• HABARI MPYA

    Tuesday, April 09, 2019

    TWIGA STARS YAPIGWA 1-0 NA DRC NA KUTUPWA NJE MAPEMA MBIO ZA OLIMPIKI YA 2020

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    TANZANIA imefungwa 1-0 na wenyeji, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) katika mchezo wa marudiano Raundi ya Kwanza kuwania tiketi ya kucheza Fainali za Soka za Wanawake Olimpiki 2020 mjini Tokyo, Japan jioni ya leo Uwanja wa Martyrs de la Pentecote mjini Kinshasa.
    Kwa matokeo hayo, Tanzania inatolewa kwa jumla ya mabao 3-2 baada ya kulazimishwa sare ya 2-2 Ijumaa iliyopita katika mchezo wa kwanza Uwanja wa Taifa mjini Dar es Salaam.
    Bao lililoizamisha Twiga Stars leo limefungwa na Grace Balongo Mfwambo aliyepiga kona iliyoingia moja kwa moja nyavuni dakika ya 45 ya mchezio huo na DRC itamenyana na Equatorial Guinea katika Raundi ya Pili kati ya tano za mchujo wa kuwania tiketi ya Olimpiki 2020.

    Twiga Stars watajutia nafasi walizopoteza katika mchezo wa kwanza nyumbani, wakilazimishwa sare ya 2-2 mabao yao yakifungwa na Deonisia Daniel dakika ya 46 na Asha Rashid ‘Mwalala’ dakika ya 79, wakati ya DRC yalifungwa na Marilene Yav dakika ya 10 na Grace Balongo dakika ya 53.
    Lakini siku hiyo Twiga Stars ilipoteza nafasi nzuri ya kuufunga kwa penalti baada ya beki Fatuma Khatib ‘Foe’, mzazi mwenzake kiungo mshambuliaji wa timu ya taifa ya wanaume, Simon Happygod Msuva shuti lake kupanguliwa na kipa wa DRC, Fideline Mudimbi dakika ya 27.
    Penalti hiyo ilitolewa baada ya Monica Kanyinda wa DRC kamuangusha Deonisia Daniel wa Twiga Stars kwenye boksi.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: TWIGA STARS YAPIGWA 1-0 NA DRC NA KUTUPWA NJE MAPEMA MBIO ZA OLIMPIKI YA 2020 Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top