• HABARI MPYA

    Monday, October 07, 2019

    SAMATTA AENDELEA NA UNAHODHA KRC GENK IKIENDELEZA WIMBI LA USHINDI LIGI YA UBELGIJI

    Na Mwandishi Wetu, GENK
    MSHAMBULIAJI wa kimataifa wa Tanzania, Mbwana Ally Samatta kwa mara nyingine tena jana alikuwa Nahodha wa klabu yake, KRC Genk ikiibuka na ushindi wa 2-1 dhidi ya Royal Excel Mouscron katika mchezo wa Ligi Daraja la Kwanza A Ubelgiji Uwanja wa Luminus Arena mjini Genk.
    Katika mchezo wa jana, mabao ya Genk yote yalifungwa na mshambuliaji mpya, Mnigeria Ebere Paul Onuachu aliyesajiliwa kutoka Midtjylland ya Denmark dakika ya 75 na 90 na ushei, wakati la Royal Excel Mouscron lilifungwa na mshambuliaji wa kimataifa wa Ghana, Jonah Osabutey dakika ya 49.
    Sasa KRC Genk imefikisha 16 baada ya kucheza mechi tisa, ingawa inaendelea kukamata nafasi ya sita, ikizidiwa pointi saba na vinara, Club Brugge wanaofuatiwa na Standard Liege yenye pointi 20 za mechi  10, Gent pointi 17 za mechi tisa sawa na Antwerp na Mechelen ambayo imecheza mechi 10.

    Mbwana Samatta ameendelea na Unahodha KRC Genk ikiendeleza wimbi la ushindi Ubelgiji

    Kwa ujumla, Samatta jana alicheza mechi 167 kwenye mashindano yote tangu ajiunge na KRC Genk Januari mwaka 2016 akitokea TP Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) akiwa amefunga mabao 68 jumla.
    Katika ligi ya Ubelgiji pekee amecheza mechi 131 na kufunga mabao 52, kwenye Kombe la Ubelgiji amecheza mechi tisa na kufunga mabao mawili, katika Super Cup mechi moja, Ligi ya Mabingwa Ulaya mechi mbili na bao moja na Europa League mechi 24 na mabao 14.
    Kikosi cha KRC Genk kilikuwa: Coucke, Maehle, Cuesta, Lucumi, Uronen, Berge, Hrosovsky/Heynen dk72, Hagi/Onuachu dk61, Ito, Bongonda/Odey dk90+3 na Samatta.
    RE Mouscron: Butez, De Medina, Hocko, Olinga/Spahiu dk72, Boya, Queiros, Garcia, Van Durmen/Mohamed dk81, Godeau, Wimmer na Osabutey/Buatu dk90+4.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SAMATTA AENDELEA NA UNAHODHA KRC GENK IKIENDELEZA WIMBI LA USHINDI LIGI YA UBELGIJI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top