• HABARI MPYA

    Thursday, February 06, 2020

    MWAMUZI ‘ALIYEIPA’ USHINDI SIMBA SC DHIDI YA NAMUNGO FC TAIFA AFUNGIWA MIAKA MITATU

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    KAMATI ya Uendeshaji na Usimamizi wa Ligi ya Bodi ya Ligi Kuu Tanzania Bara (TPLB) imemfungia miaka mitatu mwamuzi msaidizi namba mbili, Kassim Safisha aliyechezesha mechi ya Ligi Kuu baina ya mabingwa watetezi, Simba SC dhidi ya Namungo FC ya Ruangwa mkoani Lindi Januari 29, mwaka huu.
    Simba SC iliibuka na ushindi wa 3-2 Uwanja wa Taifa na Safisha anaponzwa na bao la tatu la washindi lililofungwa na mshambuliaji wa kimataifa wa Rwanda, Meddie Kagere akiwa ameotea.
    Taarifa ya Bodi baada ya kikao chake cha Februari 3, kupitia mwenendo na matukio mbalimbali ya Ligi imesema kwamba Safisha anaadhbiwa kwa kushindwa kutafsiri sheria ya kuotea katika mechi hiyo na adhabu yake imetolewa kwa mujibu wa Kanuni namba 39 (1) (a) ya Ligi Kuu kuhusu Udhibiti wa Waamuzi.

    Mwamuzi Meshack Suda ameandikiwa barua ya kukumbushwa kufanya majukumu yake kwa umakini zaidi baada ya mapungufu yake katika mechi iliyomalizika kwa sare ya 1-1 baina ya Azam FC na Mtibwa Sugar Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. iliyochezwa Januari 30,2020 katika uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam.
    Kamishina wa mchezo huo, Abdallah Zongo ameondolewa kwenye orodha ya Makamishina kwa kosa la kutoa taarifa yenye mapungufu na Adhabu hii ni kwa kuzingatia Kanuni namba 40 (1) kuhusu Udhibiti Kamishina
    Katika Ligi Daraja la Kwanza: Kiongozi wa Friends Rangers, Heri Chibakasa ‘Heri Mzozo’ amepelekwa Kamati ya Nidhamu ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kwa kosa la kupigana na mashabiki wa wapinzani wao Dodoma FC.
    Kwenye Ligi Daraja la Pili; Mwamuzi Salum Mkole amefungiwa miezi mitatu kwa kosa la kuonyesha udhaifu katika usahihi wa kutoa kadi katika mechi baina ya wenyeji Dar City na African Sports ya Tanga  Januari 31 Uwanja wa Karume, Dar es Salaam Februari 1 Uwanja wa Karume jijini Dar es salaam. 
    Dar City ilishinda 1-0 na taarifa imesema kwamba adhabu hiyo imetolewa kwa mujibu wa Kanuni namba 39 (1) kuhusu Udhibiti wa Waamuzi.
    Naye mchezaji wa African Sports, Rajabu Kipango amepelekwa Kamati ya Nidhamu ya TFF kwa kosa la kumpiga mchezaji wa Dar City.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MWAMUZI ‘ALIYEIPA’ USHINDI SIMBA SC DHIDI YA NAMUNGO FC TAIFA AFUNGIWA MIAKA MITATU Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top