• HABARI MPYA

    Thursday, October 04, 2018

    MWINYI ZAHERA NA AMRI SAID ‘STAM’ WAWAFUNIKA MAKOCHA WAZUNGU PLUIJM NA AUSSEMS LIGI KUU

    Na Lulu Ringo, DAR ES SALAAM
    KAMATI ya tuzo za Wachezaji Bora wa Ligi Kuu Tanzania Bara, imeanzisha tuzo ya mpya ya Kocha Bora wa mwezi itakayokuwa inatolewa kila mwezi kwa lengo la kutambua mchango wa makocha katika ligi hiyo.
    Akizungumza na Waandishi wa Habari leo mjini Dar es Salaam, Afisa Habari wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Clifford Mario Ndimbo amesema kwamba tayari Kamati ya tuzo hizo imeandaa vigezo mbalimbali ambavyo vitatumika kumpata kocha bora wa mwezi.
    Pamoja na hayo, TFF leo imewataja makocha bora wawili wa kwanza kwa miezi Agosti na Septemba baada ya kila mmoja kuwashinda wapinzani wake wawili alioingia nao fainali ya tuzo hizo.
    Kwa mwezi Agosti kocha Bora ni Amri Said ‘Stam’ wa Mbao FC ya mjini Mwanza aliyeshinda tuzo hiyo mbele ya makocha wa kigeni watupu, Mholanzi Hans van der Pluijm wa Azam FC na Mbelgiji Patrick Aussems wa Simba SC.
    Mwinyi Zahera (katikati) akiwa na Msaidizi wake, Noel Mwandila (kulia) na Hafidh Saleh (kushoto) 

    Amri, beki wa zamani wa Maji Maji ya Songea na Simba SC ya Dar es Salaam ameshinda tuzo hiyo baada ya kuiwezesha timu yake kushinda mechi mbili na kutoa sare moja, hivyo kuongoza Ligi Kuu kwa kipindi hicho.
    Pluijm, kocha wa zamani wa Yanga SC na Singida United naye kwa upande wake aliisaidia Azam FC kushinda michezo miwili kama ilivyokua kwa Aussems wa Simba SC..
    Kwa Septemba, Kamati hiyo imemchagua Mwinyi Zahera wa Yanga SC kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) kuwa Kocha Bora kwa mwezi huo baada ya kuwashinda Zubery Katwila wa Mtibwa Sugar na Bakari Shime wa JKT Tanzania.
    Zahera ameshinda tuzo hiyo baada ya kuiwezesha Yanga kushinda michezo mitatu na sare moja katika mwezi huo, hivyo kushika nafasi ya pili kwenye msimamo wa Ligi Kuu kwa mwezi huo, wakati Katwila aliiwezesha Mtibwa Sugar kushinda michezo mitatu, sare moja na kufungwa mmoja hivyo kushika nafasi ya tatu na Shime aliiwezesha JKT Tanzania kushinda michezo miwili na kutoa sare miwili.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MWINYI ZAHERA NA AMRI SAID ‘STAM’ WAWAFUNIKA MAKOCHA WAZUNGU PLUIJM NA AUSSEMS LIGI KUU Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top