• HABARI MPYA

    Monday, December 03, 2018

    SAMATTA ACHEZA KWA SAA MOJA KRC GENK YAICHAPA ANDERLECHT 1-0 LIGI YA UBELGIJI NA KUZIDI KUJIACHIA KILELENI

    Na Mwandishi Wetu, BRUSELLS 
    MSHAMBULIAJI wa kimataifa wa Tanzania, Mbwana Ally Samatta jana amecheza kwa saa moja na ushei kabla ya kutolewa, timu yake, KRC Genk ikiibuka na ushindi wa 1-0 ugenini dhidi ya RSC Anderlecht katika mchezo wa Ligi Daraja la Kwanza A Ubelgiji Uwanja wa Constant Vanden Stock mjini Brusells.
    Samatta aliondolewa uwanjani dakika ya 64 kumpisha mshambuliaji Mbelgiji, Zinho Gano na wakati huo KRC Genk ilikuwa bado haijapata bao lake.
    Na ni kiungo Mspaniola, Alejandro Pozuelo Melero aliyefunga bao pekee la Genk jana dakika ya 71 akimalizia pasi ya kiungo mwenzake, kinda wa umri wa miaka 20, Mnorway Sander Berge.
    Mbwana Samatta akiuwahi mpira dhidi ya mchezaji wa RSC Anderlecht jana
    Mbwana Samatta (kulia) akifuatilia maamuzi ya refa Bram Van Driessche baada ya mchezaji wa Anderlecht kuanguka
    Wachezaji wa Genk wakimpongeza mwenzao, Alejandro Pozuelo baada ya kufunga bao pekee jana dakika ya 71 

    Kwa ushindi huo, Genk iliyo chini ya kocha Mbelgiji, Philippe Clement sasa inafikisha pointi 38 baada ya kucheza mechi 17 ikiendelea kuongoza Ligi ya Ubelgiji kwa tofauti ya pointi nne na Club Brugge walio nafasi ya pili.
    Anderlecht inabaki nafasi ya nne na pointi zake 30 sawa na Sint-Truiden iliyo nafasi ya tano, nyuma ya Antwerp yenye pointi 32 baada ya wote kucheza mechi 17 pia.
    Samatta jana amecheza mechi ya 132 katika mashindano yote tangu amejiunga na KRC Genk Januari mwaka 2016 akitokea TP Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) akiwa jumla ya mabao 51.
    Katika Ligi ya Ubelgiji pekee amefikisha mechi 102 na kufunga mabao 36, Kombe la Ubelgiji mechi nane na mabao mawili na Europa League mechi 22 mabao 14.
    Kikosi cha RSC Anderlecht kilikuwa; Didillon, Lawrence, Makarenko, Najar, Santini, Kums, Amuzu/Saif dk87, Bornauw, Sambi/Verschaeren dk74, Saelemaekers na Bakkali/Doku dk64.
    KRC Genk; Vukovic, Maehle, Aidoo, Dewaest, Uronen, Berge, Malinovskyi, Pozuelo/Seck dk84, Ndongala, Trossard na Samatta/Gano dk63.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SAMATTA ACHEZA KWA SAA MOJA KRC GENK YAICHAPA ANDERLECHT 1-0 LIGI YA UBELGIJI NA KUZIDI KUJIACHIA KILELENI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top