• HABARI MPYA

    Wednesday, May 01, 2019

    YAHYA ZAYD ACHEZA SAA NZIMA LAKINI ISMAILIA YAPIGWA 1-0 NA HARAS EL HODOOD

    Na Mwandishi Wetu, CAIRO
    MSHAMBULIAJI chipukizi wa kimataifa wa Tanzania, Yahya Zayd usiku wa jana amecheza kwa karibu saa nzima timu yake, Ismailia ikichapwa 1-0 na Haras El Hodood katika mchezo wa Ligi Kuu ya Misri Uwanja wa Gehaz El Reyada mjini Cairo.
    Pamoja na kuwa wenyeji, Ismailia hawakufurukuta wakiadhibiwa na Haras El Hodood na wapinzani wenzao wa zamani wa Simba SC ya Dar es Salaam kwa bao pekee la mshambuliaji kinda wa miaka 21 kutoka Nigeria, Edu Moses dakika ya 28.
    Zayd aliyejiunga na Ismailia msimu huu kutoka Azam FC ya nyumbani, Tanzania alitolewa dakika ya 58, nafasi yake ikichukuliwa na Karim Bambo.

    Yahya Zayd usiku wa jana amecheza kwa karibu saa nzima Ismailia ikichapwa 1-0 na Haras El Hodood katika Ligi Kuu ya Misri

    Hata hivyo, mabadiliko hayo hayakuweza kuinusuru Ismailia kupoteza 10 katika msimu huu, hivyo kubaki na pointi zake 37 baada ya kucheza mechi 29 na sasa ipo nafasi ya saba.
    Baada ya ushindi wa jana, Haras El Hodood sasa wanasogea nafasi ya 15 katika Ligi Kuu inayoshirikisha timu 18 wakifikisha pointi 32 katika mchezo wa 30.
    Wachezaji wengine wa Kitanzania wanaocheza Misri, viungo Himid Mao timu yake Petrojet FC ni ya 14 ikiwa na pointi 34 za mechi 30 na Shiza Kichuya wa ENPPI anayoichezea kwa mkopo kutoka Phraco FC ipo nafasi ya 16 ikiwa na pointi 30 za mechi 29.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: YAHYA ZAYD ACHEZA SAA NZIMA LAKINI ISMAILIA YAPIGWA 1-0 NA HARAS EL HODOOD Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top