• HABARI MPYA

    Sunday, April 22, 2012

    UTUMBO NI MWINGI, LAKINI YANGA WATULIE WAJITATHMINI, VINGINEVYO...


    Kikosi cha Yanga msimu huu

    NI maajabu tu ambayo sasa yataifanya klabu  bingwa Tanzania ipate nafasi ya kucheza michuano ya Afrika mwakani, baada ya kupoteza pointi tisa mfululizo dhidi ya Coastal Union, Toto African na Kagera Sugar.
    Tayari Yanga imekwishavuliwa ubingwa wa Ligi Kuu, kutokana na watani wao wa jadi, Simba SC kutimiza pointi 56 ambazo hawawezi kuzifikia.
    Nasema maajabu kwa sababu, Yanga inabidi ishinde mechi zake zote zilizobaki wakati Azam inayohitaji kushinda mechi moja tu, ili kupata tiketi ya kucheza Kombe la Shirikisho mwakani, ifungwe mechi zote zilizobaki.
    Hakuna lisilowezekana chini ya jua, lakini sitaki kusadiki kama Azam wanaweza kuwa wazembe kiasi hicho na kupoteza nafasi hii adhimu waliyonayo hivi sasa.
    Gumzo kubwa baada ya  matokeo haya mabaya ya Yanga ni uongozi mbovu, uongozi haufai.
    Wengi wametoa maoni yao, Mwenyekiti wa Yanga Wakili Lloyd Baharagu Nchunga ajiuzulu na Kamati yake nzima ya Utendaji.
    Wanaamini hilo ndilo suluhisho- lakini ukizama ndani, wengi wanaotoa maoni hayo wana hasira kutokana na matokeo mabaya na hawataki kujadili tatizo la msingi la Yanga kukosa nafasi ni nini.
    Kwa muda mrefu, binafsi nimekuwa nikililia ligi yenye ushindani, ambayo naamini ndiyo itakuza soka letu- sasa sioni kwa nini leo nisifurahi dalili za ushindani zinaanza kulingana na hali halisi ilivyo.
    Simba bado haijawa bingwa- bali tu imekwishajihakikishia kucheza tena michuano ya Afrika mwakani na ili wawe mabingwa, wanatakiwa kumaliza biashara na si kubweteka.
    Matokeo ya mwaka huu, dhahiri yatawafanya vigogo wa soka ya nchi hii, Simba na Yanga kama kweli wanataka kuendelea kutamba katika ligi hiyo, wajipange.
    Wajipange kwa maana ya kutengeneza timu nzuri, kufanya maandalizi mazuri na kuwa makini katika uchezaji wa Ligi, kuhakikisha wanakuwa kwenye nafasi nzuri wakati wote.
    Ligi ya aina hii ndiyo ambayo itawafanya wachezaji wetu wawe na viwango vizuri, hivyo kutusaidia hata kupata timu nzuri ya taifa.
    Lakini hiyo ni kama tu matokeo ya uwanjani yanakuwa halisi na hayatokani na biashara ya kununua mechi- kwa sababu tunakuwa tunajidanganya eti tuna ligi ya ushindani, wakati ni ligi ya rushwa.
    Ligi ya rushwa itabadilisha mabingwa na hata Yanga watakosa ubingwa, lakini haiwezi kusaidia kukuza soka yetu.
    Ni wajibu wa kila mmoja kujitazama mara mbili na kuhakikisha anachangia maendeleo ya soka katika njia halali, ambazo ndio suluhisho la kweli.

    MAZOEA YANA TABU:
    Watu wamezoea ama bingwa Yanga, au Simba au mojawapo ya timu kushika nafasi ya pili na kwa sababu hiyo, matokeo ya mwaka huu yamekuwa shubiri.
    Hata wakubwa nao sasa vichwa vinawauma, kwa sababu Azam haiwezi kuvuta malefu ya mashabiki uwanjani hata ikicheza na bingwa wa Afrika.
    Hivyo ule mgawo wanaopata kutokana na mechi, utashuka mno. Hilo lazima wakubwa liwaumize sana tu kwa Yanga kukosa mechi za Afrika mwakani.
    Lakini wana Yanga pia, hao ndio walioumia zaidi kutokana na matokeo haya, kwa sababu ni timu yao wanaipenda na wanapenda ing’are. Iko wapi sasa?
    Kwa sababu hiyo wanaona wa kuwatupia lawama au kuwatoa kafara na viongozi wao.
    Sina uhakika kama hii ni sahihi, lakini napenda niseme sikatai uongozi wa Yanga una matatizo na unahitaji kujitazama mara mbili kama kweli unataka kuiletea maendeleo klabu.
    Kuna dalili za kutosha sana kwamba uongozi wa Yanga haujiamini na hauna mipango- zaidi kuna watu ndani ya Kamati ya Utendaji wapo kwa maslahi yao binafsi tu.
    Sitaki kuzama ndani juu ya hilo, kwa sababu si mada yangu kwa leo- ila nataka kuwaambia wana Yanga huu si wakati mwafaka kunyoosheana vidole, kwa sababu ligi haijaisha.
    Yanga wanahitaji kutulia kumalizia ligi na baada ya hapo sasa wafanye tathmini ya kina, watafute walikosea wapi na  ndipo wachukue hatua.
    Hawapaswi kuchukua hatua kwa shinikizo la kupagawa na matokeo, bali wafanye tathmini ya kina kabisa juu ya kile au yale yaliyosababisha matokeo haya msimu huu.
    Baada ya kuchukua ubingwa wa Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati Julai mwaka jana, wengi waliamini Yanga itakuwa tishio msimu huu.
    Lakini hali imekuwa tofauti, Yanga imekuwa kibonde msimu huu- kwa nini?
    Haya ni mambo ambayo Kamati ya Utendaji ya Yanga wanatakiwa kujiuliza, tena kwa utulivu wa hali ya juu na si kukurupuka.
    Yanga iliuanza msimu na kocha Mganda, Sam Timbe ambaye aliwapa Kombe la Afrika la Mashariki na Kati na ubingwa wa Ligi Kuu msimu uliopita, lakini baada ya mechi tatu ikamfukuza na kumrudisha Mseriba Kostadin Papic.
    Haya yalikuwa maamuzi sahihi? Kamati ijiulize. Seif Ahmad ‘Magari’ anasemaje sasa baada ya kumfukuza Timbe, kocha asiyeshaurika na asiyependwa na wachezaji, lakini aliyeleta mataji na kumleta Papic kocha anayeshaurika na kupendwa na wachezaji aliyeiporomosha timu hivi sasa?
    Napenda nieleweke sana hapa- matatizo ya uongozi katika sekta za michezo Tanzania hayataisha leo kutokana na mifumo mibovu- lakini bado hayaingiliani na matokeo mabaya.
    Fikra za viongozi wa Simba na Yanga zinaishia kwenye kusimamia timu kwa ajili ya Ligi Kuu tu na hizo mechi mbili tatu za michuano ya Afrika- hawana mtazamo wa mbali zaidi ya hapo.
    Tusahau kuzifanya timu zao kuwa zenye mihimili madhubuti kama Tout Puissant Mazembe iliyo midomoni mwetu, lakini hata kufanya vizuri kwenye Ligi iwe tatizo?
    Kushuka kwa nidhamu ya wachezaji sambamba na viwango vyao- kocha asiyejali aliyethubutu kumchezesha mechi mchezaji mwenye kadi nyekundu- yote haya yaangaliwe kwa kina. 
    Kocha ambaye kumbukumbu zinaonyesha aliwahi kumpanga kipa aliyekuwa majeruhi, Obren Curkovic katika mechi ngumu dhidi ya watani wa jadi Simba, Yanga ikafungwa 4-3.
    Kila napozikumbuka baadhi ya mechi za Simba na Yanga nilizowahi kuziona- huwa nayakumbuka mabao aliyokuwa akifungwa Obren siku ile- hasa lile la nne lililofungwa Hillary Echesa kutoka katikati ya Uwanja.
    Siwezi kumlaumu Obren, alikuwa majeruhi na hakutaka kucheza ila kocha asiyejiamini na asiyewaamini wachezaji wake alimlaizmisha kucheza.
    Kocha asiyemkubali kiungo aliyetoa krosi ya bao la ushindi katika fainali ya Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati, Rashid Gumbo hakuona hatari ya kumpanga kipa asiye fiti.
    Yanga aliyoiacha Profesa Duisan Savo Kondic ilikuwa kali mno, lakini alihujumiwa na wenye timu walipomchoka ili aondoke na akaja kocha anayefanana na rais wa zamani wa Marekani. Yanga kunani sasa?
    Namkumbuka Stephen Bengo, eti aliachwa Yanga na Papic- na Mrisho Ngassa aliuzwa Azam FC kwa sababu klabu, chini ya Mserbia huyo ilikataa kuboresha mkataba wake.
    Arsene Wenger aliamua Fabregas, Nasri waondoke kwa sababu ana misingi ya kupandisha nyota wengine kutoka kwenye akademi, Yanga wana nini?
    Ni mfululizo wa matatizo mengi, ambayo Yanga walijitakia na haya ndio matunda yake- ila suluhisho si mtu kujiuzulu. Naamini viongozi wa Yanga wamepata fundisho. Sasa wakae chini, wafanye tathmini na waibuke na sera na mikakati mipya, ambayo itairudisha Yanga kwenye michuano ya Afrika mwaka 2014 ikiwa timu ya ushindani.
    Alamsiki.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    2 comments:

    Anonymous said... April 22, 2012 at 12:43 PM

    Ni kweli utumbo ni mwingi YANGA. lakini kuna kitu umesahau UTUMBO NI MWINGI SANA KWA BIN ZUBERI. wewe ni utumbo!!! na waaandishi aina yako ndo wameifikisha yanga hapo ilipo!UNAZI unatumia kalamu yako kutetea utumbo wa viongozi. ulijitahidi sana kuichafua kamati ya ligi. ionekane inaionea yanga. wakati ulikua unajua wazi kwamba yanga walikosea kumchezesha kanavaro. Lakini kwa sababu ya njaa, au unazi, au UKANJANJA. uliamua kuivua nguo kamati nzima. ukitoa mifano ya kijinga ili tu yanga warudishiwe point ambazo si halali kwao. Leo bila aibu un arudi na kusema utumbo mwingi yanga. Mimi ninasema waandishi aina yako ndo mnaharibu yanga. acha njaa

    Mahmoud Bin Zubeiry said... April 22, 2012 at 2:38 PM

    Asante sana mdau. Nimepost maoni yako ili na wengine wakupime. Ninashukuru kwa matuso yako, kwangu ni sehemu ya changamoto za kazi. Bin Zubeiry.

    Item Reviewed: UTUMBO NI MWINGI, LAKINI YANGA WATULIE WAJITATHMINI, VINGINEVYO... Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top