BILA AZIZ KI WYDAD YACHAPWA 1-0 NA SEVILLA MECHI YA KIRAFIKI CASABLANCA
NYOTA mpya wa Wydad Athletic, Stephane Aziz Ki aliyesajiliwa kutoka Yanga ya Tanzania mwishoni mwa wiki leo hakuwepo hata benchi wakati timu hiyo ikichapwa 1-0 na Sevilla FC ya Hispania katika mechi ya kirafiki Uwanja wa Mohammed V mjini Casablanca.
Mechi hiyo ni sehemu ya maandalizi ya Wydad kwa ajili ya michuano ya Klabu Bingwa ya Dunia ya FIFA 2025 inayotarajiwa kufanyika nchini Marekani kuanzia Juni 15 hadi Julai 13.
Baada ya mechi dhidi ya Sevilla jana Casablanca – Wydad pia watacheza na FC Porto ya Ureno Jumapili kukamilisha mbili za kirafiki kabla ya Klabu Bingwa ya Dunia.
Wydad imeachana na aliyekuwa Kocha wake, Rhulani Mokwena wa Afrika Kusini baada ya kumaliza nafasi ya tatu kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya Morocco maarufu kama Botola Pro ikiwa na pointi 54, nyuma ya FAR Rabat iliyomaliza pointi 57 na mabingwa RSB Berkane waliomaliza na pointi 70 baada ya mechi 30 za msimu.
Wydad Athletic ambao sasa wapo chini ya Kocha wa nyumbani, Mohamed Amine Benhachem wamepangwa Kundi G katika Klabu Bingwa ya Dunia pamoja na Manchester City, wababe wa Italia Juventus, na Al Ain ya Falme za Kiarabu (UAE).
Mbali na Aziz Ki Wydad imeimarisha kikosi chake kuwa kuwasajili winga mkongwe, Nourredine Amrabat kutoka Hull City ya England na mshambuliaji Hamza Hanouri kutoka FUS Rabat.