• HABARI MPYA

    Friday, August 03, 2018

    YANGA SC YAAMUA KUSHIRIKI NA LIGI YA WANAWAKE...WANAANZIA DARAJA LA KWANZA

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    BAADA ya kushiriki soka ya wanaume kwa muda mrefu wa mafanikio, hatimaye klabu ya Yanga ya Dar es Salaam imeamua kushirki na Ligi ya Wanawake. 
    Mabingwa hao wa kihistoria wa Ligi Kuu ya wanaume, sasa wanaamua kuhamishia utemi wao kwenye soka ya wanawake pia, ambao timu yao itaitwa Yanga Princess.
    Yanga SC ni miongoni mwa timu 18 zilizothibitisha kushiriki Ligi Daraja la Kwanza kwa Wanawake itakayoanza Septemba 6,2018.
    Afisa Habari na Mawasiliano wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Clifford Mario Ndimbo amesema kwamba Ligi hiyo itachezwa katika mfumo wa makundi na timu 2 zitapanda daraja wakati zitakazobaki zitasalia kwenye Daraja la Kwanza. 

    Mbali na Yanga SC, timu nyingine zilizothibitisha kushiriki Ligi hiyo ni TSC ya Mwanza, Mapinduzi Princess ya Tanga, Migoli Queens ya Iringa, Ruangwa Queens ya Lindi, Viva FC ya Mtwara, Singida Warriors ya Singida. 
    Nyingine ni Katoro Queens ya Geita, Victoria Queens ya Kagera, Tanzanite FC ya Arusha, Mapinduzi Queens ya Njombe, Allans Queens ya Dodoma, Manonga Queens ya Tabora, Abeehe Bha Kyela FC ya Mbeya, Kisarawe Queens ya Pwani, Testimony ya Kilimanjaro, Mbinga Queens ya Ruvuma na Kizuka Sekondari ya Morogoro.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: YANGA SC YAAMUA KUSHIRIKI NA LIGI YA WANAWAKE...WANAANZIA DARAJA LA KWANZA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top