TIMU ya Mamelodi Sundowns ya Afrika Kusini imefanikiwa kutwaa taji la Ligi ya Mabingwa Afrika licha ya sare ya kufungana bao 1-1 na wenyeji, AS FAR Rabat usiku huu Uwanja wa Prince Moulay Abdellah Jijini Rabat nchini Morocco.
Mabao yote kwenye mchezo huo yamefungwa na viungo, Mohamed Rabie Hrimat akianza kuifungia AS FAR Rabat bao la kuongoza dakika ya 40, kabla ya Teboho Michael Mokoena kuisawazishia Mamelodi Sundowns dakika ya 45’+7.
Kwa matokeo hayo, Mamelodi Sundowns inatwaa ubingwa wa Afrika kwa ushindi wa jumla wa 2-1 kufuatia kuichapa AS Forces Armées Royales de Rabat 1-0 kwenye mchezo wa kwanza Mei 17 bao la beki wa kushoto, Maphosa Aubrey „Postman“ Modiba dakika ya 37 Uwanja wa Loftus Versfeld Jijini Pretoria.
Hilo linakuwa taji la pili tu la Ligi ya Mabingwa wa Afrika kwa Masandawana baada ya mwaka 2016 walipoifunga Zamalek 3-1 kwenye fainali, wakishinda 3-0 nyumbani na kufungwa 1-0 ugenini.



.png)
0 comments:
Post a Comment