• HABARI MPYA

    Tuesday, April 10, 2012

    KANUMBA ALAZWA MILELE, HAIJAWAHI KUTOKEA TANGU NYERERE

    Jeneza lake likishushwa kaburini
    Jeneza lake likishushwa kaburini
    Mama Kanumba kushoto akiwasili makaburini akisaidiwa na Asha Baraka
    Jeneza lake likipelekwa makaburini
    MWILI wa nyota wa filamu Tanzania, mareheumu Steven Charles Kanumba, aliyefariki dunia usiku wa kuamkia Jumamosi umezikwa jioni hii makaburi ya Kinondoni, Dar es Salaam, baada ua kuagwa viwanja vya Leaders, Kinondoni.
    Umati mkubwa wa watu ambao haujawahi kuonekana kwenye mazishi tangu kifo cha marehemu baba wa taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere Oktoba 1999, ulihudhuiria mazishi hayo kuanzia kwenye kuagwa Leaders.
    Watu wengi walizimia na kupoteza fahamu. Ilikuwa majonzi huzuni na vilio vya kila namna.
    Mke wa Rais Jakaya Kikwete, Mama Salma Kikwete na Makamu wa rais Dk Ghalib Mohamed Bilal ni miongoni mwa viongozi wa serikali waliohudhuria.
    Lakini pia viongozi wa vyama vya siasa, dini na asasi nyingine za kijamii, ikiwemo michezo, sanaa na burudani walifika.
    Jeneza la marehemu lilibebwa na wasanii wenzake waliokuwa wamevalia nadhifu. Huruma kwa mama wa marehemu, Florence Mtegoa aliyekuwa akisaidiwa na Asha Baraka.
    Hakika kwa ujumla ni huzuni. Huzuni kubwa. Wengi hawaamini kama Kanumba ameondoka na leo hii ndio alipumzishwa katika nyumba yake ya milele,
    Kanumba amebaki Kinondoni. Hatutamwona tena. Tutabaki kumuangalia kupitia filamu zake nzuri, ambazo daima zitatamba na kufanya vizazi na vizazi vimjue, alikuwa nani.  
    Kanumba alifariki dunia ghafla usiku wa kuamkia Jumamosi na chanzo cha kifo chake inaelezwa ni kugombana na mpenzi wake, mwigizaji mwenzake, Lulu.
    Imeelezwa Lulu alikuwa anazungumza na simu na Kanumba akataka kujua anaongea na nani.
    Lulu hakutaka kumpa simu Kanumba na ndipo wakaanza kuvutana na mwenzake akadondoka chini.
    Inaelezwa alidondokea kisogo katika eneo gumu na ndipo hali ikawa mbaya kabla ya kifo chake. 
    Lulu bado anashikiliwa kituo cna Polisi Oysterbay, Dar es Salaam.

    AMEACHA NINI?
    STEVEN Charles Kanumba alikuwa anamiliki kampuni ya Kanumba The Graet Film, iliyokuwa na maskani yake eneo la Sinza Meeda.
    Kampuni hiyo, iliyokuwa imeajiri watu watano, ambao ni Zakayo, Kiullo, Sethi, Biggie, Junior, Mya na dada mwingine wa mapokezi, ambaye jina lake halikuweza kupatikana mara moja.
    Meneja wa kampuni hiyo, inayojihusisha na utayarishaji wa filamu, Mayasa Mrisho ‘Mya’ amefanya mahojiano na bongostaz mchana huu juu ya mustakabali wa kampuni hiyo, baada ya kifo cha marehemu.
    Katika mahojiano hayo, Mya anasema kwamba kampuni iko vizuri na inaweza kuendelea na kazi, lakini wanasubiri familia ya marehemu waamue.
    “Sisi ni wafanyakazi, ila kampuni ipo na inahitaji muendelezaji tu, wafanyakazi wapo na wenye uzoefu wa kutosha, sisi tutasubiri tamko la familia ya marehemu tujue mustakabali wetu,”anasema Mya.
    Mya ambaye alimpokea Kanumba katika kundi la Kaole mwaka 2002, anasema kwamba binafsi kwake kifo cha msanii huyo ni pigo mara mbili.

    PATO LA MAREHEMU NA TAARIFA ZA FEDHA:
    Mya hajui kampuni ilikuwa inaingiza kiasi gani japo kwa mwezi, lakini pia hafahamu zaidi kuhusu sehemu ambazo Kanumba alikuwa akiweka fedha zake au fedha za kampuni.
    “Kwa watu ambao tunatakiwa tunawalipa tulikuwa hatulipi kwa cheki, (Kanumba) alikuwa ananipa fedha cash nalipa watu. Yaani mishahara nini au hata kama malipo yote kwa niaba ya kampuni,”anasema Mya.
    Lakini Mya anasema anakumbuka marehemu alikuwa mteja wa benki ya NBC na benki nyingine.
    Ni kiasi gani cha faida walikuwa wanatengeneza kwa filamu moja?
    “Mmh! Sijui,”anasema Mya. “Hiyo ni siri yake mwenyewe na tulikuwa hatumuingilii,”.
    Lakini uchunguzi wa bongostaz umegundua katika kila filamu moja iliyokuwa ikiingia sokoni ya Kanumba kwa takriban miaka miwili sasa, kama alilipwa kidogo ni Sh. Milioni 20.
    Kwa miaka miwili Kanumba amekuwa akifanya kazi na kampuni ya Steps Entertainment Limited iliyo chini ya Mkurugezni wake Dilesh Solanki.
    Siku za mwanzoni, Kanumba alikuwa anaingiza filamu mpya kila mwezi sokoni ingawa sasa utaratibu umebadilika na filamu moja ilikuwa kila baada ya miezi miwili au mitatu.
    Jitihada za bongostaz kuzungumza na Dilesh leo hazikuzaa matunda. “Tafadhali naendesha gari na leo niko bize sana hatuwezi kuzungumza, labda umpigie msaidizi wangu Jay,”alisema Dilesh alipopigiwa simu na bongostaz kuzungumzia kuhusu Kanumba.
    Jay hakupatikana alipopigiwa simu, na Mya anasema kwamba Kanumba alikuwa anapata fedha pia mikataba ya matangazo ya biashara aliyokunayo.
    “Kwa sasa nayojua ni tangazo la Oxfam, Zantel na Star Times,”anasema.

    MKE, MCHUMBA, MTOTO?
    Mya anasema yeye kwake Kanumba alikuwa zaidi ya bosi kazini, alikuwa kama ndugu yake na wote kila mmoja alikuwa ana siri za ndani za mwenzake.
    “Mimi nina siri nyingi za Kanumba na yeye ana siri zangu nyingi, yaani alikuwa zaidi ya bosi pale kazini,”anasema Mya.
    Je, Mya anafahamu chochote kuhusu Kanumba alikuwa ana mototo? “Kwa kweli katika siku zote za kuwa na Kanumba, tangu tukiwa Kaole hadi anakutwa na umauti, sijawahi kusikia akiniambia habari za kuwa na mototo.
    Sijui. Na sidhani kama angekuwa ana mtoto asingeniambia,”anasema Mya.
    Kuhusu mchumba au mwenza wa Kanumba katika maisha yake, Mya alikataa kuzungumzia hilo. “Hilo kwa kweli siwezi kuzungumzia hata kidogo,”anasema.
          
    ZAIDI YA NYUMBA YA KUPANGA?
    Mauti yamemkuta Kanumba alikuwa anaishi kwenye nyumba ya kupanga Sinza Vatican, aliyohamia takriban mwaka mmoja kutoka kwao Tandika alipokuwa akiishi.
    Je, Mya anafahamu kama Kanumba alikuwa ana nyumba au alikuwa anajenga sehemu yoyote?
    “Ndiyo,”anasema Mya. “Kanumba alikuwa anajenga nyumba nzuri na ya kifahari Mbezi ya Kimara, ambayo ilikuwa inakaribia kuisha masikini,”anasema.

    KAZI ZILIZO JIKONI:
    Mya anasema kwamba Kanumba anafariki dunia, wakati filamu yake moja iitwayo Ndoa Yangu ikiwa njiani kuingia sokoni.
    “Hii nafikiri itakuwa imeshalipwa na ni Steps hao hao ndio wanaiuza. Ni filamu moja kali sana kwa kweli, nafikiri itaingia sokoni mwezi huu,”anasema Mya.
    Lakini pamoja na hiyo, Mya anasema kuna filamu nyingine ambayo rasmi hiyo ndio itakuwa picha ya mwisho Kanumba.
    Hiyo ni Mr Price ambayo kwa sasa inafanyiwa editing na ilitakiwa kuingia sokoni baada ya Ndoa Yangu.
    HISTORIA YAKE:
    Steven Charles Kanumbaa alizaliwa Januari 8, mwaka 1984 mkoani Shinyanga kabla ya umauti kumfiia Aprili 6, mwaka 2012.
    Elimu ya msingi alipata katika shule ya Bugoyi, na baadaye akajiunga na  sekondari ya Mwadui, kabla ya kuhamia Dar Christian Seminary.
    Baada ya kumaliza Kidato cha Nne Dar Christian, Kanumba alijiunga na sekondari ya Jitegemee, Dar es Salaam pia kwa elimu ya Kidato cha Tano na Sita.
    Ni ni wakati huo akiwa Jitegemee Kanumba alianza shughuli za sanaa katika Kundi la Kaole Sanaa Group la Magomeni, Dar es Salaam.
    Baada ya kukomaa Kaole, Kanumba aliamua kuanzisha kampuni yake mwenyewe ya filamu na hadi anakutwa na umauti alikuwa mwigizaji anayefahamika Afrika nzima.
    Ameshirikiana na wasanii wakubwa duniani kama Ramsey Nouah wa Nigeria na amefanya kazi na mastaa wengine kadhaa wa Nigeria.
    Miongoni mwa filamu ambazo alifanya ni Dar To Lagos, She is My Sister, Ancle JJ, Oprah, Tufani, Johari, Gharika, Baragumu, Sikitiko Langu, Dangerous Desire, Cross My Sin, Village Pastor, Family Tears na kadhalika.
    Hivi karibuni, alikaririwa akisema atagombea Ubunge katika uchaguzi mkuu ujao wa mwaka 2015.
    Kanumba atakumbukwa na wengi sana kwa ucheshi wake- upole na ushirikiano mzuri na wenzake katika kazi.
    Kifo cha Kanumba ni pigo katika tasniya ya filamu Tanzania. Taifa limempoteza mtu ambaye alikwishaanza kuitangaza vema nchi kupitia sanaa hiyo na ambaye angetarajiwa kuitangaza zaidi katika anga za kimataifa zaidi kupitia sanaa hii.
    Nigeria sasa wanajua Tanzania sasa filamu. Nchi nyingi za Afrika zinajua sasa nah ii sehemu ya kazi nzuri kwa Kanumba.
    Mwenyewe aliwahi kukaririwa alifika hadi Hollywood hadi Marekani, ambayo ni ‘makka’ ya wacheza filamu. Kwa sasa mwili wa marehemu upo katika hospitali ya Taifa ya Muhimbili, Dar es Salaam.
    Mama Kikwete
    Mungu aiweke pema peponi roho ya marehemu. Amin.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: KANUMBA ALAZWA MILELE, HAIJAWAHI KUTOKEA TANGU NYERERE Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top