• HABARI MPYA

    Saturday, August 04, 2018

    OKWI AFUNGA MAWILI SIMBA SC YASHINDA 3-1 DHIDI YA TIMU YA PALESTINA MECHI YA KIRAFIKI UTURUKI

    Na Mwandishi Wetu, ISTANBUL
    TIMU ya Simba SC imeibuka na ushindi mzuri wa mabao 3-1 dhidi ya timu ya F.C.E Ksaifa ya Palestina katika mchezo wa kirafiki uliofanyika mjini Istanbul, Uturuki leo.
    Na shujaa wa Simba SC alikuwa ni mshambuliaji wa kimataifa wa Uganda, Emmanuel Okwi aliyefunga mabao mawili huku bao lingine likifungwa na mshambuliaji Mnyarwanda, Meddie Kagere. 
    Okwi aliwasabahi Wapelestina dakika ya 16 tu kwa bao la kwanza kabla ya kuongeza la pili dakika ya 50 na dakika nne baadaye Nader Alkrinaui akawafungia F.C.E Ksaifa.
    Mnyarwanda mwenye asili ya Uganda, Mohammed ‘Meddie’ Kagere akatokea benchi kuchukua nafasi ya Okwi na kuifungia Simba SC bao la tatu dakika ya 87.

    Emmanuel Okwi amefunga Simba SC ikishinda 3-1 dhidi ya F.C.E Ksaifa ya Palestina

    Huo ulikuwa mchezo wa pili wa Simba SC wa kujipima nguvu katika ziara yake ya Uturuki, baada ya kutoka sare ya 1-1 na MC Oujder ya Morocco katika mchezo wa kwanza Jumatano. 
    Kikosi cha Simba SC kimeweka kambi katika hoteli ya Reen Park & Resorts mjini Istanbul, kikifanya mazoezi yake katika moja ya viwanja saba vilivyoizunguka hoteli hiyo.
    Mabingwa hao wa Tanzania wanatarajiwa kurejea nchini Agosti 5 tayari kwa tamasha la kila mwaka la klabu, Simba Day ambalo hufanyika Agosti 8 Uwanja wa Taifa mjini Dar es Salaam na mgeni rasmi atakuwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa.
    Na siku hiyo, Simba SC itamenyana na mabingwa mara mbili wa Afrika, Asante Kotoko ya Ghana waliobeba taji hilo enzi za Klabu Bingwa Afrika katika miaka ya 1970 na 1983. 
    Kikosi cha Simba kilichocheza leo ni; Aishi Manula/Deo Munishi 'Dida', Shomari Kapombe, Mohammed Hussein ‘Tshabalala’/Asante Kwasi, Pascal Wawa, Erasto Nyoni/Paul Bukaba, Jonas Mkude/Said Ndemla, James Kotei/Muzamil Yassin, Cletus Chama/Hassan Dilunga, Shiza Kichuya/Mohammed 'Mo' Ibrahim, Emmanuel Okwi/Meddie Kagere na Adam Salamba/Mohammwd Rashid.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: OKWI AFUNGA MAWILI SIMBA SC YASHINDA 3-1 DHIDI YA TIMU YA PALESTINA MECHI YA KIRAFIKI UTURUKI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top