• HABARI MPYA

    Monday, December 03, 2018

    KENYA YAFUZU AFCON BAADA YA CAF KUIENGUA SIERRA LEONE

    SHIRIKISHO la Soka Afrika (CAF) limeamua kuiondoa Sierra Leone kwenye michuano ya kuwania tiketi ya kucheza Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika mwaka 2019.
    Taarifa ya CAF leo, imesema kwamba maamuzi hayo yamefanyika katika kikao cha Kamati Kuu ya shirikisho hilo Ijumaa mjini Accra, Ghana.
    Na CAF imechukua hatua hiyo baada ya Tume ya Kuzuia Rushwa ya nchi hiyo kumuondoa madarakani Rais wa Shirikisho la Soka Sierra Leone (SLFA), Isha Johansen na Katibu Mkuu wake, Christopher Kamara Oktoba mwaka huu.
    Pamoja na kuiondoa Sierra Leone, CAF pia imefuta matokeo ya mechi zake zote za Kundi F ambalo sasa linabakiwa na timu za Kenya, Ghana na Ethiopia.

    Na moja kwa moja Ghana na Kenya zinafuzu moja kwa moja kwenye fainali hizo – Harambee Stars wakiwa timu ya pili ya Afrika Mashariki kufuzu baada ya Uganda, wakati Tanzania itaangalia mustakabali wake Machi mwakani L. 
    Kenya inayoongoza Kundi F kwa pointi zake saba, ikifuatiwa na Ghana pointi sita, inafuzu kwa mara ya kwanza tangu mwaka 2004 nchini Tunisia na mara ya tano jumla baada ya 1972, 1988, 1990 na 1992. Ethiopia yenye pointi moja tu ikiwa imekamilisha mechi zake, inaishia hapa. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: KENYA YAFUZU AFCON BAADA YA CAF KUIENGUA SIERRA LEONE Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top