• HABARI MPYA

    Tuesday, September 04, 2018

    MWENYEKITI WA ZAMANI WA TAIFA STARS, MZEE MENGI ATEULIWA KUWA MLEZI WA SERENGETI BOYS

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    SHIRIKISHO la Soka Tanzania (TFF)leo limemtangaza Mwenyekiti wa Makampuni ya IPP,  Reginald Mengi kuwa mlezi wa timu ya taifa ya vijana chini ya umri wa miaka 17, Serengeti Boys.
    Taarifa ya TFF leo imesema kwamba Mengi amekuwa akiifuatilia kwa karibu timu hiyo na amekuwa mmoja wa wadau wakubwa wa soka la vijana. 
    "Amekuwa ni mpenda maendeleo ya mpira wa Miguu hususani soka la Vijana na amekuwa shabiki mkubwa wa Serengeti Boys,".

    Mzee Reginald Mengi ameteuliwa kuwa mlezi wa Serengeti Boys

    "TFF tunaamini tutashirikiana vizuri na Ndugu Mengi katika maendeleo na ustawi wa soka la Vijana.  Mengi ni mwanamichezo ambaye hakika amekuwa mstari wa mbele katika kukuza na kuendeleza soka la Vijana," amesema. 
    Taarifa hiyo imesema kwamba mara kadhaa Mengi amekuwa akiwasiliana na TFF kufuatilia maendeleo ya timu ya Taifa ya U17 kwenye mashindano mbalimbali. 
    "TFF tunafarijika kwa Ndugu Mengi kukubali kuwa mlezi wa timu hii ya Serengeti Boys na tunaamini kwa pamoja tutaifanya timu hii kuwa msingi mzuri katika maendeleo ya ustawi wa soka la Vijana,".
    Mengi ni mwana michezo kihistoria, ambaye anafahamika kama mpenzi wa klabu ya Yanga, ambaye mwaka 1995 aliishauri klabu hiyo kuwa Kampuni na kuachana na desturi ya kutegemea wafadhili wa Kiasia.
    Lakini pia, Mzee Mengi amewahi kuwa Mwenyekiti wa Kamati ya timu ya taifa ya wakubwa, Taifa Stars ambayo wakati mwingine iliwajibika kusaidia timu za vijana pia.  
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MWENYEKITI WA ZAMANI WA TAIFA STARS, MZEE MENGI ATEULIWA KUWA MLEZI WA SERENGETI BOYS Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top