• HABARI MPYA

    Wednesday, February 05, 2020

    WAZIRI MWAKYEMBE AIPA BMT SIKU TATU KUMPA MAJIBU JUU YA MAREFA KULALAMIKIWA NCHINI

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    WAZIRI wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dk. Harrison Mwakyembe amelitaka Baraza la Michezo (BMT) kumpa majibu ya malalamiko ya maamuzi katika ligi mbalimbali nchini ndani ya siku tatu kuanzia kesho Februari 6, 2020.
    Waziri Mwakyembe amechukua hatua hiyo kufuatia kuwepo kwa mfululizo wa matukio ya uonevu baina ya vilabu hususani maamuzi ya viwanjani hasa katika Ligi Kuu.
    “Wizara imeendelea kupokea tuhuma mbalimbali/uonevu katika mashindano ya ligi mbalimbali za mpira wa miguu yanayoendelea nchini, lakini wadau hawaoni hatua zikichukuliwa mara moja na kupatiwa mrejesho,” imesema taarifa ya Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Eleuteri Mangi leo.
    Tamko la Waziri Mwakyembe linakuja wakati tayari Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Wallace Karia ameitaka Kamati ya Waamuzi kukutana na Bodi ya Ligi ili kutathmini mwenendo wa uchezeshaji wa Waamuzi wa Ligi Kuu.
    Rais Karia amesema kwamba katika kikao hicho watakuwepo baadhi ya Maafisa wa TFF kutoka Idara ya Mashindano.
    Rais Karia ametaka kikao hicho baina ya pande hizo tatu kitazame kwa kina kuhusu mwenendo wa uchezeshaji wa marefa ili kuondoa malalamiko katika eneo hilo ambalo ni muhimu katika maendeleo ya mpira wa miguu nchini.
    Na hayo yanafuatia mfululizo wa matukio ya marefa ya kutoa maamuzi mabovo kwenye Ligi Kuu, zaidi yakionekana kuwanufaisha mabingwa watetezi, Simba SC.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: WAZIRI MWAKYEMBE AIPA BMT SIKU TATU KUMPA MAJIBU JUU YA MAREFA KULALAMIKIWA NCHINI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top