• HABARI MPYA

    Sunday, January 13, 2019

    NI AZAM FC TENA MABINGWA MAPINDUZI KWA MARA YA TANO, YA TATU MFULULIZO

    Na Mwandishi Wetu, PEMBA
    TIMU ya Azam FC imefanikiwa kutwaa Kombe la Mapinduzi baada ya ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Simba SC, zote za Dar es Salaam katika mchezo uliofanyika Uwanja wa Gombani, kisiwani Pemba jioni ya leo.
    Pamoja na Kombe, Azam FC, timu inayomilikiwa na bilionea Alhaj Sheikh Said Salim Awadh Bakhresa imezawadiwa fedha taslimu Sh. Milioni 15, wakati Simba SC wamepata Sh. 10,000.
    Shujaa wa Azam FC leo ni mshambuliaji Mzambia, Obrey Chirwa aliyeifungia timu hiyo bao la ushindi dakika ya 82 kwa kichwa akimalizia krosi ya winga Mghana, Enock Atta-Agyei.
    Mgeni rasmi, Makamu wa Rais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Balozi Seif Ali iddi alimkabidhi Kombe Nahodha wa Azam FC, Aggrey Morris

    Hiyo inakuwa mara ya tano na mara ya tatu mfululizo kwa Azam FC kutwaa taji hilo tangu michuano hiyo ianzishwe mwaka 2007, baada ya awali kulibeba katika miaka ya 2012, 2013, 2017 na 2018.
    Na hii ni mara ya tatu wanaifunga Simba SC kwenye fainali ya michuano hiyo baada ya 2012 na 2017, wakati mwaka 2013 waliifunga Tusker FC ya Kenya na 2018 waliifunga URA FC ya Uganda.
    Katika mchezo huo uliochezeshwa na refa Mfaume Ali, kiungo Mudathir Yahya Abbas alianza kuifungia Azam FC dakika ya 44 akimalizia pasi ya winga Mghana, Enock Atta-Agyei.
    Beki wa kati, Yussuf Mlipili akaisawazishia Simba SC dakika ya 61 akimalizia vizuri kona iliyochongwa na kiungo Shiza Ramadhani Kichuya.
    Mgeni rasmi, Makamu wa Rais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Balozi Seif Ali iddi alimkabidhi Kombe Nahodha wa Azam FC, Aggrey Morris baada ya mchezo huo na wachezaji wa timu hiyo wakamwagika uwanjani kusherehekea.
    Kikosi cha Azam FC kilikuwa: Razak Abalora, Nicolas Wadada, Bruce Kangwa, Aggrey Morris, Yakub Mohammed, Stephan Kingue, Salum Abubakar ‘Sure Boy’, Mudathir Yahya, Obrey Chirwa/Donald Ngoma dk44, Tafadzwa Kutinyu/Ramadhani Singano ‘Messi’ dk24 na Enock Atta-Agyei.
    Simba: Ally Salim, Zana Coulibally, Asante Kwasi, Yussuf Mlipili, Paul Bukaba, Mohammed ‘Mo’ Ibrahim, Shiza Kichuya, Haruna Niyonzima, Adam Salamba/Michael Andrew dk90, Abdul Suleiman/ Shaaban Salum dk56 na Rashid Juma/ Dickson Mhilu dk84.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: NI AZAM FC TENA MABINGWA MAPINDUZI KWA MARA YA TANO, YA TATU MFULULIZO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top