• HABARI MPYA

    Wednesday, September 19, 2018

    KITENGE AAHIDI HAT TRICK ZAIDI PAMOJA NA KUNYIMWA MPIRA BAADA YA KUWAPIGA YANGA

    Na Lulu Ringo, DAR ES SALAAM
    MSHAMBULIAJI  wa Stand United, Alex Kitenge raia wa Burundi ameahidi kufunga ‘hat trick’ zaidi japokuwa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) limemnyima mpira wake baada ya kuifunga Yanga mabao matatu katika mchezo wa Ligi Kuu uliochezwa Semptemba 16 Taifa, Dar es Salaam.
    Juzi wakati timu ya Stand ikikubali kichapo cha mabao 4-3 Mrundi huyu ndie mchezaji alieipatia timu yake mabao hayo matatu ‘hat trick’ lakini hadi kufikia leo hii cha kustaajabisha hajakabidhiwa mpira huo kama ilivyo desturi ya mpira mchezaji anaefunga magoli matatu hukabidhiwa mpira uliotumika katika mchezo huo

    Alex Kitenge alikabidhiwa mpira halafu akanyang'anywa Jumapili baada ya kupiga hat trick dhidi ya Yanga

    Akizungumza na Bin Zubeiry Sports - Online mchezaji huyo amesema kilichotokea kwake ni jambo la kawaida na haliwezi kumtoa mchezoni isipokuwa atajitahidi kufunga hat trick nyingine nyingi.
    “Hili suala nalichukulia kawaida, haliwezi kunitoa mchezoni, siwezi kusema kwa kuwa wameninyima mpira nitoke mchezoni, hapana nitapigana. Mungu anisaidie nifunge nyingine, jambo hili haliwezi ni kunisumbua wala kuniletea matatizo”, amesema Alex Kitenge, mshambuliaji huyo wa Stand United mwenye asili ya Kongo.
    Hata hivyo Alex ameeleza kuwa chanzo cha kutopewa mpira huo na TFF ni upungufu wa mipira inayotumika katika michezo ya Ligi kuu.  
    “Waliniambia kuwa kuna mipira 15 inayotumika kuchezea Ligi, hivyo mimi nisubiri watanitafutia mpira mwingine mpya na sijui hata ni lini watanipa,”alisema mchezaji huyo. 
    Kufuatia kuchelewa kwa makabidhiano ya mpira huo, Alex ameamua kutofuatilia tena mpira huo na kilichobaki ni yeye kuhakikisha anafanya kazi yake vizuri.
    “Sijui ni lini watanipa mpira wangu mimi nimeamua kutouulizia tena, acha nifanye kazi yangu kwa usalama maana hata nikisema niufatilie ntamuuliza nani ?”. Amesema Mrundi huyo.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: KITENGE AAHIDI HAT TRICK ZAIDI PAMOJA NA KUNYIMWA MPIRA BAADA YA KUWAPIGA YANGA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top