• HABARI MPYA

    Sunday, September 16, 2018

    SAMATTA ALIMWA KADI YA NJANO KRC GENK YAWABABUA ANDERLECHT 1-0 LIGI YA UBELGIJI

    Na Mwandishi Wetu, GENK
    MSHAMBULIAJI wa kimataifa wa Tanzania, Mbwana Ally Samatta jana usiku ameonyeshwa kadi ya njano timu yake, KRC Genk ikiibuka na ushindi wa 1-0 RSC Anderlecht katika mchezo wa Ligi Daraja la Kwanza A Ubelgiji.
    Katika mchezo huo uliofanyika Uwanja wa Luminus Arena mjini Genk, Samatta alionyeshwa kadi ya njano dakika ya mwisho kabisa, ya tano ya muda wa nyongeza baada ya kutimia dakika 90 za kawaida za mchezo. 
    Na hiyo ilikuwa kadi ya nane ya njano jumla anaonyeshwa katika muda wote wa kuichezea Genk tangu amejiunga nayo Januari mwaka 2016 akitokea Tout Puissant Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) na bahati nzuri kwake hajawahi kuonyeshwa kadi nyekundu kihistoria.
    Mbwana Samatta akipambana katika mechi ya jana kabla ya kulimwa kadi ya njano dakika ya mwisho

    Bao pekee la mchezo wa jana lilifungwa na beki Mbelgiji, Sebastien Dewaest dakika ya 49 akimalizia pasi ya kiungo Mspaniola, Alejandro Pozuelo Melero na ushindi huo unawapeleka nafasi ya pili kwenye msimamo wa Ligi wakifikisha pointi 17 baada ya kucheza mechi saba, nyuma ya vinara, Club Brugge wenye pointi mbili zaidi.
    Genk wanafuatiwa na Gent wenye pointi 13 sawa na Anderlecht, wakati Standard Liege inakamilisha tano bora kwa pointi zake 12, wote wakiwa wamecheza mechi saba.  
    Nahodha huyo wa Tanzania, Samatta mwenye umri wa miaka 25 sasa, jana amefikisha mechi 92 za kuichezea Genk, kati ya hizo 60 ameanza na 32 ametokea benchi akiwa ameifungia timu hiyo jumla ya mabao 29 kwenye mashindano pekee – yaani bila kuhusisha michezo ya kirafiki. 
    Kikosi cha KRC Genk jana kilikuwa: Vukovic, Maehle, Lucumi, Dewaest, Nastic, Berge, Heynen/Seck dk85, Pozuelo/Paintsil dk93, Ndongala/Aidoo dk82, Trossard na Samatta.
    RSC Anderlecht: Didillon, Milic, Sanneh, Najar, Appiah/Saief dk64, Makarenko, Trebel, Saelemaekers, Gerkens/Musona dk64, Dimata/Bakkali dk75 na Santini.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SAMATTA ALIMWA KADI YA NJANO KRC GENK YAWABABUA ANDERLECHT 1-0 LIGI YA UBELGIJI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top