sudan Kusini kuunawa mpira kwenye eneo la hatari.
    Wachezaji wa Kenya wakimpongeza mfungaji wa bao lao tatu, David Owino leo Nyayo

    Sudan Kusini ilisawazisha dakika ya 26 kupitia kwa Nahodha wao, Richard Jistin aliyepiga shuti kali la mpira wa adhabu umbali wa mita 25 ambalo lilimshinda kipa Duncan Ochieng.
    Jacob Keli aliifungia Harambee bao la pili dakika ya 29 akiunganisha krosi ya Allan Wanga kutoka upande wa kulia.
    Atudo alikosa penalti dakika ya 70, baada ya kipa wa Sudan Kusini, Juma Jinaro kumuangusha Jacob Keli akiwa anakwenda kufunga. 
    David Owino aliifungia Harambee bao la tatu dakika ya 78 baada ya kuwatoka mabeki wa Sudan Kusini.   
    Matokeo haya yanamaanisha Kenya na Ethiopia sasa zinalingana kwa kila kitu, pointi nne kila mmoja, mabao matatu ya kufunga na bao moja la kufungwa, wakati Zanzibar sasa ni ya tatu kwa pointi zake tatu na Sudan Kusini inashika mkia.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: KENYA WAOTEA VIBONDE, WAWACHAPA 3-1 NYAYO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top