SIMBA SC WAZURU KABURI LA HAYATI RAIS MWINYI, WATOA MISAADA KWA YATIMA ZANZIBAR
UONGOZI wa Simba SC leo umezuru katika kaburi la Hayati Ali Hassan Mwinyi, Rais wa zamani wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwenye Kijiji cha Mangapwani, Mkoa wa Kaskazini Unguja Wilaya ya Kaskazini B, Zanzibar na kumuombea dua aendelee kupumzika kwa Amani.
Hiyo ni moja ya matukio ya kijamii kuelekea mchezo wao wa marudiano wa Fainali ya Kombe la Shirikisho Afrika dhidi ya RSB Berkane Jumapili kuanzia Saa 10:00 jioni Uwanja wa New Amaan Complex, Zanzibar.
Aidha, katika hatua nyingine kwa kushirikiana na Mo Dewji Foundation, Simba SC pia imetembelea na kutoa misaada kwenye vituo viwili vya kutunza watoto yatima, Amani na Mountsuri.
Aliyewahi kuwa Kaimu Makamu wa Rais, Iddi Kajuna alitoa msaada binafasi katika kituo cha Mountsuri.
Baada ya kufungwa mabao 2-0 kwenye mchezo wa kwanza Jumamosi iliyopita Uwanja wa Manispaa ya Berkane mjini Berkane nchini Morocco – Simba SC inatakiwa kushinda 3-0 ili kutwaa taji hilo au ishinde 2-0 na bingwa apatikane kwa mikwaju ya penalti.
