• HABARI MPYA

    Friday, September 07, 2018

    NDUDA AREJESHWA KIKOSINI SIMBA SC BAADA YA KUMALIZA TOFAUTI ZAKE NA VIONGOZI

    Na Lulu Ringo, DAR ES SALAAM
    KIPA Said Mohammed Nduda amerejeshwa kwenye kikosi cha Simba SC kufuatia kumalizwa kwa tofauti baina yake na uongozi.
    Akizungumza na Bin Zubeiry Sports – Online leo jioni mjini Dar es Salaam, Nduda amesema kwamba tayari ameanza kufanya mazoezi na timu yake hiyo, Simba SC kuelekea mchezo wa mechi ya kirafiki dhidi ya AFC Leopards ya Kenya kesho.
    “Nimefanya mazoezi na timu kuelekea mechi itakayochezwa kesho Uwanja wa Taifa na hiyo baada ya kumaliza tofauti kati yangu na uongozi wa Simba,”amesema kipa huyo wa zamani wa Mtibwa Sugar na Yanga.
    Ndunda amesema kwamba baada ya kuzikwa kwa tofauti hizo anaelekeza nguvu zake kwenye bidii ya mazoezi ili awe fiti kumvutia kocha mpya, Mbelgiji Patrick J Aussems ampe nafasi.

    Said Mohammed Nduda amerejeshwa kikosini Simba SC kufuatia kumaliza tofauti zake na uongozi

    Ndunda amesema anakabiliwa na changamoto ya kuwa vizuri ili apewe nafasi na kujenga mazingira ya kupewa mkataba mpya atakapomaliza huu wa sasa Mei mwakani.
    “Mimi klabu ya Simba napita kama njia, lakini kwa wakati huu nitaipa klabu yangu kipaumbele hadi pale mkataba wangu utakapofikia ukingoni,” ameongeza.
    Ndunda alisajiliwa Simba SC Julai mwaka jana baada ya kung’ara kwenye michuano ya COSAFA Castle nchini Afrika Kusini akiiwezesha Tanzania kumaliza nafasi ya tatu na kushinda tuzo ya Kipa Bora wa michuano hiyo.
    Lakini akawa ana bahati mbaya baada ya kuumia goti mazoezi katika kambi ya visiwani Zanzibar Agosti, timu ikijiandaa na mchezo wa Ngao ya Jamii dhidi ya mahasimu wa jadi, Yanga na kujikuta anakuwa nje kwa msimu wote kufuatia kwenda kutibiwa India.
    Mwishoni mwa msimu alirejea na kupata fursa ya kudaka katika mechi chache za kujipima, lakini ajabu mwanzoni mwa msimu huu, Simba SC ikatangaza kumtoa kwa mkopo kufuatia kusajiliwa kwa kipa mwingine mzoefu, Deo Munishi ‘Dida’.
    Sasa Simba SC inakuwa na makipa wane, pamoja na Dida na Nduda, wengine ni ‘Tanzania One’, Aishi Manula na Abdul Salim aliyepandishwa kutoka timu ya vijana.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: NDUDA AREJESHWA KIKOSINI SIMBA SC BAADA YA KUMALIZA TOFAUTI ZAKE NA VIONGOZI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top