• HABARI MPYA

    Saturday, October 06, 2018

    SIMBA SC YAAMUA KUACHANA NA MASOUD JUMA KWA SABABU HAELEWANI NA ‘BOSI’ WAKE MBELGIJI AUSSEMS

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    HATIMAYE klabu ya Simba SC imetoa tamko la kuachana na Kocha Msaidizi, Mrundi Masoud Juma baada ya takriban mwaka mmoja wa kuwa na klabu.
    Kaimu Rais wa Simba SC, Salim Abdallah ‘Try Again’ ametoa tamko hilo leo asubuhi katika kipindi cha Kurasa za Mwisho cha Azam Sports 2 baada ya kuulizwa juu ya hatima ya mchezaji huyo wa zamani wa kimataifa wa Burundi.
    Try Again akasema kwamba kutokana na Juma kushindwa kuelewana na kocha mkuu, Mbelgiji Patrick Aussems wamelazimika kuamua moja kwa manufaa ya klabu.
    Salim amesema uongozi wa Simba umekuwa ukijitahidi kusuluhisha na kuwaweka sawa makocha hao, lakini imeshindikana, hivyo ndani ya siku chache zijazo utatangaza rasmi kuachana na kocha huyo raia wa Burundi.
    “Kuna kutoelewana kati ya mwalimu na msaidizi wake, sisi kama viongozi tumekuwa tukijaribu kuwaweka sawa, lakini kwa jinsi hali inavyokwenda, haielekei muelekeo mzuri, kwa hiyo ni vigumu kusema kwa sasa. Kadri dakika na saa zinavyokwenda tutayatolea maelezo,” amesema Abdallah.
    Historia ya Masoud Juma Simba SC inaeleeka kufungwa wakati wowote
    Juma aliwasili nchini Oktoba 19, mwaka mwaka jana akitokea Rwanda alipokuwa anafundisha timu ya Rayon Sport, kuchukua nafasi ya aliyekuwa kocha Msaidizi wa Simba, Mganda Jackson Mayanja aliyeng’atuka.
    Alianza kazi chini ya Mcameroon, Joseph Omog lakini akafukuzwa, akaletewa Mfaransa, Pierre Lechantre aliyemalizia msimu na timu ikatwaa ubingwa kabla ya kufukuzwa – na Mbelgiji, Patrick J Aussems anakuwa kocha wa tatu mkuu wa Mrundi huyo.
    Lakini wakati Lechantre anaondoka alimtupia lawama Juma akidai alimsaliti na inaelezwa alitafuta nafasi ya kuzungumza na Aussems kumueleza juu ya kocha huyo wa Burundi. 
    Bado uongozi wa Simba SC unasubiriwa kutoa hatma ya Masoud ambaye tangu Oktoba mwaka jana amekuwa Kaimu Kocha Mkuu mara mbili na timu ikaendelea kufanya vizuri.
    Dalili za Masoud kuondolewa Simba SC zilianza kuonekana katikati ya mwezi uliopita baada ya kuachwa kwenye safari ya mechi za mikoani, Mtwara, Mwanza na Shinyanga ambako timu ilishinda mechi moja tu 3-1 dhidi ya Mwadui FC, nyingine mbili ikitoa sare ya 0-0 na Ndanda FC na kufungwa 1-0 na Mbao FC.    
    Wakati huo majibu ya uongozi juu ya Masoud kutosafiri na timu yalikuwa ni ana shughuli nyingine za klabu alizopangiwa kufanya ikiwemo kuwachunguza wapinzani wa Simba SC katika mechi zijazo.
    Na alipoibuka benchi wakati wa mechi dhidi ya Yanga iliyomalizika kwa sare ya 0-0 Jumapili iliyopita Uwanja wa Taifa mjini Dar es Salaam imani ikarejea kwamba atabaki – lakini leo Abdallah ameweka bayana mustakabali wa mwalimu huyo.  
    Masoud alikuwa Msaidizi wa Omog katika mechi 10 tu, timu ikishinda mechi sita, sare tatu na kufungwa moja kwa penalti 4-3 na Green Warriors Mwenge katika hatua za awali za Kombe la Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), maarufu kama Azam Sports Federation Cup (ASFC) Uwanja wa Azam Complex, Chamazi mjini Dar es Salaam.
    Baada ya kutolewa na Green Warriors katika Kombe la TFF, Omog akafukuzwa na Masoud akakaimu Ukoha Mkuu, timu ikicheza mechi saba, kushinda nne, sare moja na kufungwa mbili kabla ya ujio wa Kocha mpya Mkuu, Mfaransa Pierre Lechantre.
    Na wakati wa Lechantre Simba ilicheza mechi 22 na kushinda 14, sare saba na kufungwa moja kabla ya Mfaransa huyo kuondolewa na Masoud tena kuwa Kaimu Kocha Mkuu akiiongoza timu katika mechi nane na kushinda tano, kufungwa mbili na sare moja.
    Na wakati huu wa Aussems, pamoja na zile mechi tatu ambazo hakusafiri, SImba imecheza jumla ya mechi 13, ikishinda saba, sare tano na kufungwa moja. Je, hiyo ndiyo itahitimisha safari Masuod Juma Simba SC – au, atapata nusura tena? Ni jambo la kusubiri na kuona. 
    Masoud Juma (katikati) akiwa na Joseph Omog (kushoto), bosi wake wa kwanza Simba SC. Kulia ni kocha wa makipa, Muharammi Mohammed 'Shilton'  

    REKODI YA MASUDI JUMA SIMBA
    (KOCHA MSAIDIZI WA OMOG)
    1. Simba 4-0 Njombe Mji (Ligi Kuu Uhuru)
    2. Simba 1-1 Yanga (Ligi Kuu Uhuru)
    3. Simba 1-0 Mbeya City (Ligi Kuu Sokoine)
    4. Simba 0-0 Nyundo FC (Kirafiki Mpanda)
    5. Simba 3-1 Kangesa FC (Kirafiki Sumbawanga)
    6. Simba 1-0 Tanzania Prisons (Ligi Kuu Sokoine)
    7. Simba 1-1 Lipuli FC (Ligi Kuu Uhuru)
    8. Simba 3-1 KMC (Kirafiki Chamazi, Omog alikuwa likizo Cameroon)
    9. Simba 4-0 African Lyon (Kirafiki Chamazi, Omog alikuwa likizo Cameroon)
    10. Simba 1-1 (Penalti 3-4) Green Warriors (Kombe la TFF Chamazi)
    Masoud Juma (kushoto) hapa akiwa Kaimu Kocha Mkuu wa Simba SC baada ya Pierre Lechantre kuondoka 

    KAIMU KOCHA MKUU
    1. Simba 2-0 Ndanda FC (Ligi Kuu Nangwanda)
    2. Simba 1-1 Mwenge FC (Kombe la Mapinduzi Zanzibar)
    3. Simba 3-1 Jamhuri FC (Kombe la Mapinduzi Zanzibar)
    4. Simba 0-1 Azam FC (Kombe la Mapinduzi Zanzibar)
    5. Simba 0-1 URA FC (Kombe la Mapinduzi Zanzibar)
    6. Simba 4-0 Singida United  (Ligi Kuu Uhuru)
    7. Simba 2-0 Kagera Sugar  (Ligi Kuu Kaitaba)

    KOCHA MSAIDIZI WA PIERRE LECHANTRE
    1. Simba 4-0 Maji Maji FC (Ligi Kuu Taifa)
    2. Simba 3-0 Ruvu Shooting FC (Ligi Kuu Uhuru)
    3. Simba 1-0 Azam FC (Ligi Kuu Taifa)
    4. Simba 4-0 Gendarmerie Tnare  (Kombe la Shirikisho Taifa)
    5. Simba 2-2 Mwadui FC (Ligi Kuu Kambarage)
    6. Simba 1-0 Gendarmerie Tnare  (Kombe la Shirikisho Djibouti)
    7. Simba 5-0 Mbao FC (Ligi Kuu Taifa)
    8. Simba 3-3 Stand United (Ligi Kuu Taifa)
    9. Simba 2-2 Al Masry  (Kombe la Shirikisho Taifa)
    10. Simba 0-0 Al Masry  (Kombe la Shirikisho Port Said)
    11. Simba 2-0 Njombe Mji FC (Ligi Kuu Taifa Njombe)
    12. Simba SC 1-0 Mtibwa Sugar (Ligi Kuu Taifa) 
    13. Simba 3-1 Mbeya City  (Ligi Kuu Taifa)
    14. Simba 2-0 Tanzania Prisons  (Ligi Kuu Taifa)
    15. Simba 1-1 Lipuli FC  (Ligi Kuu Samora)
    16. Simba 1-0 Yanga SC  (Ligi Kuu Taifa)
    17. Simba 1-0 Ndanda FC  (Ligi Kuu Taifa)
    18. Simba 1-0 Singida United  (Ligi Kuu Namfua)
    19. Simba 2-2 Dodoma Combine  (Kirafiki Jamhuri)
    20. Simba 0-1 Kagera Sugar  (Ligi Kuu Taifa mbele ya Rais Magufuli)
    21. Simba 1-1 Maji Maji  (Ligi Kuu Songea)
    22. Simba 0-0 (3-2 Penalti) Kariobangi Sharks  (SportPesa SuperCup Nakuru)
    Masoud Juma (kushoto) akiwa na Pierre Lechanre mazoezini

    KAIMU KOCHA MKUU
    1. Simba 0-0 (5-4 Penalti) Kakamega Homeboys (SportPesa SuperCup Nakuru)
    2. Simba 0-2 Gor Mahia (SportPesa SuperCup Nakuru)
    3. Simba SC 4-0 Dakadaha FC (Kombe la Kagame Taifa Kundi C)
    4. Simba SC 2-1 APR (Kombe la Kagame Taifa Kundi C)
    5. Simba SC 1-1 Singida United (Kombe la Kagame Taifa Kundi C)
    6. Simba SC 1-0 AS Ports (Robo Fainali Kombe la Kagame Taifa)
    7. Simba SC 1-0 JKU (Nusu Fainali Kombe la Kagame Taifa)
    8. Simba SC 1-2 Azam FC (Fainali Kombe la Kagame Taifa)
    Masoud Juma (katikati) akiwa na 'mbaya wake', Patrick J Aussems (kushoto). Kulia ni kocha wa mazoezi ya viungo, Mtunisia Adel Zrane

    KOCHA MSAIDIZI WA PATRICK J AUSSEMS)
    1. Simba SC 1-1 F.C.E KSAIFA (ya Palestina, kirafiki ziara ya Uturuki)
    2. Simba SC 3-1 MC Oujder (ya Morocco, Kirafiki ziara ya Uturuki)
    3. Simba SC1-1 Asante Kotoko (ya Ghana, Kirafiki Taifa)
    4. Simba SC 0-0 Namungo FC (Kirafiki Uwanja wa Majaliwa, Ruangwa, Lindi)
    5. Simba SC 2-1 Arusha United (Kirafiki Uwanja wa S.A. Abeid, Arusha)
    6. Simba SC 2-1 Mtibwa Sugar (Ngao ya Jamii Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza)
    7. Simba SC 1-0 Tanzania Prisons (Ligi Kuu Taifa)
    8. Simba SC 2-0 Mbeya City (Ligi Kuu Taifa)
    9. Simba SC 4-2 AFC Leopards (Kirafiki Taifa)
    10. Simba SC 0-0 Ndanda FC (Ligi Kuu Mtwara, alibaki Dar)
    11. Simba SC 0-1 Mbao FC (Ligi Kuu Mwanza, alibaki Dar)
    12. Simba SC 3-1 Mwadui FC (Ligi Kuu Shinyanga, alibaki Dar)
    13. Simba SC 0-0 Yanga SC (Ligi Kuu Taifa)
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SIMBA SC YAAMUA KUACHANA NA MASOUD JUMA KWA SABABU HAELEWANI NA ‘BOSI’ WAKE MBELGIJI AUSSEMS Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top