RAIS DK MWINYI AWAAHIDI SIMBA SC DOLA 100,000 WAKITWAA KOMBE LA CAF

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi amewaahidi Simba SC dola za Kimarekani 100,000, zaidi ya Sh. Milioni 250 iwapo watatwaa Kombe la Shirikisho Afrika kesho.
Simba SC watamenyana na RSB Berkane ya Morocco kesho kuanzia Saa 10:00 jioni Uwanja wa New Amaan Comolex, Zanzibar wakihitaji kupindua matokeo ya kufungwa 2-0 kwenye mchezo wa kwanza Jumamosi iliyopita nchini Morocco ili watwae taji hilo.
Na jioni ya leo Rais Mwinyi amewatembelea Simba SC kambini kwao na kuzungumza na wachezani na makocha pamoja na viongozi kuwapa motisha kuelekea Fainali hiyo ya kihistoria kesho.
“Nimetembelea kambi ya Timu ya Klabu ya Simba na kupata nafasi ya kuzungumza na Wachezaji, viongozi mbalimbali na benchi la ufundi kuelekea mchezo wa kesho wa fainali ya Kombe la Shirikisho Afrika utakaochezwa katika Uwanja wa New Amaan Complex dhidi ya Timu ya RS Berkane kutoka Morocco,” amesema Rais Mwinyi katika taarifa yake na kuongeza;
“Nimewaahidi Dola 100,000 za kimarekani iwapo Simba itashinda ubingwa wa Kombe la Shirikisho Afrika,”.
Mapema viongozi wa Simba walizuru Kaburi la Rais wa kwanza wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar Hayati Abeid Amaan Karume na kumuombea aendelee kupumzika kwa amani.
Hiyo ni baada ya jana pia kuzuru Kaburi la Rais wa zamani wa Zanzibar na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Ali Hassan Mwinyi.