• HABARI MPYA

    Saturday, January 24, 2009

    JKT RUVU YAIBWAGA AZAM DAR


    Akiwa mwenye mawazo na majonzi baada ya timu yake kulala 2-0 mbele ya Simba wiki iliyopita, ni Kocha wa Villa Squad, Kenny Mwaisabula ambaye Jumapili tena timu yake inashuka dimbani kumenyana na Polisi Moro kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.



    JKT Ruvu leo Jumamosi ilitoka kifua mbele kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam baada ya kuilaza Azam FC mabao 2-1 katika mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, uliofanyika kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
    Hadi mapumziko, timu hizo zilikuwa zimekwishafungana 1-1, Azam ikitangulia kupata bao kwa mkwaju wa penalti, uliopigwa na kiungo Shekhan Rashid, dakika ya 30 baada ya beki mmoja wa JKT kuunawa mpira uliopigwa na Mganda, Dan Wagaruka kwenye eneo la hatari.
    Haruna Adolph aliisawazishia JKT dakika ya 43, bao lililotokana na JKT kugongeana pasi safi kibao kabla ya mpira kumkuta mfungaji. Hussein Bunu aliifungia JKT bao la pili dakika ya 50.
    Ligi hiyo inatarajiwa kuendelea kesho Jumapili kwa mchezi kati ya Villa Squad ya Dar es Salaam na Polisi ya Morogoro, kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
    Villa, inayofundishwa na Kenny Mwaisabula, iliyo katika nafasi ya pili kutoka mkiani, itakuwa inasaka ushindi kwa udi na uvumba, baada ya juzi kupoteza pambano lake dhidi ya Simba, licha ya kucheza soka ya kusisimua.
    Polisi Morogoro, wakiwa nafasi moja juu ya Villa, watakuwa wanataka kupigana kufa na kupona, kuhakikisha wanajiondoa katika ukanda wa kushuka daraja, huku nao wakiwa na kumbukumbu ya mechi yao ya mwisho, ambayo pia walijeruhiwa na Simba kwa bao 2-1 kwenye uwanja huo huo.
    Katika mchezo wa kwanza baina ya timu hizo uliopigwa kwenye uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro, vijana hao wa Dar es Salaam waliibuka na ushindi wa bao 1-0 liliwekwa kimiani na mkongwe Idd Moshi Shaaban.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: JKT RUVU YAIBWAGA AZAM DAR Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top