• HABARI MPYA

    Monday, November 04, 2019

    YANGA SC YAPIGWA 3-0 CAIRO NA PYRAMIDS FC NA KUTUPWA NJE KOMBE LA SHIRIKISHO LA AFRIKA

    Na Mwandishi Wetu, CAIRO
    SAFARI ya Tanzania katika michuano ya klabu barani Afrika imekamilika usiku wa kuamkia leo baada ya Yanga SC kutolewa na wenyeji, Pyramids FC kufuatia kuchapwa 3-0 Uwanja wa Jeshi la Anga wa Juni 30 mjini Cairo katika mchezo wa marudiano wa mchujo wa kuwania kuingia hatua ya makundi ya Kombe la Shirikisho.
    Yanga sasa inatolewa kwa kipigo cha jumla cha 5-1 kufuatia kufungwa 2-1 kwenye mchezo wa kwanza mjini Mwanza Jumapili wiki iliyopita.
    Yanga SC ndiyo klabu pekee ya Tanzania iliyokuwa imesalia kwenye michuano ya Afrika baada ya Simba SC, KMC na Azam FC kwa upande wa Tanzania Bara na Malindi na KMKM za Zanzibar kutolewa mapema mwaka huu. 
    Mabao ya Pyramids katika mchezo wa jana yalifungwa na Mburkina Faso, Eric Traore dakika ya 28, Mohamed Farouk dakika ya 80 na Abdullah Elsaid dakika ya 90 na ushei.

    Pyramids FC inaungana na, El Masry ya Misri pia, Enyimba, Rangers za Nigeria, RS Berkane, HUSA za Morocco, Nouadhibou ya Mauritania, Horoya ya Guinea, Zanaco ya Zambia, San Pedro ya Ivory Coast, El Nasr ya Libya, Djoliba ya Mali, Motema Pembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), Bidvest Wits ya Afrika Kusini na Paradou ya Algeria kuingia hatua ya makundi.
    Kikosi cha Pyramids FC jana kilikuwa; Ahmed Elshanawy, Ragab Bakar, Ahmed Manous, OMaer Gaber, Abdallah Bakry, Mohamed Hamdy, Mohamedy Fathy, Dounga, Abdallah Elsaid, Eric Traore na Mohamed Farouq.
    Yanga SC; Farouk Shikhalo, Juma Abdul, Ally Mtoni, Ally Ally, Lamine Moro, Abdulaziz Makame, Deus Kaseke, Papy Kabamba Tshishimbi, Sadney Urikhob, Juma Balinya na Balama Mapinduzi.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: YANGA SC YAPIGWA 3-0 CAIRO NA PYRAMIDS FC NA KUTUPWA NJE KOMBE LA SHIRIKISHO LA AFRIKA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top