• HABARI MPYA

    Monday, December 03, 2018

    RAJA WATWAA KOMBE LA SHIRIKISHO LICHA YA KUPIGWA 3-1 NA AS VITA

    TIMU ya Raja Casablanca ya Morocco imefanikiwa kutwaa Kombe la Shirikisho Afrika nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) jana licha ya kichapo cha mabao 3-1 kwenye mchezo wa marudiano dhidi ya wenyeji, AS Vita Club.
    Kwa matokeo hayo, Raja wanabeba taji hilo kwa ushindi wa jumla wa 4-3 baada ya awali kushinda 4-0 kwenye mchezo wa kwanza mjini Casablanca. 
    Na ushindi huo unamaanisha vigogo hao wa Morocco wamemaliza ukame wa miaka 15 wa kusbiri taji la Afrika, tangu walipotwaa Kombe la CAF mwaka 2003.

    Hilo linakuwa taji la sita la Shirikisho la Soka Afrika (CAF) kwa Wamorocco hao, ambao tayari wametwaa mataji mengine kama Ligi ya Mabingwa mara tatu na Super Cup mara moja. 
    Abdelilah Hafidi aliifungia Raja bao la kuongoza dakika ya 21 kwa ustadi wa hali ya juu mbele ya mashabiki 80,000 waliojitokeza Uwanja wa Martyrs mjini Kinshasa.
    Bao lilimaanisha Vita Club ambao taji lao pekee la CAF walilichukua miaka 45 iliyopita, walihitaji kufunga mabao matano ili wabebe taji hilo.
    Jean-Marc Makusu, aliyeanzishwa baada ya kupona maumivu aliyoyapata kwenye mchezo wa kwanza akaisawazishia Vita kwa shuti la mpira wa adhabu dakika ya 45.
    Mtokea benchi, Mukoko Batezadio akaifungia bao la pili Vita Club dakika ya 71 na Fabrice Ngoma akafunga la tatu dakika ya 74.
    Lakini Raja ikasimama imara na kuwadhibiti wenyeji wasipate mabao zaidi na mechi hivyo kufanikiwa kutwaa taji hilo la CAF.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: RAJA WATWAA KOMBE LA SHIRIKISHO LICHA YA KUPIGWA 3-1 NA AS VITA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top