• HABARI MPYA

    Sunday, September 09, 2018

    BONDIA MTANZANIA HASSAN MWAKINYO AMTWANGA MUINGEREZA KWA TKO BIRMINGHAM

    Na Mwandishi Wetu, BIRMINGHAM
    BONDIA Hassan Mwakinyo wa Tanzania jana amefanikiwa kushinda kwa Technical Knockout (TKO) sekunde ya 45 raundi ya pili dhidi ya Muingereza, Sam Eggington Uwanja wa Arena Birmingham, zamani Barclaycard Arena mjini Birmingham, England.
    Katika pambano hilo lisilo la ubingwa uzito wa Light Middle, Mwakinyo alimzidi kabisa mpinzani wake tangu mwanzo kabla ya kummaliza katika raundi ya pili kuelekea pambano kuu jana kati ya Muingereza, Amir Khan na Samuel Vargas Colombia anayeishi Canada.
    Khan aliyeshinda kwa pointi za majaji wote, alimuangusha Vargas mwanzoni mwa raundi ya pili, naye akaangushwa mwishoni mwa raundi hiyo wote waliinuka haraka kuendelea hadi kumaliza raundi.

    Hassan Mwakinyo baada ya kumshinda kwa TKO Muingereza, Sam Eggington Uwanja wa Arena Birmingham jana
    Khan aliyemuangusha Vargas na raundi ya tatu pia pamoja na kumjeruhi pua, kwa ushindi huo anaweza kupigana na Manny Pacquiao au Kell Brook.
    Na Mwakinyo baaada ya ushindi huo wa jana atapanda tena ulingoni Oktoba 20, kuzipiga na mwenyeji Wanik Awdijan ukumbi wa Alex Sportcentrum mjini Nuremberg, Ujerumani katika pambano la kuwania taji la vijana la IBF uzito wa Middle.
    Pambano la jana lilikuwa la tatu Mwakinyo anapoigana nje ya Tanzania akiwashinda kwa mara ya pili baada ya kumshinda pia kwa TKO Anthony Jarmann wa Namibia Agosti 8, mwaka jana ukumbi wa Grand Palm Hotel mjini Gaborone nchini Botswana.
    Desemba 2, mwaka jana Mwakinyo alipoteza kwa pointi mbele ya mwenyeji, Lendrush Akopian ukumbi wa Krylia Sovetov mjini Moscow, Urusi.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: BONDIA MTANZANIA HASSAN MWAKINYO AMTWANGA MUINGEREZA KWA TKO BIRMINGHAM Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top