• HABARI MPYA

    Tuesday, September 01, 2020

    BAADA YA USAJILI, SASA TUNATAKA KUONA SOKA INACHEZWA UWANJANI

    Na Dominick Salamba, DAR ES SALAAM
    NIMEJIKUTA nakumbuka mbali ingawa si mbali sana ni enzi za utoto wangu kipindi cha rika letu wale wa umri wangu watakumbuka pia.
    Kipindi ambacho zilikiwa zikikaribia sikukuu iwe Eid, Krismasi,Pasaka na zingine unazozijua ilikuwa ni wakati wa sisi watoto kuwa kwenye presha kubwa tukiwaza Kama tutapata nguo za sikukuu,viatu na vitu vingine,na hata vilipopatikana basi uvijaribisha ndani kisha utunzwa kwa umakini mkubwa ili siku ya sikukuu husika watu tutoke kwa mbwembwe na madoido.
    Inapofika siku ya sikukuu ndipo mbivu na mbichi uonekana Kwani kunakuwa hakuna siri tena ubora halisi wa zile pamba zako pia uonekana kwa wengine Kwani ndio wakati wa kulinganisha na zile za wengine ndipo tulipogundua utofauti wa ulichonacho na wengine aisee ngoja tuishia hapa turudi kwenye mada yetu.

    Usajili tayari umekamilika kwa kila timu na kila timu imesajili kwa kadri ya uwezo wao na mahitaji pia,hivyo kilichobaki ni kuona thamani ya kile kilichosajiliwa,kuona ujuzi wa waalimu namna ambavyo wanaweza kutengeneza mseto mzuri Kati ya wale wa zamani na hawa wapya,kuona namna ambavyo timu zitarekebisha udhaifu wa msimu uliopita na kuboresha zaidi ule ubora waliokuwa nao msimu uliopita..
    Kwani dirisha la usajili limewekwa ili kuweza kutoa nafasi ya timu kujihimarisha kwa kadri ya mapungufu waliyonayo na si lazima usajili pia ukiona kikosi kipo imara unaweza kuendelea nacho..
    Lakini pia usajili unaofanyika ni lazima uwe unazingatia hali ya uchumi kwa ujumla mana kuna wakati unaweza kufanya usajili lakini baada ya muda hali ya uchumi ikatetereka na hapa ndipo linapokuja swala la umuhimu wa kuwekeza katika soka la vijana ili kuweza kuwapandisha ili kuja kuwa mbadala wa waliondoka kwa kuhitajiwa mahala pengine au walioachwa kwa kupoteza ubora wao hivyo kutumia hazina ya vijana ili kuja kuongeza kitu tena kwa gharama ndogo lakini kupata ubora unaokidhi mahitaji ya timu husika.
    Hapa kwetu imekuwa ni Kama  desturi kuandaa timu ya msimu hadi msimu bado hatupo vizuri kwenye kuhakikisha tunakuwa na timu moja ambayo itasimama walao kwa misimu mitano mpaka Saba jambo ambalo linasaidia sana kulinda uchumi wa klabu tofauti na ilivyo sasa ambapo kila msimu unakuwa ni msimu mpya siyo tu wa ligi bali hata vikosi ubadilika kabisa nusu ya wachezaji uondoka na wengine kuachwa.
    Kwa namna hii huwezi kuona mwendelezo unaostahili wa wachezaji wetu ni vigumu kuona matatazo ya msingi katika kikosi lakini pia falsafa ya timu kuingia hasa kwa wachezaji wa timu husika..
    Ifike mahali timu ziamue kuwa na malengo ya muda mrefu ili tuone ushindani wa kweli,timu ziache kufanya usajili Kama fasheni za nguo za misimu na sikukuu.
    Tayari tumeona usajili wa msimu ujao tarehe 6 mwezi huu wa Tisa ligi inaanza wote tumeridhika na sajili zetu Sasa ni wakati wa kuona mpira uwanjani,tuone msimu wa tofauti msimu ambao tutashuhudia kelele za mpira mzuri zaidi uwanjani kuliko kelele kulalamika za mashabiki,viongozi na wasemaji wa timu zetu.
    Ni wakati wa kuona kila watu wakitumia weledi wao katika maeneo yao kwa maana viongozi watimize majukumu yao,wachezaji na mabenchi ya ufundi yafanye kazi kwelikweli,maamuzi yawe yenye kuridhidha,mashabiki tujitokeze kwa wingi viwanjani ukiwa na jezi ya timu yako Kwani tambua kuwa wewe shabiki una nafasi kubwa ya kuifanya timu yako ipige hatua.
    Kwa namna ambavyo dirisha la usajili lilivyofana basi ni matumaini yangu kuwa hata viwanja vitatamalaki mashabiki wengi ili kuifanya Tanzania kuwa nchi ya kuigwa katika soka la Afrika kutokana na mapenzi makubwa tuliyonayo katika soka letu la nyumbani.
    Na zile timu ambazo zimepanda daraja ni wakati wa kutuonesha kuwa wamepanda kwa kuwa walistahili kupanda Huku wakazi wa mikoa husika wakiziunga mkono kwa Hali na Mali katika ushiriki wao wa Ligi kuu soka Tanzania bara..
    (Dominick Salamba ni mchambuzi wa soka anapatikana pia kupitia katika Akaunti zake za Twitter: _@dominicksalamb1 na Instagram: _@dominicksalamba au namba ya simu  +255713942770)
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: BAADA YA USAJILI, SASA TUNATAKA KUONA SOKA INACHEZWA UWANJANI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top