• HABARI MPYA

    Tuesday, April 10, 2012

    SAMATTA, OCHAN WAREJEA SIMBA SC

    Samatta
    MBWANA Ally Samatta na Patrick Ochan watakutana tena na wachezaji wenzao wa zamani, viongozi wao- kwa ujumla na timu ya zamani, Simba SC.
    Katika kuhakikisha Simba inazidi kuimarika kwa michuano ya Kombe la Shirikisho Afrika, mfanyabiashara maarufu na mwanamichezo Azim Dewji anakusudia kuileta nchini timu ya soka ya TP Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), kwa ajili ya kuipa makali Simba kabla ya
    wawakilishi hao wa Tanzania hawajaivaa Al Ahly Shandy ya Sudan.
    Dewji aliyeifadhili Simba kwa miaka mingi, alisema jana Dar es Salaam kuwa ziara inaratibiwa na kampuni yake ya Simba Trailers na kwamba
    ameshazungumza na kuafikiana na Rais wa Mazembe, bilionea Moise Katumbi Chapwe na pia uongozi wa Simba.
     “Pamoja na kuwazawadia pesa wachezaji wa Simba, nimeona nitoe mchango zaidi kwa kuwaletea mechi ya kujipima nguvu na timu bora ya Mazembe ya
    Kongo,” alisema Dewji aliyetoa sh milioni 15 kwa Simba baada ya kuitoa ES Setif ya Algeria.
    Kwa mujibu wa Dewji, mchezo baina ya Mazembe na Simba unatarajiwa kufanyika Aprili 22 mwaka huu jijini Dar es Salaam, ikiwa ni wiki moja kabla ya `Wekundu wa Msimbazi’ kuumana na Al Ahly.
    Alisisitiza kuwa, Mazembe itakuwa kipimo sahihi kwa Simba kutokana na kuwa na kikosi chenye hadhi ya juu.
    Mazembe iiliyotwaa ubingwa wa Afrika mara nne, ikiwa pamoja na mwaka 2009 na 2010 kabla ya kuondolewa mashindanoni mwaka jana kutokana na
    dosari katika usajili wake, inajivunia utajiri mkubwa wa fedha na vipaji vya mastaa kama Muteba Kidiaba, Tresor Mputu, Given Singuluma, Stoppila Sunzu, Rainford Kalaba, Patrick Ochan na washambuliaji raia
    wa Tanzania, Mbwana Samata na Thomas Ulimwengu.
    Licha ya kutikisa katika Ligi ya Mabingwa Afrika katika miaka ya hivi karibuni, Mazembe pia ilitamba katika Klabu Bingwa wa Dunia mwaka 2010 huko Japan ambako ilifika fainali, hatua ambayo haikuwahi kufikiwa na klabu yoyote ya Afrika katika michuano hiyo.
    “Kupambana na kikosi bora kwa Afrika wakati kama huu itakuwa bahati kubwa kwa Simba, tuombe Mungu mambo yote yaende vizuri ili wawakilishi
    wetu wanoe makali ya kuitikisa zaidi Afrika katika Kombe la Shirikisho,” alisema.
    Wakati Simba imetinga raundi ya tatu kwa kuing’oa Setif kwa faida ya bao la ugenini, baada ya sare ya jumla ya 3-3, Al Ahly Shandy imeitupa nje ya michuano ya mwaka huu Ferroviario ya Msumbiji kwa jumla ya mabao 3-0.
    Mshindi baina ya Simba na Al Ahly Shandy atatinga hatua ya Nane Bora ambayo timu nne kuchuana katika kila kundi kusaka tiketi ya nusu fainali.
    Nayo Mazembe, licha ya kujipima na Simba kwao itakuwa fursa ya kuongeza makali ya kushiriki katika Ligi ya Mabingwa Afrika, kwani nayo imesonga mbele baada ya mwishoni mwa wiki kuifumua Power Dynamos ya Zimbabwe kwa 6-0. Timu hizo zilifungana 1-1 katika mchezo wa kwanza huko Harare, Zimbabwe.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SAMATTA, OCHAN WAREJEA SIMBA SC Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top