• HABARI MPYA

    Wednesday, January 09, 2019

    YANGA SC YAAGA KOMBE LA MAPINDUZI KWA USHINDI WA 3-1 DHIDI YA JAMHURI

    Na Mwandishi Wetu, ZANZIBAR
    YANGA SC imehitimisha mechi zake za Kundi B Kombe la Mapinduzi kwa ushindi wa mabao 3-1 dhidi ya Jamhuri FC ya Pemba jioni ya leo Uwanja wa Amaan, Zanzibar.
    Ushindi huo unaifanya Yanga SC ifikishe pointi sita baada ya mechi zake zote nne ikishinda mbili na kufungwa mbili, ingawa hazitoshi kuwafanya wabaki kwenye michuano hiyo na kesho watarejea Dar es Salaam.  
    Jamhuri ambayo nayo inaaga ikiziacha Malindi na Azam zikienda Nusu Fainali, ilikuwa ya kwanza kupata bao leo dakika ya tat utu kupitia kwa mchezaji wake, Hajji Ramadhani aliyemalizia pasi ya Husse Rajab.

    Yanga wakasawazisha bao hilo dakika ya 20 kupitia kwa mchezaji wake, Faraji Kilaza aliyemalizia pasi ya kiungo Pius Buswita kabla ya Shaaban Mohammed kuifungia timu hiyo bao la pili dakika ya 28.
    Buswita akawainua tena vitini mashabiki wa Yanga SC kwa kufunga bao la tatu dakika ya 32 baada ya kazi nzuri ya kiungo mwenzake, Gustafa Simon.
    Yanga ikapata pigo dakika ya 43 baada ya mfungaji wake wa bao la kwanza Faraji Kilaza kuumia na kushindwa kuendelea na mchezo, nafasi yake ikichukuliwa na Cheda Hussein.
    Kipindi cha pili pamoja na Yanga SC kuendelea kutawala mchezo, lakini haikuweza kupata mabao zaidi na kuvuna ushindi wa 3-1.
    Mchezo wa mwisho wa Kundi B unafuatia usiku huu kuanzia Saa 2:15 usiku kati ya Azam FC na Malindi SC hapo hapo Uwanja wa Amaan. 
    Kikosi cha Yanga SC kilikuwa: Ibrahim Hamid, Yassin Saleh, Gustafa Simon, Cleophace Sospeter, Said Juma, Maka Edward, Shaaban Mohammed/Erick Msangati dk83, Pius Buswita, Matheo Anthony/Salim Mkama dk89, Faraji Kilaza/Cheda Hussein dk43 na Deus Kaseke/Ramadhan Mrisho dk75.
    Jamhuri FC: Khalid Bakar, Masoud Said/Khamis Ali dk46, Kambu Zuberi, Emmanuel Joseph, Yussuf Makame, Mohammed Mgau, Mbarouk Ali/Humoud Abrahman dk53, Hajji Ramadhani, Suleiman Nassor/Samir Seif dk77, Khalfan Abdallah na Hussein Rajab/Juma Thausi dk60.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: YANGA SC YAAGA KOMBE LA MAPINDUZI KWA USHINDI WA 3-1 DHIDI YA JAMHURI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top